Ukeketaji unaathiri wasichana na wanawake na gharama ya matibabu ni dola bilioni 1.4 kwa mwaka kimataifa --WHO

Get monthly
e-newsletter

Ukeketaji unaathiri wasichana na wanawake na gharama ya matibabu ni dola bilioni 1.4 kwa mwaka kimataifa --WHO

UN News
6 February 2020
By: 
Mwanamke akiwa ameshikilia kisu kilichotumika kwenye ukeketaji.
UNICEF/Catherine Ntabadde
Mwanamke akiwa ameshikilia kisu kilichotumika kwenye ukeketaji.

Wakati dunia ikiadhimisha siku ya kutokomeza ukeketaji, shirika la afya ulimwenguni, WHO limesema kitendo hicho kinadhoofisha uchumi pamoja na nguvu kazi.

WHO imesema sio tu kwamba ukeketaji ni ukiukaji wa haki za binadamu lakini unaathiri afya kimwili na kiakili kwa mamilioni ya wasichana na wanawake na pia kutumia raslimali nyingi muhimu za nchi na kwamba uwekezaji zaidi unahitajika kumaliza ukeketaji na madhila unaosababisha.

Kwa mujibu wa makadirio mapya gharama ya matibabu kutokana na athari za ukeketaji huenda ikafika dola bilioni 1.4 kimataifa kwa mwaka iwapo mahitaji yote ya kiafya yatashughulikiwa. Katika nchi binafsi, gharama hii inakaribia asilimia 10 ya matumizi ya mwaka mzima ya afya kwa wastani ambapo katika baadhi ya nchi idadi hii huenda ikafika asilimia 30.

WHO imesema wanawake na wasichana waathirika wa ukeketaji wanakabiliwa na hatari kubwa katika afya yao na uzima, hii ni pamoja na athari pindi tu baada ya kukeketwa ikiwemo: maambukizi, kuvuja damu nyingi au kiwewe pamoja na magonjwa ya muda mrefu ambayo huenda yakatokea maishani.

Pia wanawake ambao wamekeketwa wana uwezekano mkubwa wa kupata tishio la kupoteza maisha wakati wa kujifungua, kukabiliwa na magonjwa ya akili na maambukizi ya muda mrefu.

Pia huenda wakahisi uchungu wakati wa hedhi, wakienda haja ndogo au wakati wa kitendo cha kujamiana. Abida Dawud ni mmoja wa waathirika wa ukeketaji akiwa eneo la Afar nchini Ethiopia.

(Sauti ya Abida)

“Mimi ni manusura wa ukeketaji, niña watoto wane, wavulana wawili na wasichana wawili, kazi yangu kubwa ni kutoa mafunzo kuhusu madhara ya ukeketaji. Tunawaambia akina mama na wasichana kwamba ukeketaji una madhara kwa wasichana wetu na kwetu sisi, huenda sehemu ya mwili wangu ilichukuliwa lakini siwezi kamwe kutoa moyo wangu. Ndani ya moyo wangu ninawaza ni jinsi gani tunaweza kutomeza ukeketaji.”

Kwa upande wake manusura mwingine wa ukeketaji Khadija Mohammed kutoka eneo hilo la Afar pia amesema,

(Sauti ya Khadija)

“Iwe ni kwa kutangaza kwenye radio au televisheni au kuzungumzwa na watu wa Afar, ujumbe ni kutokomeza ukeketaji, iwapo hatutatokomeza kitendo hicho basi vizazi vijavyo vitaendeleza ukeketaji. Ni lazima tuusitishe hapa.”

Kwa kutumia takwimu za nchi 27 zilizo na visa vingi vya ukeketaji, makadirio ya kiuchumi yanaonesha faida za wazi za kiuchumi kufuatia kutokomeza ukeketaji. Iwapo kitendo hicho kitatokomezwa zaidi ya asilimia 60 kutokana na gharama za kiafya zingeweza kuokolewa.

Tangu mwaka 1997 hatua zimepigwa katika kutokomeza ukeketaji kupitia kazi ndani ya jamii, utafiti na marekebisho katika sheria na será. Nchi 26 barani Afrika na Mashariki ya kati zimeweka sheria ya wazi dhidi ya ukeketaji, pamoja na nchi 33 zilizo na wahamiaji kutoka nchi kunakofanyika vitendo vya ukeketaji.

Ukeketaji unatambulika kama ukiukaji wa haki za binadamu na hauna faida zozote za kiafya na unasababisha madahra. WHO inashikilia msimamo wake kwamba ukeketaji haupaswi kutekelezwa wakati wowote.