Wanamapinduzi waliorejea: Kutimiza ndoto, kupata uhuru

Get monthly
e-newsletter

Wanamapinduzi waliorejea: Kutimiza ndoto, kupata uhuru

Wamarekani Waafrika wana historia ndefu ya kurejea nyumbani
Afrika Upya: 
25 March 2024
Supplied
Diallo Sumbry
Ikiwa huwezi kusoma sasa, sikiliza tu toleo la sauti: 

Umoja wa Mataifa uliteua Mwongo wa Kimataifa wa Watu wa Asili ya Kiafrika kuanzia 2015 hadi 2024, ili kukuza utambuzi, haki na maendeleo ya vizazi vya Kiafrika duniani kote. Kupitia programu mbalimbali, matukio, na kampeni za uhamasishaji, Mwongo huu unalenga kuliunda jukwaa la mazungumzo, maelewano na mabadiliko chanya katika maisha ya watu wanaoishi katika diaspora. Afrika Upya litachapisha ‘Katika Kuusaka Utambulisho Uliopotea Kitambo’ – mfululizo wa sehemu nne unaoangazia safari ambazo Wamarekani Waafrika wanazifanya ili kuungana tena na Afrika – bara ambalo mababu zao waliliita nyumbani:

Mwaka 1977, mfululizo mdogo wa kuvunja rekodi ulijinyakulia mahali pake katika hatua muhimu ya historia ya Marekani. Huku ukikitwa kwa  riwaya ya Alex Haley ya mshindi wa Tuzo ya Pulitzer, Roots: The Saga of an American Family, igizo hilo la runinga liliufichua ukatili wa biashara ya utumwa kupitia bahari ya Atlantiki na athari zake kwa vizazi vilivyofuata.

Ghafla usiku kucha — usiku nane kamili — Roots, mshindi wa Tuzo ya Emmy ilibadilisha lugha chafu ya ubaguzi ya “Rejea Afrika” kuwa wito wa kuchukua hatua, fursa kwa Wamarekani Waafrika ili kuurejesha urithi wao ulioibwa.

Kurejea Afrika 

Takriban miaka 40 baada ya Roots kutolewa, Diallo Sumbry alienda Ghana kutafuta nidhamu ya kiroho. "Awali, nilikuja kusoma udhihirisho na sayansi ya kitamaduni ya Kiafrika," mjasiriamali huyo wa Washington DC alisema.

Katika ziara mwaka 2016, Bw. Sumbry aliupokea unabii, kwamba “kama ningehamia Ghana na kuamua kufanya biashara hapa, mambo yangeniendea vyema. Ningetimiza misheni yangu ya maisha, na Ghana ingekuwa makao yangu ya kiroho.”

Ziara kumi na mbili baadaye, alijikuta akiutimiza unabii huo kwa kuwaunganisha tena watu wa diaspora ya Afrika na bara la Afrika.

Akiwa msanifu mwenza wa “Mwaka wa Kurejea”, wa Ghana, Bw. Sumbry alisaidia kuwezesha kampeni ya kimataifa kwa ajili ya ukumbusho wa miaka 400 wa kuwasili kwa kwanza kulikorekodiwa kwa Waafrika watumwa huko Marekani mwaka 1619.

[Mwaka wa Kurejea wa 2019 ulikuwa mpango wa serikali ya Ghana na Adinkra Group, ambalo lilitaka kuwahimiza Waafrika katika diaspora kukaa na kuwekeza katika bara hilo].

Huku kukiwa na zaidi ya wageni milioni 1.1 wa kimataifa, kulingana na Mamlaka ya Utalii ya Ghana, kurejea huko kunaweza kurekodiwa kama kurejea nyumbani kukuu zaidi kwa Wamarekani Waafrika wanaovuka Atlantiki katika historia.

"Mwaka wa Kurejea" ulibadilisha utalii wa Kiafrika," Bw. Sumbry alisema.

Mwaka 2020, kampeni ya "Mwaka wa Kurejea" ilibadilika na kuwa “Zaidi ya Kurejea," mpango wa miaka 10 wa mamlaka ya utalii. "Kila uendako, watu wanazungumza kuhusu diaspora," Bw. Sumbry alisema. "Ilizua kitu, na labda hatutaona upeo kamili wa athari yake kwa miaka mingi ijayo."

Kitulizo kutoka kwa ubaguzi wa rangi

Kila mtu mwenye asili ya Kiafrika anapaswa kutembelea bara hili angalau mara moja maishani mwake, kulingana na Bw. Sumbry, ambaye hupanga safari kupitia kampuni yake, Adinkra Group, ambako anahudumu kama rais na afisa mkuu mtendaji.

"Tajriba hiyo inaweza kuwapa Wamarekani Waafrika kiwango cha juu cha uhuru," alisema. "Hakuna ubaguzi wa rangi hapa kama tunavyoona huko Marekani. Umejikita zaidi hapa. Unaweza kuhisi roho yako na mababu zako. Unaweza kuwa ulivyo.”

Juhudi zake huenda zikaweka jina la Sumbry kwenye orodha ya watu wa kihistoria waliopigania harakati za ‘Kurejea-Afrika’. Atakuwa katika kundi bora.

Mwaka 1815, mkuu wa biashara za meli wa Massachusetts Paul Cuffe alitilia shaka iwapo angefikia usawa wa rangi maishani mwake. Mhisani huyo aliwashawishi Wamarekani Waafrika wengine 38 kuishi nchini Sierra Leone, na alifadhili makazi yao huko.

Kulingana na Chama cha Kihistoria cha White House, Bw. Cuffe anaaminika kuongoza vuguvugu la kwanza fanifu la Kurejea-Afrika nchini Marekani; juhudi zake zilitumika kama msukumo kwa  Jamii ya Ukoloni ya Marekani, iliyoanzishwa mwaka wa 1816 kuanzisha Liberia na kuwapa makazi Wamarekani Waafrika huko.

Karne moja baadaye, mzaliwa wa Jamaika Marcus Garvey alihamia Jiji la New York na kuwahimiza Wamarekani Waafrika kuabiri meli za Black Star Line kwa ajili ya safari ya kurejea kwa kuvuka bahari ya Atlantiki.

Rais wa Ghana Kwame Nkrumah alipata msukumo kutoka kwa mwanazuoni wa Pan-Afrika aliyeelimishwa na Harvard W.E.B. Dubois, ambaye alishiriki kuanzisha Chama cha Kitaifa cha Maendeleo ya Watu Wenye Rangi (NAACP) mwaka wa 1909 ambacho kingekuwa shirika la haki za kiraia lililodumu kwa muda mrefu zaidi nchini Marekani

Kulingana na Wakfu wa Haki za Kikatiba, Bw. Dubois aliukana uraia wake wa Marekani na kuwa raia wa Ghana, ambako alikaa siku zake za mwisho. Alizikwa kwenye jumba la makumbusho lililopewa jina kwa heshima yake huko Accra.

Mapema miaka ya 1960, mshairi Maya Angelou na mwanawe wa kiume pia  waliishi Ghana miongoni mwa Waamerika Waafrika kutoka nje takriban 200 ambao aliwataja kama "Wanamapinduzi Waliorejea."

"Tulikuwa Wamarekani Weusi walioishi Afrika Magharibi, ambako — kwa mara ya kwanza maishani mwetu — rangi ya ngozi yetu ilikubaliwa kuwa sawa na ya kawaida," Bi. Angelou aliandika katika tawasifu yake, All God’s Children Need Traveling Shoes.

Hadi leo, maoni ya Bi Angelou yanawahusu kina mama Wamarekani Waafrika  ambao wameamua kurejea nymbani. 

Amani nyumbani 

Katika mashirika ya Marekani, Ashley Cleveland alikuwa akifanya kazi yake aliyoienzi ya teknolojia akiwa na cheo cha mtendaji na mshahara mkubwa huku wasimamizi wakimchukulia kana kwamba alikuwa katika nafasi ya msaidizi wa usimamizi. 

"Wanawake Weusi huletwa katika mashirika, na husherehekewa mwanzoni," mzaliwa huyo wa Boston alisema. "Kisha wanapitia uchokozi huu mdogo, na mwishowe wanaachiliwa."

Baada ya kuachishwa kazi mara tatu katika kipindi cha miaka mitano, aliingia katika kituo cha matibabu ya kisaikolojia, na akakipata kikiwa kimejazwa na wanawake wengine weusi wa ngazi ya juu wenye simulizi kama hizo. Aliuchukua mwaka mmoja kuyapanga upya maisha yake: Alibadilisha kutembelea madaktari wa magonjwa ya akili pamoja na kutumia dawa alizoandikiwa na daktari na kupanda na kutembea kwenye fukwe za Tanzania katika Afrika Mashariki.

Awali, alikuwa na shaka ikiwa anapaswa kuhamia ng'ambo mtoto wake wa kwanza alipozaliwa. Hivi majuzi, mama huyo wa watoto wawili alihamia Johannesburg. Wakati hafanyi kazi kama mkuu wa ukuaji wa BrandUp Global, anawiana na Bi. Angelou kwa kuziambia familia nyingine za Wamarekani Waafrika ni kwa nini lazima zihamie katika bara hilo. "Ninaeleza manufaa ambayo kunawapa watoto Weusi kuishi katika jamii ambamo rangi ya ngozi zao si tatizo." 

Bi Cleveland, ambaye watoto wake wanajifunza Kizulu na Kiswahili katika shule ya msingi, alisema kwamba wana ujuzi zaidi na wanapata changamoto kiakili ng’ambo. "Wana utoto bora. Hatuna wasiwasi tena kuhusu kuwapeleka shuleni na kuwazia ikiwa watarudi salama."

Alipoulizwa kama alikuwa na mipango yoyote ya kurudi nyumbani, alijibu: “Wapi? Marekani? Nina amani hapa hivi kwamba sitakiwi kuiwacha. Hatuna wasiwasi kuhusu kusimamishwa na polisi. Sifanyi kazi na wasiwasi huo kama mzazi tena. Hapa, mimi ni mama bora."

Kwa Bi. Cleveland, Afrika ni nyumbani.


Bi. Beard ni mwandishi na mwalimu anayeishi New York.

Mada: