Kubaini uwezo halisi wa ndizi ‘bandia’

Get monthly
e-newsletter

Kubaini uwezo halisi wa ndizi ‘bandia’

Selamawit Araya Kidane (from Ethiopia) talks about her research on the nutritional benefits of the Enset plant.
Afrika Upya: 
23 March 2021
ILRI/Georgina Smith
Husband and wife prepare enset at their home in Doyogena District, Ethiopia.

Selamawit Araya Kidane (kutoka Ethiopia) anazungumzia safari yake ya kuwa mwananematolojia (wanasomea kuhusu minyoo inayokula viumbe vidogo kama bakteria na kuathiri mimea, wanyama na binadamu) vilevile utafiti wake kuhusu mmea wa Enset – kwa kawaida huitwa ‘ndizi bandia’ kwa sababu unafanana na mgomba ila  hauzai matunda yanayoweza kuliwa. Shina lake, ala ya majani na shina la ardhini huvunwa na kutengenezwa kuwa bidhaa zilizosheheni virutubisho vya wanga.

Selamawit Araya Kidane
Selamawit Araya Kidane

Tueleze kuhusu wewe. Ulizaliwa wapi na kukulia wapi ?

Nilizaliwa Saudi Arabia kwa wazazi wahamiaji wa Ethiopia. Tulihamia hadi Addis Ababa, Ethiopia nilipokuwa na umri wa miaka tisa.

Nini kilikuhamasisha kuhusu sayansi kwa ujumla, na haswa nyanja ya utafiti ya nematolojia?

Nikiwa sekondari, nilipenda sana biolojia. Nilipenda sana fiziolojia ya mimea na maumbile. Nilipata shahada ya kwanza ya sayansi katika kilimo cha mazao ya bustani mwaka 2018 (hortculture) kutoka chuo kikuu cha Jimma nchini Ethiopia. Magonjwa ya mimea ilikuwa sehemu muhimu ya masomo yangu ya shahada ya kwanza na ndivyo nilivyogundua kuhusu vimelea- vijiminyoo vidogo ambavyo viko katika kila mazingira kote ulimwenguni. Nilivutiwa na hivi viumbe vidogo lakini muhimu na nilitaka kuvijua zaidi. Lakini kulikuwa na taarifa kidogo kuhusiana na mada hiyo. Mnamo mwaka 2010, nilifanikiwa kuomba udhamini wa VLIR-UOS ili kuendelea na masomo ya Nematolojia katika chuo kikuu cha Ghent, Ubelgiji. [Udhamini wa VLIR-UOS hupewa wanafunzi kutoka Afrika, Asia na Latini Amerika kwa ajili ya programu za uzamili katika chuo kikuu cha Flemish].

Tueleze kidogo zaidi kuhusu vimelea?

Vimelea vinaweza kuishi huru kwenye udongo au katika maji, ambapo wanakula vijidudu vidogo (bakteria, kuvu, mwani na vimelea vingine) na uchafu wa kikaboni. Wanaweza kuwa vimelea vinavyoleta madhara makuwa kwa binadamu, wanyama na mimea.

Utafiti wangu wa shahada ya uzamili ulilenga zaidi spishi ya vimelea ijulikanayo kama Caenorhabditis Elegans –ambayo imetumika kwa miaka mingi kama mfano wa kuzisoma hali nyingi za watu na wanyama. Uchunguzi wetu ulitumia kimelea hiki kujua masuala ya kuzeeka(umri).

Utafiti wako wa PhD unalenga sehemu gani?

Nashukuru kwa ushirikiano kati ya chuo kikuu cha Ghent na Taasisi ya Kimataifa ya Kilimo cha Tropiki (IITA) nilishirikiana na watafiti wa nematologia wanaofanya kazi Afrika.

Baada ya kufanya kazi kwa muda mfupi kama afisa wa mipango katika shirika la Mabadiliko ya Kilimo la Ethiopia(Ethiopian Agricultural Transformation Agency), nilipewa nafasi ya kuendelea na shahada ya uzamivu (PhD) katika chuo kikuu cha Norwegian University of Life Sciences,  chini ya usimamizi wa pamoja wa wananematolojia wa IITA na Kituo cha Kimataifa cha Fiziolojia ya Wadudu na Ikolojia (ICIPE). Masomo yangu yalidhaminiwa na shirika la Maendeleo la Norway (NORAD)

Utafiti wangu unalenga kuchunguza athari za vimelea vinavyoharibu mimea katika mmea wa ensent na jinsi athari zinazosababishwa nao zinaweza kushughulikiwa.

Enset ina umuhimu gani kama zao la chakula?

Wakati ukiwa hautambuliki sana nje ya Ethiopia, enset ni chakula kikuu muhimu sana nchini humo, ukiwa na takriban asilimia 20 ya watu (watu zaidi ya milioni 20) wanaoutegemea.

Licha ya kwamba Enset mwitu inapatikana barani Afrika, mmea huu umepandwa nchini Ethiopia tu. Enset inalimwa katika sehemu za kaskazini na kaskazini –magharibi mwa nchi, ni mmea unaoshiria kilimo na tamaduni, ukihakikisha usalama wa chakula, mapato ya kifedha na chakula cha wanyama, pamoja na kuzuia mmomonyoko wa udongo na kupoteza udongo katika nyanda za juu zilizoinuka.

Mojawapo wa vyakula vya Enset vinavyotambulika sana ni Kocho, chakula mfano wa mkate uliovundikwa na haswa kutumika badala ya chakula maarufu cha Ethiopia Injera. Umuhimu wa Enset ulijulikana wakati wa baa kubwa la njaa nchini Ethiopia katika miaka ya 1980, ambalo halikuathiri jamii zilizokua zinalima zao la Enset.

Mafanikio ya utafiti wako ni yapi ?

Zao la Enset linaendelea kudunishwa na watafiti, huku uchunguzi wa kisayansi dhidi yake ukiwa mdogo sana. Pia ni machache sana yanayojulikana kuhusu vimelea vinavyoathiri mmea huo, athari vinavyosababisha na jinsi ya kuzimudu. Kutokana na hilo, utafiti wetu umefungua njia kwa namna nyingi.

Tumefanya utafiti mkubwa hadi sasa ili kubaini ni spishi gani ya kimelea iliyopo na ni ipi inakuwa tishio kubwa kwa Enset. Kwa mara ya kwanza, tumekagua nafasi ya malighafi ya kupandia katika kuenea kwa wadudu hawa na kutathmini vitu mbalimbali kwa ajili ya kupambana nao.

Utafiti wako unachangia vipi katika Malengo ya Maendeleo Endelevu?

Lengo namba mbili la Maendeleo Endelevu: Kumaliza Njaa, linalenga kumaliza njaa ulimwenguni ifikapo mwaka 2030. Hata hivyo lengo hili halionekani kuwa na mwelekeo, hasa ukizingatia madhara ya janga la COVID-19, ambayo yametabiri ongezeko la idadi ya watu walio na njaa. Kwa hiyo, ni muhimu kuubadili mfumo wa ulimwengu wa chakula na kilimo.

Kutegemea sana kundi maalum la mazao makuu ni tishio ambalo ulimwengu haliwezi kulimudu tena. Kwa hiyo, mimea iliyotelekezwa ama isiyotumiwa sana, ambayo inajumuisha spishi ya kale ya Enseti inahitaji kuenezwa.

Uchunguzi wetu umetoa nafasi kwa utafiti zaidi ili kuendeleza uzalishaji wa Enseti. Pia tumetengeneza itifaki mbalimbali, tumebuni mbinu mpya na njia,  na kuongeza ufahamu kwa ajili ya uchunguzi na usimamizi wa vimelea vya mimea, ambavyo huathiri sana, kama si yote, mazao yaliyopandwa na kusababisha athari ya mabilioni ya dola kila mwaka.

Je kumekuwa na ushawishi wowote wakati wa safari yako ya masomo? Ni kina nani  washauri wako wakuu?

Mshawishi wangu mkuu alikuwa mama yangu.  Kwa kuwa yeye mwenyewe hakuwa na elimu rasmi, alikuwa amedhamiria kuwa watoto wake, nikiwemo mimi, ambaye ni binti yake wa pekee, waendelee kadri iwezekanavyo. Msimamizi na mshauri wangu Dkt.Danny Coyne, mwanasayansi wa afya ya udongo  na mtaalam katika nematolojia ya mimea huko IITA, amenipa busara zake, ameniongoza na kunipa motisha, na kunikumbusha kuwa lengo la mwisho la utafiti wetu ni: kuboresha maisha ya wakulima wadogo Afrika.

 

Mada: