Vituo rafiki kwa watoto jimboni Ituri vyasaidia watoto kujifunza

Get monthly
e-newsletter

Vituo rafiki kwa watoto jimboni Ituri vyasaidia watoto kujifunza

UN News
21 May 2020
By: 
Watoto wakimbizi wa ndani wakiwa kwenye hema lililochanika katika makazi ya wakimbizi wa ndani ya Abs nchini Yemen.
OCHA/Giles Clarke
Watoto wakimbizi wa ndani wakiwa kwenye hema lililochanika katika makazi ya wakimbizi wa ndani ya Abs nchini Yemen.

 Nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC, shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF, linaendesha vituo rafiki kwa watoto kukusanyika kucheza na kujifunza, baada ya watoto hao kujikuta wakimbizi wa ndani kutokana na ghasia katika jimbo la Ituri.

Mapigano ya kikabila katika jimbo hilo yameendelea tangu mwanzoni mwa mwaka huu hali ambayo imesababisha UNICEF kuweka vituo hivyo katika kambi za wakimbizi wa ndani ikiwemo mji mkuu wa jimbo la Ituri, Bunia, ili watoto waweze siyo tu kujifunza na kucheza, bali pia kusikilizwa.

UNICEF inasema kuwa ni katika vituo hivi ambapo pia wanapata fursa ya kuhesabu watoto ambao wamekimbia makwao na wanaishi kwenye kambi za wakimbizi wa ndani bila wazazi au walezi.

Msimamizi wa vituo hivi rafiki kwa watoto mjini Bunia ni Grace Malosi Dhedza ambaye anasema kuwa, “vituo hivi kwanza vinajengwa na DIVAS, ambacho ni kitengo masuala ya jamii kwa kutumia fedha kutoka UNICEF. Ni sehemu iliyojengwa kwa watoto wakimbizi kuweza kuonana, kwa sababu watoto wanaofika hapa tumebaini wana matatizo lukuki. Kuna wale ambao wameshuhudia wazazi wao wakiuawa, na kuna wale walioshuhudia nyumba zao zikichomwa moto, mali zao zikiporwa na hili limewapatia kiwewe.”

Katika kituo hiki kuna wafanyakazi ambao wanasaidia watoto kujifunza mambo kupitia mbinu mbali mbali kama vile nyimbo na michezo huku baadhi ya watoto wakiwa na wazazi wao.

Bi. Dhedza akafafanua pia kuhusu huduma kama zile za kisaikolojia na kwamba, “tuna michezo pia. Wazo lilikuwa kwamba, tunaweza kubaini watoto wasioambatana na wazazi wao. Pindi kuna mtoto ambaye amekuja peke yake, tunafanya utafiti hadi pale anaweza kuunganishwa na familia yake.”

Kutokana na kushamiri kwa ghasia jimboni Ituri, UNICEF inasema inaendelea kuhakikisha uwepo wake nchini DRC na kuendesha operesheni za kuokoa maisha hasa jimboni humo  kupitia ushirikiano na wadau mbalimbali, lakini limesema mahitaji ya watu ni makubwa na yanaendelea kuongezeka.