UNMISS yaondolea wanafunzi Yambio adha ya kusomea chini ya miti

Get monthly
e-newsletter

UNMISS yaondolea wanafunzi Yambio adha ya kusomea chini ya miti

UN News
25 June 2020
By: 
Wanafunzi wakisomea chini ya mti, Hudaydah, Yemen.
UNICEF/UN0153963/Obadi
Wanafunzi wakisomea chini ya mti, Hudaydah, Yemen.

Nchini Sudan Kusini, ujumbe wa Umoja wa Mataifa UNMISS umewaondolewa wanafunzi wa eneo moja mjini Yambio jimboni Equitoria Magharibi adha ya kusomea chini ya mti kwa kuwajengea madarasa ambamo watasomea bila bughudha yoyote

Uamuzi wa UNMISS umefanyika baada ya doria zao za mara kwa mara eneo hilo, kuwakutanisha na watoto wenye ari ya kujifunza lakini hawakuwa na madarasa na hivyo kulazimika kusomea chini ya miti.

Wakazi wa maeneo hayo ya Bazumburu na Sakure yaliyopo kilometa 35 kutoka mjini Yambio, walihama kufuatia vita vya wenyewe kwa wenyewe vilivyoanza Desemba mwaka 2013, lakini kufuatia makubaliano mapya ya amani yam waka 2018, wakazi wameanza kurejea nyumbani, lakini changamoto bado ni malazi na maeneo ya kusomea.

Walinda amani kupitia mradi wa matokeo ya haraka wa UNMISS, QIP, waliona njia ya kuimarisha zaidi amani ni kujenga shule ambapo afisa wa ulinzi wa UNMISS, Tahiru Ibrahim anasema kuwa, “kila wakati tunapita, tuliona watoto wanasomea chini ya miti na tukasema hili halikubaliki katika karne hii ya 21 ambapo mtu unaweza kuwa na miundombinu ya shule. Na ari ya wanafunzi na kujitolea kwa walimu navyo vilitupatia hamasa. Kwa hiyo tuliamua kuungana na jamii na tukabaini pia idadi kubwa ya watoto na wazazi wamerejea kwenye makazi ya wakimbizi wa ndani.”

Ingawa bado kuna maeneo machache ya mivutano, UNMISS iliona kwamba ni muhimu kuwapatia watoto fursa kwenye eneo ambalo wanaweza kustawi zaidi hivyo Moses Baggari, afisa ulinzi na ustawi wa watoto, , UNMISS anasema kuwa, “Sudan Kusini iko kwenye mazingira ya vita lakini huwa tunasema kila siku ya kwamba hebu tumpatie mtoto kalamu na kitabu badala ya risasi na bunduki.”

Hatua ya UNMISS iliungwa mkono na jamii ambayo ilijitokeza kwenye msaragambo, wanawake wakibeba maji kusaidia kujenga shule ya watoto wao. Mary Sebit mmoja wa wakazi hao anasema kuwa, “ tunajaribu kuteka maji ili shule ijengwe kwa sababu tumechoka. Hakuna madarasa kwa watoto wetu kusomea. Mvua ikinyesha, wanarejea nyumbani huku madaftari na vitabu vikiwa vimelowa.”

Mamlaka za eneo hili nazo zimeunga mkono hatua hii kama asemavyo Joseph Aquto ya kwamba, “sisi katika Wizara ya Elimu tuna furaha kwa sababu shule hii itakuwa mazingira bora kwa watoto kusoma bila bugudha yoyote.”

Kwa UNMISS, mradi huu ni wa kujenga amani ya kudumu kwa kizazi cha sasa na vijavyo ambapo Bwana Ibrahim anasema kuwa, “tumejizatiti kuendelea kusaidia watu wa Sudan Kusini katika kusaka amani ya kudumu na pia kuimarisha ustawi wa kijamii na kiuchumi.”

Kila shule iliyopo Sakure na Bazumburu imejengewa darasa na choo, hali ambayo itakuwa mujarabu kwa eneo hili ambalo uzoefu wa miezi 9 ya mvua sasa hautalazimu wanafunzi kukimbilia nyumbani bali wataendelea kusoma na hivyo kuwa na uhakika wa mustakabali bora wao na familia zao.