Mwaka mmoja baadaye: Athari za mzozo baina ya Urusi na Ukrainia kwa Afrika

Get monthly
e-newsletter

Mwaka mmoja baadaye: Athari za mzozo baina ya Urusi na Ukrainia kwa Afrika

Kushughulikia deni huku tukiimarisha kilimo, upatikanaji wa nishati na biashara barani kunaweza kupunguza mzigo kwa chumi zinazokaribia kuanguka
Bitsat Yohannes-Kassahun
Afrika Upya: 
13 February 2023
António Guterres watches grain being loaded on the Kubrosliy ship in Odesa, Ukraine
UN Photo/Mark Garten
Secretary-General António Guterres watches grain being loaded on the Kubrosliy ship in Odesa, Ukraine.

Katika ulimwengu wa kisasa unaoungana kwa mengi, risasi zinazofyatuliwa uoande mmoja wa dunia zinaathiri mno maeneo mengine yanayoonekana kuwa mbali. Mwaka mmoja tangu Urusi ivamie Ukrainia mnamo Februari 24, nchi za Afrika, ingawa ziko umbali wa maili nyingi, hazijaepuka na athari za uvamizi huo.

Ingawa mengi yanaweza kusemwa kuhusu utata wa kisiasa na kisera unaohusu mzozo huo, athari halisi na inayoonekana katika maisha ya Waafrika wengi wa kawaida inatatiza nyoyo sana.

Kutokana na hali ya kuongezeka kwa bei za vyakula na nishati na kupungua kwa kapu la ufadhili wa ushirikiano wa kiuchumi wa kimataifa, nchi za Afrika pia zinajikaza kuwa katika nafasi ya mabadiliko makubwa katika sera za kimataifa za nishati, hata zinapofikiwa na wabia mbalimbali ambao pia wanapambana na athari za kupatikana kwa nishati kwa raia wao wenyewe.

Mnamo 2020, nchi 15 za Afrika ziliagiza zaidi ya asilimia 50 ya bidhaa zao za ngano kutoka Urusi au Ukrainia. Nchi sita kati ya hizi (Eritrea, Misri, Benin, Sudan, Djibouti, na Tanzania) ziliagiza zaidi ya asilimia 70 ya ngano yao kutoka eneo hilo.

Uhaba mkali wa kimataifa wa nishati

Mtazamo wa Kiuchumi wa Ulimwengu wa 2022 unatoa taswira kamili ya hali ya nishati duniani, na kueleza kwamba "inaleta mshtuko mkubwa na tata sana na usio na kifani."

Shida hii inakuja wakati uchumi wa Afrika bado unajaribu kujinasua kutokana na athari za janga la COVID-19, ambalo kwalo bara halikuwa na rasilimali za kutosha kujikinga.

Kufikia katikati ya mwaka wa 2022, bei za nishati duniani zilipanda zaidi ya bei iliyowahi kushuhudiwa katika miongo mitatu, nayo bei ya gesi asilia ikiongezeka na kuuzwa zaidi ya Euro 300 kwa kila saa moja ya megawati. Gharama hizi za juu za gesi asilia zimeshuka kwa kiasi kikubwa kufikia Februari 2023, hadi chini ya dola 100 kwa kila saa moja ya megawati, kutokana na halijoto  wakati wa majira ya baridi kali katika maeneo ya kaskazini ya ulimwengu.

Serikali za Ulaya kwa kiasi kikubwa zilikinga raia wao kutokana na majanga haya ya bei kwa kutumia zaidi ya dola bilioni 640 kwa ruzuku ya nishati, kudhibiti bei za bidhaa rejareja, na kufadhili biashara. Serikali za Afrika, kwa upande mwingine, hazikuwa na uwezo wa kifedha wa kuwakinga watumiaji kwa hatua kama hizo, zilizohitajika sana kukabiliana na kupanda kwa bei ya nishati.

Mbali na shinikizo kutokana na kushuka kwa viwango vya ubadilishaji sarafu, na bei za juu za bidhaa, mfumuko wa bei  ulifikia asilimia 10 katika asilimia 40 ya nchi za Afrika. Zaidi ya hayo, nchi saba za Afrika zililemewa na deni kufikia Januari 2023, na 14 zaidi ziko katika hatari kubwa ya kulemewa na deni, jambo ambalo linazifanya zishindwe kutekeleza hatua zuizi kikamilifu. 

Kwa sababu hiyo, familia za Afrika, ambazo, kulingana na Mfumo wa Fedha wa Kimataifa, tayari zinatumia zaidi ya asilimia 50 ya matumizi yao ya jumla kwenye chakula na nishati, ziliathirika pakubwa na bei ya juu ya nishati duniani inayosababishwa na mizozo, pamoja na athari zao zisizo za moja kwa moja kwa gharama ya usafirishaji na bidhaa.

Bidhaa za chakula huchukua karibu asilimia 42 ya matumizi ya nyumbani ya Waafrika, na kufikia kiwango cha asilimia 60 katika nchi zilizoathiriwa na mizozo na ukosefu wa usalama.  Nchini Ufaransa na Marekani, vyakula vinawakilisha asilimia 13 na asilimia 6 ya matumizi ya nyumbani, mtawalia,  shirika la Umoja wa Mataifa linaeleza.

Mzozo wa nishati duniani pia ulileta mabadiliko ya sera, huku nchi nyingi sasa zikitaka kutumia gesi asilia na miradi mingine ya nishati ya kisukuku ili kukidhi mahitaji yao ya nishati.

Gesi asilia pia inazidi kupendwa na watu kama "uwekezaji wa kijani", kutokana na ahadi zilizotolewa kwenye mazungumzo ya tabianchi ya kimataifa ya COP26 huko Glasgow mnamo Novemba 2021 ili kupunguza ufadhili wa maendeleo kwa miradi ya gesi asilia.

Kwa nchi za Afrika, hii imemaanisha matakwa mapya katika kufuatilia kwa haraka miradi ya gesi asilia na gesi ya viowevu (LNG), ingawa hasa kwa ajili ya kuuzwa Ulaya na mingine nje ya bara.

Ingawa hii inaweza kuleta uwekezaji zaidi katika sekta ya nishati barani, manufaa hayawezi kusababisha upatikanaji wa nishati kwa Waafrika wenyewe. Badala yake, hii inahatarisha kuendeleza uchumi unaotegemea bidhaa, na kudumaza matarajio ya bara hili la viwanda.

 Kutatizwa kwa mifumo ya chakula barani Afrika

Wakati Afrika ina zaidi ya asilimia 65 ya ardhi isiyolimwa duniani, inaagiza chakula kutoka nje, na hivyo, imeathirika pakubwa na kupanda kwa bei ya chakula duniani, na kusababisha kuongezeka kwa uhaba wa chakula.

Kulingana na IMF, bei za vyakula vikuu barani Afrika "zilipanda kwa wastani wa asilimia 23.9 mwaka 2020-22 - zaidi tangu janga la kifedha duniani la 2008."

Hii ina athari kali kwa Waafrika wengi, ambapo bidhaa za chakula huchukua sehemu kubwa zaidi katika bajeti za matumizi ya nyumbani. Bidhaa za chakula huchukua karibu asilimia 42 ya matumizi ya nyumbani ya Waafrika, na kufikia kiwango cha asilimia 60 katika nchi zilizoathiriwa na mizozo na ukosefu wa usalama.  Nchini Ufaransa na Marekani, vyakula vinawakilisha asilimia 13 na asilimia 6 ya matumizi ya nyumbani, mtawalia,  shirika la Umoja wa Mataifa linaeleza.

Kwa mujibu wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), nchi za Afrika hutumia zaidi ya dola bilioni 75 kuagiza zaidi ya tani milioni 100 za kimetriki za nafaka kila mwaka. Mnamo 2020, nchi 15 za Afrika ziliagiza zaidi ya asilimia 50 ya bidhaa zao za ngano kutoka Urusi au Ukrainia. Nchi sita kati ya hizi (Eritrea, Misri, Benin, Sudan, Djibouti, na Tanzania) ziliagiza zaidi ya asilimia 70 ya ngano yao kutoka eneo hilo.

AfDB inabainisha kuwa uvamizi wa Urusi kwa Ukrainia kulisababisha upungufu wa karibu tani milioni 30 za nafaka katika barani, pamoja na ongezeko kubwa la gharama.

Ripoti ya Umoja wa Mataifa ya Hali ya Kiuchumi na Matarajio ya Dunia ya 2023 inaonyesha kuwa Afrika tayari ilikuwa na kiwango kikubwa cha uhaba wa chakula duniani mwaka 2020 huku asilimia 26 ikikabiliwa na uhaba mkubwa wa chakula na asilimia 60 ya watu walioathirika na uhaba wa chakula kwa kiwango cha wastani au kikubwa kulingana na Shirika la Chakula na Kilimo (FAO).

Tunatazamia msimu wa kilimo wa 2023-2024, bei na upatikanaji wa mbolea kwa wakulima barani Afrika utaamua jinsi bara hili litakavyokabiliana na uhaba mkubwa wa chakula.

Kwa mujibu wa Benki ya Dunia, uzalishaji wa chakula barani Afrika tayari unatatizika kutokana na matumizi duni ya mbolea, na “wastani wa kiwango cha matumizi ya mbolea cha kilo 22 kwa hekari moja, ikilinganishwa na wastani wa dunia ambao ni mara saba zaidi (kilo 146 kwa kila hektari).

Wakati wa ‘Mkutano Mkuu wa 2 wa Dakar kuhusu Kulisha Afrika: Uhuru wa Chakula na Ustahimilivu' uliofanyika tarehe 25-27 Januari 2023, AfDB iliripoti kuwa idadi hii iliongezeka kwa kasi mwaka 2022, huku Waafrika sasa wakiwakilisha theluthi moja (karibu watu milioni 300) ya idadi ya watu duniani ambayo kwa sasa inakumbwa na njaa na uhaba wa usalama.

Bei za mbolea

Kuvurugwa kwa usambazaji wa pembejeo za kilimo, ikijumuisha uagizaji wa mbolea kutoka Urusi, Ukrainia na Belarusi, kulitishia zaidi usalama wa chakula barani Afrika. Shirika la Mpango wa Chakula Duniani (WFP) liliripoti kuwa bei ya mbolea duniani imepanda kwa asilimia 199 tangu Mei 2020, huku bei ya mbolea ikiongezeka maradufu nchini Kenya, Uganda na Tanzania mwaka 2022.

WFP inabainisha kuwa "ijapokuwa haya ni matokeo ya vita vya Ukrainia, bei za vyakula, mafuta na mbolea tayari zilikuwa zimefikia kiwango cha juu zaidi kufikia mwisho wa 2021." "Mpango wa Black Sea Grain Initiative," uliosimamiwa na Umoja wa Mataifa na Uturuki na kutiwa saini Julai 2022, umepunguza baadhi ya "upungufu wa mbolea" kwa kuruhusu usafirishaji wa mbolea kutoka Ukrainia hadi kwingineko duniani.

Tunatazamia msimu wa kilimo wa 2023-2024, bei na upatikanaji wa mbolea kwa wakulima barani Afrika utaamua jinsi bara hili litakavyokabiliana na uhaba mkubwa wa chakula.

Kwa mujibu wa Benki ya Dunia, uzalishaji wa chakula barani Afrika tayari unatatizika kutokana na matumizi duni ya mbolea, na “wastani wa kiwango cha matumizi ya mbolea cha kilo 22 kwa hekari moja, ikilinganishwa na wastani wa dunia ambao ni mara saba zaidi (kilo 146 kwa kila hektari)".

Benki inakadiria kuwa usafirishaji wa mbolea kutoka kwa wauzaji wakuu kwa Afrika, ambao ni Ukrainia, Urusi na Belarusi, ambao bado umetatizwa, utaathiri uzalishaji wa chakula barani Afrika na kuzidisha uhaba wa chakula katika mwaka wa 2023.

Zaidi ya hayo, Benki ya Dunia inabainisha kuwa wazalishaji wengine wa mbolea wanapiga marufuku uuzaji nje wa pembejeo hizi muhimu ili kuwakinga wakulima wao wenyewe, na kuwaacha wakulima wa Afrika bila chaguzi nyingi.

Hitimisho

Huku ulimwengu ukitafakari kuhusu majanga mbalimbali yaliyotokana na mzozo wa mwaka mzima, Waafrika lazima wakabiliane na vitisho visivyotarajiwa vya muda mfupi kwa uchumi wao, mifumo ya chakula, na ustawi wao. Kwa hakika, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres, akizungumza katika Wito wa Kuchukua Hatua wa Usalama wa Chakula Duniani Mei 2022, alionya, "Tusipowalisha watu, tunalisha mizozo."

Katika hotuba yake ya ufunguzi katika mkutano huo, Rais Macky Sall wa Senegal alitaarifu kuwa, “Kutoka shambani hadi kwenye sahani, tunahitaji uhuru kamili wa chakula, na lazima tuongeze ardhi inayolimwa na upatikanaji wa soko ili kuimarisha biashara ya mipakani.

Kwa uongozi madhubuti, kuna baadhi ya mikakati ambayo inaweza kupunguza mzigo kwa uchumi unaolemewa:

  1. Kwa mfano, kutenga tena Fedha Maalum za Mfuko wa Fedha wa Kimataifa za dola bilioni 100 kusaidia nchi za Afrika na kurekebisha deni la kibinafsi na la umma kuzipa nchi hizi nafasi ya kifedha kukabiliana na janga.

 

  1. Pia kuna mwanga wa matumaini katika kukabiliana na athari za muda mrefu za mzozo huo. Muhimu zaidi ni nia njema ya kisiasa ya serikali za Afrika kulenga tena kilimo.

Katika Mkutano Mkuu wa 2 wa Dakar, Viongozi wengi wa Nchi na Serikali wa Afrika walikuwa na nia ya kuimarisha matumizi ya umma katika kilimo ili kujenga mfumo wa chakula wa Afrika unaojitosheleza na kustahimili.

Katika hotuba yake ya ufunguzi katika mkutano huo, Rais Macky Sall wa Senegal alitaarifu kuwa, “Kutoka shambani hadi kwenye sahani, tunahitaji uhuru kamili wa chakula, na lazima tuongeze ardhi inayolimwa na upatikanaji wa soko ili kuimarisha biashara ya mipakani. ”

  1. Kwa hakika, utekelezaji wa Eneo Huru la Biashara Afrika (AfCFTA), ambalo linaahidi ufanisi wa biashara ya mipakani, kungeruhusu usambazai bora wa  karibu tani milioni 30 za mbolea ambazo Afrika huzalisha kila mwaka. Uzalishaji huu ni mara mbili ya kiwango cha mbolea ambacho bara hili linatumia kwa sasa.
  2. Vilevile, AfDB inapanga kuwekeza dola bilioni 10 "ili kuifanya Afrika kuwa kapu la chakula duniani." Uwekezaji kama huo unaweza kusaidia sana katika kukopa suluhisho za kiteknolojia, kama vile matumizi ya mimea inayostahimili joto nchini Misri ili kuongeza mazao yake ya ngano. Nchi hiyo inapanga kuwa msafirishaji wa ngano kwa nchi zingine za Afrika katika mwaka wa 2023.
  3. Kwa upande wa nishati, kuharakisha upatikanaji wa nishati endelevu, ya kutegemewa na kwa bei nafuu, iwe kwa maendeleo ya viwanda, ajira kwa vijana wa bara hili, au kuhakikisha usalama wake wa chakula, kila kitu kilicho Afrika kiwe na mchanganyiko wa nishati sawia.

Msururu wa changamoto zinazoingiliana miaka hii michache iliyopita umebainisha jambo moja. Waafrika lazima wawe na msimamo mmoja ili kuepuka mzunguko mwingine wa unyonyaji wa bidhaa za rasilimali za nishati za bara hili, na kufanya kazi ili kuhakikisha upatikanaji wa nishati kwa wote barani Afrika.

Bitsat Yohannes-Kassahun ni Kiongozi wa Kikundi cha, Nishati na Tabianchi, katika Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Mshauri Maalumu wa Afrika (OSAA).

Bitsat Yohannes-Kassahun
More from this author