Tanzania na Kenya miongoni mwa wanufaika wa fuko la mazingira duniani, GEF

Get monthly
e-newsletter

Tanzania na Kenya miongoni mwa wanufaika wa fuko la mazingira duniani, GEF

UN News
11 June 2020
By: 
Miradi kama hii ya FAO ya kutengeneza maeneo ya kunywa maji wanyama huko Turkana nchini Kenya, ni miradi ya kuepusha mvutano kati ya wakulima na wafugaji na pia hutunza mazingira. (2011)
FAO/Kenya Team
Miradi kama hii ya FAO ya kutengeneza maeneo ya kunywa maji wanyama huko Turkana nchini Kenya, ni miradi ya kuepusha mvutano kati ya wakulima na wafugaji na pia hutunza mazingira. (2011)

Shirika la Umoja wa Mataifa la chakula na kilimo, FAO,  hii leo limekaribisha hatua ya fuko la mazingira duniani, GEF, ya kutenga dola milioni 174 kwa ajili ya miradi 24 inayoshughulikia shaka na shuku za kilimo na mazingira katika mataifa 30 duniani.

Taarifa ya FAO iliyotolewa leo mjini Roma, Italia imesema kuwa hatua hiyo imetangazwa wakati wa mkutano wa 58 wa GEF uliofanyika kwa njia ya mtandao, ikiwa ni mara ya kwanza kutokana na janga la Corona au COVID-19.

Miradi hiyo inajikita kwenye madhara ya majanga ya mazingira katika kilimo ambapo miradi minne huko Nicaragua, Guinea, Kenya na Uzbekistan itachangia katika mifumo ya chakula, matumizi na uhifadhi wa ardhi ,miradi ambayo inafadhiliwa na GEF.

Ukiwa unasimamiwa na Benki ya Dunia, mfuko huu unalenga kutunza bayonuai kwa kujumuisha mifumo ya uzalishaji kwa mapana zaidi.

Mathalani katika mradi mmoja nchini Tanzania, ulioanzishwa mwaka 2019 ukisimamiwa na shirika la chakula na kilimo la Umoja wa Mataifa, FAO, kinachofanyika ni kushughulikia mmomonyoko wa udongo na mifumo anuai katika ardhi zenye ukame.

Katika miradi mingine minne, FAO itaweza kusaidia serikali katika mataifa 9 yasiyo na bahari, visiwa vidogo na zile za mataifa yanayoendelea, kukabiliana na hatari za kipekee za kimazingira kutokana na maeneo ambako nchi hizo zinapatikana.

Akizungumzia hatua hii, Mkurugenzi Mkuu wa FAO, Qu Dongyu amesema, “miradi hiyo iliyopitishwa imebuniwa kwa lengo la kuimarisha mifumo ya chakula ya kitaifa huku ikizingatia uhifadhi wa mazingira kwa maslahi ya binadamu na sayari dunia. Hii itasaidia wakulima, wavuvi, na waendeleza wadogo wa misitu ili kupanua wigo wa njia zao za kujipatia kipato na kuongeza pia mneo kwa madhara ya mabadiliko ya tabianchi na ugonjwa wa virusi vya Corona au COVID-19.”

Tangu kuwa wakala wa GEF tangu mwaka 2006, FAO imeshasaidia zaidi ya serikali 130 na kutekeleza zaidi ya miradi 200 yenye thamani ya mabilioni ya dola ambayo hadi sasa imenufaisha takribani wanawake na wanaume wapatao milioni 5.