Rwanda katika Umoja wa Mataifa (UN): Usawa wa chanjo, ujumuishwaji, amani, na usawa wa kijinsia yaongoza masuala tunayoyapa kipaumbele

Get monthly
e-newsletter

Rwanda katika Umoja wa Mataifa (UN): Usawa wa chanjo, ujumuishwaji, amani, na usawa wa kijinsia yaongoza masuala tunayoyapa kipaumbele

— Balozi Valentine Rugwabiza, Mjumbe wa Kudumu wa Rwanda katika Umoja wa Mataifa.
Zipporah Musau
Afrika Upya: 
7 April 2021
Balozi Valentine Rugwabiza (kushoto) na Bi. Amina J. Mohammed ni Naibu Katibu Mkuu Umoja wa Mataifa
Balozi wa Rwanda Umoja wa Mataifa
Balozi Valentine Rugwabiza (kushoto) na Bi. Amina J. Mohammed ni Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika sherehe ya miaka 25 ya uhuru wa Rwanda

Balozi Valentine Rugwabiza kutoka Rwanda ni kati ya wajumbe wachache wa kudumu wanawake wa mataifa yao katika UN jijini New York. Katika msururu wa AfrikaUpya wa kuangazia wajumbe wanawake wanaowakilisha mataifa yao katika makao makuu ya UN, alizungumza naye Zipporah Musau kuhusu masuala anayoyapa kipaumbele, changamoto kufikia sasa na sababu zake kupigania Wajumbe wa Kudumu wanawake zaidi. Hapa kuna madondoo.

Ambassador Valentine Rugwabiza
Balozi Valentine Rugwabiza

AfrikaUpya: Hebu tuanze na safari yako katika wadhifa huu. Je, imekuwaje na unaweza kutaja maeneo yapi matatu ya ufanisi wako?

Balozi Rugwabiza: Asante, kwa fursa ya kufanya mazungumzo haya. Twajisikia nyumbani na AfrikaUpya.

Nimekuwa nikifanya kazi kwa zaidi kidogo ya miaka 30 sasa. Huo ni muda mrefu sana lakini katika Afrika, watu wanajivunia umri mpevu na umuhimu wake kuhusiana na tajriba pamoja na busara. Sehemu kubwa ya taaluma yangu imegawika katika sekta ya kibinafsi na utumishi wa umma – katika taifa langu na kama mtumishi wa umma wa kimataifa.

Nilianza taaluma yangu katika sekta ya kibinafsi ambako nilihudumu kwa takriban miaka 10, kisha nikaanzisha kampuni nchini Rwanda, ambayo nilisimamia kibia kwa pamoja na dadangu. Nilipanga kisha nikaanzisha muungano wa wanawake wajasiriamali nchini Rwanda. Aidha mimi ni mwanachama mwanzilishi wa Muungano wa Sekta ya Kibinafsi Nchini Rwanda. Hata hivyo, ushawishi na nafasi ya wanawake ilikuwa inakosa pale. Wanawake walishiriki katika biashara, hata katika mazingira yetu maalumu na yenye changamoto baada ya 1994, ila nafasi yao haikujtokeza katika usimamizi wa muungano huo katika ngazi zote. Kwa hivyo, tulipanga kuwa na uwakilishi wa wanawake.

Kisha nikapewa fursa ya kuiwakilisha Rwanda katika UN jijini Geneva kama Mjumbe wa Kudumu na Balozi. Niliyatekeleza haya kwa miaka mitatu kisha nikateuliwa kama Naibu Mkrugenzi Mkuu wa Shirika la Biashara Duniani (WTO), na nikawa mwanamke wa kwanza katika wadhifa huo. Kwa hivyo, unaweza kutafakari jinsi nilivyo na furaha sasa, kwa kuwa tuna mwanamke wa kwanza Mkurugenzi wa WTO - Dkt. Ngozi Okonjo-Iweala. 

Kutoka hapo, nilirejea Rwanda ambako nilichaguliwa kama Waziri wa Uwekezaji, na baadaye Waziri wa Masuala ya Jumuiya ya Afrika Mashariki. Ni kutoka hapo ambapo niliteuliwa katika wadhifa wangu wa sasa ambapo nimekuwa kwa miaka minne iliyopita.  

Unaweza kusema sifa kuu ya safari hii ni gani?

Katika nyanja zote za safari yangu – iwe ni katika sekta ya kibinafsi, kama mtuimishi wa umma wa kimataifa, au katika kiwango cha kitaifa – kilichonipa msukumo zaidi ni kuwa na ujumuishwaji. Ninaamini sana ujumuishwaji na ninafahamu kwamba mfumo, au taifa, lisilo na ujumuishwaji haliwezi kuendelezwa. Na ninatumai kwamba hili ni moja kati ya mafunzo tunayojifundisha kutokana na janga tandavu la COVID-19. Mtu anastahili kujiuliza, ni kwa nini mataifa tajiri yaliyo na raslimali nyingi ajabu yamewapoteza watu wake wengi? Hili linatokana na sababu moja tu – kutengwa na ukosefu wa usawa. Hili halihusu utajiri, wala raslimali chache, au uwezo mdogo, wa kuwatunza raia wake. Uwezo upo, ila baadhi ya watu wametengwa kimuundo na kitaasisi. Unapokuwa na mfumo uliojengwa kwa msingi wa kutengwa, pindi unapokabiliwa na changamoto ya kimataifa,ukosefu huo wa usawa hudhihirika na kuwekwa wazi.

Kwa hivyo, kwangu mimi, limekuwa suala la ujumuishwaji, haswa wa wanawake na wa Waafrika. Ni ujumuishwaji wa masuala yanayopewa kipaumbele, mambo mbalimbali yanayowashughulisha watu, na mitazamo tofautitofauti. Iwapo mitazamo yako binafsi haizingatiwi, basi matokeo ya kimataifa au ya kikanda hayatakunufaisha.

Ujumuishwaji unastahili kuanzia katika hatua za mwanzo. Haiwezekani kwamba tufanye kila kitu – upangaji, mikakati, hata tukubaliane kuhusu raslimali mbalimbali na njia za kuitekeleza mikakati hiyo – na pindi hayo yote yanapokuwa tayari, kisha tunawaalike Waafrika fulani katika meza duara. Huo si ujumuishwaji, ni kujifanya.

Ni ujumuishwaji wa vijana pia. Na simaanishi kwamba haya yatatokea bila gharama. Kuna njia isiyo ya busara ya kuwatenga vijana kote ulimwenguni, kama mahitaji ya tajriba. Bila shaka uwekezaji katika kuwafundisha na kuwatayarisha kunahitaji juhudi na wakati. Iwapo hatutawajumuisha vijana, tusipowapa mafundisho na kuhakikisha kwamba hawapewi tu majukwaa ya kujifundisha, bali pia wanafahamu namna ya kufanya michango yao itambuliwe, basi kimsingi u peke yako. Kufikia wakati unapoondoka ofisini, unaweza kuwa umekuwa na taaluma bora, ndio, bali katika mkabala wa mabadiliko ya kimfumo, hapana kubwa utakalokuwa umelitimiza.

Ni mambo yapi matatu makuu unayoweza kusema umeyatimiza kama Mjumbe wa Kudumu wa Rwanda hapa New York?

Rwanda ni miongoni mwa mataifa yanayochangia idadi kubwa ya wanajeshi walinda usalama wa UN. Kwa hakika tu miongoni mwa mataifa ya kwanza matatu yanayochangia wanajeshi, huku takribani wanajeshi wetu wa kiume na wa kike takriban 6,000 wakiwa wametumwa katika jumbe za kulinda amani.

Hili linadhihirisha kwamba ulinzi wa usalama, amani na usalama ni muhimu sana kwetu, kwa kuwa linahusiana na historia yetu. Katika wakati wetu wa uhitaji mkuu [wakati wa vita vya kimbari vya 1994 dhidi ya Watutsi nchini Rwanda], tuliwachwa peke na jamii ya kimataifa, ujumbe wa kulinda amani uliokuwa nchini Rwanda wakati huo uliagizwa na Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuondoka nchini.

Ninastahili kutaja hapa kwamba, licha ya maagizo hayo, kikosi kimoja kiliamua kusalia nchini – cha Waghana. Hatutalisahau hilo, haijalishi ni baada ya vizazi vingapi. Kwao maisha yetu yalikuwa na thamani. Hawakuzuia mauaji, bali waliyaokoa maisha ya maelfu kadhaa ya watu.

Aidha, marehemu Kapten Mbaye Diagne, mlinda amani wa Senegal, aliamua kutoondoka na akafariki katika harakati za kuokoa maisha. Hatukuuona utu kutoka kwa wale waliokuwa na jukumu la kudumisha amani na usalama. La, tulishuhudia utu kutoka kwa Waafrika wenzetu, wakiyahatarisha maisha yao. Kwa hivyo, sasa tunajua – katika mioyo yetu, katika fikra zetu, sisi sote – ni Afrika haswa tunayostahili kulinda. Tunastahili kulindana. Kwa hivyo, kwetu sisi, kuhakikisha kwamba kuna amani na usalama katika Afrika ni kitu ambacho tumewekeza ndani na tunachangia, bila kujali udogo wake.

Tumechangia pia katika kuimarisha dhana ya ulinzi wa raia. Tumelifanya hili kuwa suala la kawaida kidogo kupitia kwa kile tunachokiita  Kigali Principles on Protection of Civilians (Kanuni za Kigali kuhusu ulinzi wa raia)  ambapo tunatoa miongozo bayana ya ulinzi katika hali zisizo hatari kabisa kama ile ya vita vya kimbari dhidi ya Watutsi mwaka wa 1994, na pia jinsi ya kuzuia [hali kama hizo], na muhimu zaidi, namna ya kuwalinda watu badala ya kuwawacha.

Aidha, mimi binafsi nimeshiriki bia kwa ufanisi uwenyekitiwa Azimio kuhusu mageuzi katika nguzo ya amani na usalama katika Umoja wa Mataifa, ambalo linasisitiza, miongoni mwa mambo mengine, ulinzi, na ugavi wa mamlaka kwa kamanda, kwa walio nyanjani, na kuhakikisha kwamba tu wepesi na tunaweza kuchukua hatua kwa njia iliyo kamilifu.

Ni katika kipindi hiki pia ambapo, kwa mara ya kwanza kabisa, iliporatibiwa katika Baraza Kuu la UN kwamba kilichofanyika nchini Rwanda mwaka 1994 kilikuwa ‘Vita vya Kimbari dhidi ya Watutsi’ – awali mwaka 2018 na baadaye tena mwaka jana 2020. Hili lina umuhimu mkubwa kwetu kwa kuwa tunafahamu, hatima ya kubirua historia, au kukana historia. Hili ni deni letu, angalau, kwanza, kwa wahanga wa vita hivyo baada ya kupoteza mengi, ya kulinda heshima ya walioaga, na pia kwa jamii nzima ya Rwanda.

Changamoto kuu katika kazi yako ni gani kufikia sasa?

Ah! Changamoto kuu katika hii kazi si ya kipekee kwa Rwanda. Ni changamoto iliyo maarufu katika jumbe nyingi za Afrika. Tuna timu ndogo, ndogo zaidi katika jumbe zetu, ilhali hatuwezi kukosa kuhudhuria kwa kuwa hiyo ndiyo kawaida ya diplomasia – unaufanya ushawishi kupitia kwa majadiliano. Hili tatizo ni kawaida katika asilimia 80 ya jumbe za Afrika hapa New York. Ukiulinganisha ujumbe wa Rwanda na ujumbe mwingine wowote ule wa matifa ya Ulaya, yana zaidi ya mara tano au sita ya idadi ya wanadiplomasia, ilhali majukumu ya mataifa wanachama ni sawa. Hata hivyo, ingawaje tuna timu ndogondogo sana, tuna ari ya hali ya juu na tunatoa michango mikubwa.

Je, kuna changamoto nyingine ambayo ungependa kuzungumzia?

Kwangu mimi, ninapenda pia kuangalia changamoto zinazoyakabili mataifa ya Afrika. Ni muhimu sana kuwa na ushirikishi fanifu kuhusiana na mambo yanayofanyika katika bara hili, tunahitaji utaratibu wa ushirikishi wa kitaasisi. Kama unavyojua, Mkutano wa Viongozi wa Mataifa wa AU hufanyika mara mbili kwa mwaka. Hatuwezi kuutegemea Mkutano huo wa Viongozi kuyapata maamuzi yetu kisha tuyajumuishe katika masualayanayopewa kipaumbele na Kundi la Afrika. Tunahitaji kuwa na mfumo unaotenda kazi kwa msingi wa kudumu zaidi.

Huku unaposonga mbele, ni masuala yapi matatu unayoyapa kipaumbele kwa mwaka huu wa 2021?

Usawa wa matibabu na ujumuishwaji yanasalia masuala ya kipaumbele kabisa. Kuhusu usawa wa matibabu, sote tunashuhudia yanayofanyika kuhusiana na chanjo ya COVID-19, kwa hivyo usawa wa chanjo ni suala la kipaumbele.  Yaliyofanyika kuhusiana na chanjo ni kipimo kuonyesha iwapo ushirikiano wa kimataifa unafanya kazi au la. Na kufikia sasa, uamuzi ni kwamba haufanyi kazi. Hili lina maana kwamba tunastahili kuhakikisha kwamba ule unaoitwa ‘wema kwa wote’ inashughulikiwa kama wema kwa wote. Lakini mahususi kabisa katika matibabu, litakuwa kuhakikisha kwamba kuna maandalizi ya unyumbufu wa matibabu, kujenga mifumo nyumbufu.

Aidhausawa wa kijinsia na uwezeshaji wa wanawake utaendelea kuwa suala muhimu kwetu sisi. Tumeendelea kusalia miongoni mwa watetezi 10 wa mwanzo wa kampeni ya 'He for She' [kampeni ya UN kuhusu usawa wa kijinsia].

Vilevile, niliuchukua usukani mwishoni mwa mwaka jana [2020] wa uwenyekiti bia kwa pamoja na Mjumbe wa Kudumu wa Qatar, wa Kundi la Marafiki kuhusu Usawa wa Kijinsia, linaloyaleta pamoja zaidi ya mataifa 150 pamoja. Tunataka kuhakikisha kwamba usawa wa kijinsia tunaoushuhudia katika Usimamizi wa Umoja wa Mataifa hauhusishi tu nyadhifa za juu. Kweli, Katibu Mkuu, António Guterres amefanya kazi aula katika kutimiza usawa wa kijinsia katika nyadhifa za juu. Hata hivyo, usawa halisi wa kijinsia na ujumuishwaji halisi hufanyika katika ngazi ya kati ya usimamizi. Kwa hivyo, hili linastahili kuendelezwa na kufanywa sehemu kindakindaki ya utendakazi wa wasimamizi.

Labda unafahamu pia kwamba Rwanda hutajwa kama ‘taifa la kidijitali’ mara nyingi. Kwa hivyo usawa wa kidijitali utaendelea kuwa suala kuu la kipaumbele kwangu mimi na kwa taifa langu.

Aidha nitalitaja eneo moja zaidi  maendeleo endelevu. Ninaongoza kibia na marafiki wengine wachache, kazi kuhusu namna ya kujenga upya kwa njia bora na endelevu kutoka kwa janga la COVID-19, kwa kuwa limesababisha kuteseka kwingi. Tunastahili kuhakikisha kwamba tunabadilisha namna tunavyoyafanya mambo na kwamba tunaushughulikia ujumuishwaji kabisa, uendelevu na unyumbufu kwa njia thabiti mno.

Bila shaka, ijapokuwa ninalitaja kama suala la mwisho, si suala dogo kwa vyovyote vile. Amani na usalama ni msingi wa kila kitu, na tunastahili kuhakikisha kwamba tunaitoa michango yetu katika kutatua mizozo iliyoko katika bara hili la Afrika.

Kuna Wajumbe wa Kudumu wanawake wachache wa mataifa ya Afrika katika UN. Kwa sasa, katika mataifa ya Afrika, ni Angola, Chad, Eritrea, Rwanda na Afrika Kusini yenye wanawake wanaohudumu kama Wajumbe wa Kudumu wa mataifa hayo. Madagaska pia ina mwanamke anayehudumu kama Naibu wa Balozi. Unafikiri ni kitu gani kinachostahili kufanywa ili kuiongeza idadi hiyo?

Naam, tunahitaji kuuhamasisha uongozi wetu katika ngazi mbalimbali kuhusu umuhimu wa kutimiza, kama sio usawa, basi uwakilishwaji bora katika diplomasia, sio tu katika jukwaa kubwa kabisa la kimataifa, ambamo ni New York, bali pia katika majukwaa mengine ya kimataifa, kama Geneva na Addis Ababa.

Wakati mwingine ni vyema pia, kuweka wazi takwimu, kuonyesha habari kuhusu uwakilishi wa wanawake. Na, kusema kweli, hili sio tatizo la Afrika pekee. Miezi michche iliyopita, nilikutana na mwenzangu kutoka Uholanzi. Na ingawaje Uholonzi imekuwa ikipigania sana usawa wa kijinsia, balozi wa sasa wa Uholanzi ndiye Balozi mwanamke wa Kwanza wa Uholanzi katika Umoja wa Mataifa. Na hiki sio kisa kimoja tu. Kwa hivyo, bila shaka, tunaangazia sana bara Afrika, lakini utashangaa kwamba tunafanya vyema kuliko kanda nyinginezo. Ninaweza kusema kwamba, ni mataifa ya Karibia pekee ndiyo yanayofanya vizuri kuhusiana na uwakilishaji halisi wa wanawake katika nyadhifa muhimu.