Kurejea kwa hali ya kawaida barani Afrika baada ya COVID-19: ni mbio za masafa mafupi au marefu?

Get monthly
e-newsletter

Kurejea kwa hali ya kawaida barani Afrika baada ya COVID-19: ni mbio za masafa mafupi au marefu?

Orodha ya jitihada ambazo nchi zitalazimika kufanya ili kukabiliana na athari ya janga hili ni ndefu mno.
Afrika Upya: 
25 March 2021
Conference of African Ministers of Finance, Planning and Economic Development  22 March 2021
Mkutano wa Mawaziri wa Fedha wa Afrika, Mipango na Maendeleo ya Uchumi 22 Machi 2021.

Nchi za Afrika bado hazijaona mwanga dhidi ya janga la COVID-19, lakini ni lazima zifanye kwa haraka mabadiliko makubwa ya kiuchumi ili kujiandaa kwa ajili ya baadae kwa sababu haiwezekani tena kurudi katika mfumo wao wa kabla ya janga.

Ingawa janga hili limezalisha uhitaji wa dharura wa ongezeko la msaada wa kimataifa kwa Afrika ndani ya utaratibu wa muundo wa kisasa zaidi wa ushirikiano wa mataifa, ukanda huu utalazimika kushika usukani wa mustakabali wake kwa kukuza aina mpya ya ushirikiano na sekta binafsi - katika ngazi ya kitaifa na kimataifa - ili kupata fedha zinazohitajika kwa ajili ya kurejesha uchumi wao na kukabiliana na athari za muda mfupi na za muda mrefu za janga hili.

Hizi ndizo zilizokuwa hoja kuu za kutiliwa maanani katika mkutano wa ngazi ya juu "Majadiliano ya kina: Je, mfumo wa ushirikiano wa nchi zenye lengo la pamoja ulijiandaa kwa janga la COVID-19 na je sekta binafsi zilifanya ya kutosha?" uliofanyika wakati wa kitengo cha kiwizara cha Awamu ya Hamsini na Tatu ya Mkutano wa Mawaziri wa Fedha, Mipango na Maendeleo ya Kiuchumi mnamo Machi 22, 2021.

Ufikiaji wa chanjo za COVID-19

Katika ulimwengu ulioendelea, uzinduzi wa kampeni za chanjo na matokeo chanya ya kwanza ya hatua za kukabiliana na janga la kiuchumi yamezipa nchi hizo mwanzo mzuri katika mbio za kukabiliana na muktadha mpya wa kiuchumi baada ya COVID-19.

Hata hivyo, Afrika, bado iko nyuma katika foleni kuhusiana na ufikiaji wa chanjo,  na ni bara pekee ambalo limekosa fedha kupunguza athari za kiafya katika uchumi wake, na bado lipo mbali katika kutokomeza tatizo hilo.

Ili kuzuia kuenea kwa janga hili, nchi zote zimeanza kuchukua hatua za kujilinda, jambo ambalo limesababisha nchi kurejea katika dhana ya sera ya kulinda viwanda vyake vya ndani dhidi ya ushindani na nchi za nje. Hii imeleta sintofahamu, licha ya kuwasili kwa chanjo, na sasa, tunazungumza kuhusu wimbi la pili na la tatu na kutokea kwa aina mpya za COVID-19, asema Waziri wa Uchumi na Udhibiti wa nchi ya Gabon, Nicole Roboty.

Hali hii inaweza kuwa na athari kubwa za muda mfupi na mrefu kwa maendeleo ya Afrika, na athari halisi kwa sehemu zilizosalia ulimwenguni, na kufanya wataalamu kutoa mwito wa kuongezwa kwa usaidizi kwa Afrika, kulingana na Mkurugenzi wa IMF kwa Afrika, Abebe Aemro Selassie.

"Ninafikiri ukanda huu unaenda kukabiliana na miaka michache migumu kwa kiasi fulani. Kitakachotokea katika kipindi cha miaka 5 - 8 ijayo barani Afrika ni suala la masilahi kwa jamii ya kimataifa. Mabadiliko ya kidemografia yanayofanyika katika bara hili yanamaanisha kwamba angalau kidemografia - lakini pia kwa maoni yangu kiuchumi - karne ya 21 ndiyo karne ya Afrika,” aliongeza.

Bw. Selassie alipongeza uamuzi wa hivi karibuni wa nchi za G7 kutoa Haki mpya Maalum za Sarafu (SDR) kwa manufaa ya nchi zinazoendelea na zile zilizo katika hatari ya COVID-19, hatua ambayo inapaswa kuzinufaisha nchi zenye uchumi wa kati kama vile Gabon. 

Hata hivyo, kwa mara nyingine, msaada wa kimataifa kwa Afrika hauwezi kuegemezwa kwenye muundo sasa kama zamani kwa kuwa utalazimika kufanyika ndani ya utaratibu mpya, ushirikiano wa nchi zenye lengo moja baada ya COVID-19, na kusaidia kuliwezesha bara hili kukabiliana vilivyo na majanga yajayo.

"Jambo la kwanza tunalohitaji kutambua ni kwamba janga ambalo tunakabiliana nalo sasa halitakuwa la mwisho. Mfumo wa sasa wa ushikiano wa nchi zenye lengo moja uliundwa katikati ya karne ya 20, kama tunavyofahamu sote, na ukweli umebadilika sana tangu wakati huo", alisema Arkebe Oqubay, Waziri wa ngazi ya juu na Mshauri Maalum wa Waziri Mkuu wa Ethiopia, na mgombea wa wadhifa wa Mkurugenzi Mkuu wa UNIDO.

Kitu ambacho Afrika inahitaji ni karne inayoweza kutabirika zaidi siku za usoni, mwitikio wa pamoja wa kimataifa na kikanda na mfumo uliopambanuliwa upya wa ushirikiano wa nchi zenye lengo moja. Hili ni suala la kimsingi kwa maoni yangu. Katika hali isiyoweza kutabirika kama hii ya sasa, itakuwa vigumu kukabiliana na janga bila miitikio iliyoratibiwa, Bw. Oquabay aliongeza.

Zaidi ya usaidizi kutoka taasisi za kimataifa, Afrika italazimika kuchukua hatua muhimu, hasa katika masuala kama vile chanjo, ufikiaji ambao utakuwa na athari za kiuchumi katika mwaka unaokuja.

Afrika pia italazimika kuchukua fursa baada ya COVID-19 ili kuleta mageuzi katika uchumi wake, kwa sababu kurejea katika muundo wa kiuchumi wa kabla ya janga hakutairuhusu kuzalisha nafasi za kutosha za kazi kwa mamilioni ya vijana kila mwaka kwenye soko lake la ajira.

Mataifa kupangilia upya vipaumbele

Ili kufikia lengo hili, nchi kadhaa kama vile Ethiopia, Gabon na Naijeria ziko katika mchakato wa kupangilia upya masuala yao ya kimkakati yanayohitaji kupewa kipaumbele na kuwekeza katika maendeleo endelevu, yanayolinda mazingira, kuweka mazingira ya viwanda na kuendeleza maguezi ya nishati.

"Kuna fursa kubwa katika nchi zetu. Ndiyo, kunazo hatari, lakini ukiangalia biashara ambazo zimekuwepo kwa miaka mingi, kuna fursa nyingi nzuri kati yake. Tunatafuta biashara zitakazokuja na kushirikiana na biashara za ndani kukua nchini Naijeria," alisema Zainab Ahmed, Waziri wa Fedha, Bajeti na Mpango wa Kitaifa wa Naijeria.

"Serikali ya Ethiopia inatambua kwamba kuangazia sekta za viwanda na uzalisha ni njia bora ya kuhakikisha ukuaji endelevu. Viwanda haviwezi kujengwa bila mazingira yanayohitajika", Bw. Oqubay alisema.

Pamoja na jitihada hizi, nchi za Afrika zitalazimika kubadilisha njia zao za kushirikiana na sekta binafsi, zote za ndani na kimataifa. Sekta binafsi zitakuwa na nafasi ya kufanya maamuzi katika kurejesha uchumi baada ya COVID-19 kwa sababu ya uwezo wake wa kuzalisha kazi.

Hata hivyo, uhusiano kati ya serikali mbalimbali na sekta binafsi lazima uangaliwe upya, alionya Masood Ahmed, Rais wa Kituo cha Maendeleo ya Kimataifa (CGD) kilicho na makao makuu yake jijini Washington.

"Katika awamu ya kwanza [ya janga], nchi zilinuia kusaidia kila kampuni katika sekta binafsi kwa sababu ilikuwa ni dharura, lakini sasa, katika kurejea katika hali ya awali, baadhi ya kampuni zitaendelea na zingine hazitaendelea, kwa sababu mazingira ya kiuchumi yanaenda kubadilika", alieleza.

Sasa, mazungumzo yenye changamoto zaidi lazima yafanyike kuhusu aina ya kampuni zinazofaa kupewa msaada, kwa namna gani na jinsi ya kuweka ushirikiano unaotambua kwamba maisha hapo baadae hayatakuwa tu kama zamani. Hiyo inahitaji kiwango fulani cha uelewa wa pamoja wa matokeo ya siku zijazo, kupunguza dhana ya "sisi na wao" kati ya sekta ya umma na ile ya binafsi, aliongeza.

Kimataifa, nchi za Kiafrika zitalazimika kutegemea mitaji ya soko, ambayo ni 40% ya deni la la nje la ukanda huu, kupunguza upungufu wa kifedha uliosababisha kuzorota kwa maendeleo ya Afrika hata kabla ya janga hili, na huenda sasa likawa tishio katika kurejesha uchumi wake baada ya COVID-19.

Nchi za Kiafrika zitalazimika kuwekeza katika imani ya mwekezaji ili kujenga imani katika masoko ya mitaji.

Katika changamoto zilizopita, wawekezaji waliangalia viwango na vyanzo vingine vinavyoaminika kama vile IMF, lakini wawekezaji waliangaliana zaidi wenyewe. Wawekezaji wanaweza kujifanya kama kundi katika hali za majanga, alisema Alastair Wilson, Mkurugenzi Mkuu na Mkuu wa Moody's Sovereign Risk Group na Moody's Investment Services.

Tabia ya kawaida ambayo imeshuhudiwa katika majanga yaliyopita imekuwa ni uondoaji wa mtaji katika nchi zilizotambuliwa kama ziko katika hatari na kupelekwa katika nchi zinazoonekana kama ni zenye faida na hazina hatari sana.

Katika hali ya aina hii, mashirika ya ukadiriaji si sehemu ya tatizo lakini ni sehemu ya suluhu, kwa sababu katika aina hii ya soko ni muhimu kuwa na sauti iliyokadiriwa kuleta namna fulani ya uthabiti, Bw. Wilson alisema.

Ili kuvutia na kuweka uwekezaji thabiti wa nje, ni lazima serikali za Kiafrika zipunguze hatari kwa kuimarisha ubora wa taasisi zao za kitaifa na kuchukua hatua kama vile kuimarisha utawala bora, uwazi, urahisi wa kufanya biashara, vita dhidi ya rushwa na kuwekeza katika miundombinu, teknolojia na mtaji wa binadamu.

Mbio za marathon

Orodha ya jitihada ambazo nchi za Afrika zitalazimika kufanya katika muda wa miaka michache ijayo ili kukabiliana na athari za janga hili linaloendelea la kiuchumi ni ndefu mno.

"Fikiria kuhusu suala hili kama marathon badala ya mbio za masafa mafupi na kwa hakika ni marathon ambayo tutashiriki wakati ambapo inabadilishwa na mazingira yaliyopo duniani," alisema Bw. Ahmed.

Tazama "The Big Debate: Was the multilateral system prepared for the COVID-19 crisis and did the private sector do enough?" iliofanywa tarehe 22 Machi 2021 hapa:  https://www.youtube.com/watch?v=u1bQEUNTkig  (kuanzia saa 10:20:00 hadi 11:43:00)

Mada: