Pamoja na hatua ilizopiga, DRC bado inahitaji kusaidiwa- Leila Zerrougui

Get monthly
e-newsletter

Pamoja na hatua ilizopiga, DRC bado inahitaji kusaidiwa- Leila Zerrougui

UN News
By: 
Leïla Zerrougui, cheffe de la Mission des Nations Unies en République démocratique du Congo (MONUSCO) devant le Conseil de sécurité.
UN Photo/Loey Felipe
Leila Zerrougui akilihutubia Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa.

Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa leo limekuwa na kikao maalum mjini New York Marekanikujadili hali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC ambapo, mwakilishi maalum wa Katibu Mkuu nchini DRC ambaye pia ni mkuu wa ujumbe wa  Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini humo, MONUSCO , Leila Zerrougui amewaeleza wajumbe kuhusu hali ya sasa ya DRC.

Bi Zerrougui pamoja na kupongeza hatua ya hivi karibuni iliyooneshwa na DRC katika uchaguzi na kukabidhiana madaraka kwa amani, amesema bado kuna maeneo mengi ambayo yanatakiwa kuangaziwa na kufanyiwa kazi hususani suala la usalama.

Mathalani ameeleza kuhusu hali ya Kivu Kaskazini ambako pia kwa sasa mlipuko mkubwa wa Ebola ambao ni wa pili kwa ukubwa katika historia ya ugonjwa huo unaendelea, makundi ya ADF na Mai-Mai yanaendelea kuwashambulia raia kama wanavyofanya FARDC na pia katika baadhi ya matukio wakiwashambulia wafanyakazi wa MONUSCO, “kufuatia mashambulizi dhidi ya vituo vya kudhibiti Ebola kule Butembo na Katwa, MONUSCO imetuma tena askari na wafanyakazi wengine ili kusaidia usalama wa wafanyakazi wa vituo vya kudhibiti Ebola pia operesheni na hata juhudi za kuzungumza na jamii ili kutatua hali ya kugomea vita dhidi ya Ebola.” Bi Zerrougui amesema.

Aidha Bi Zerrougui amewaeleza wajumbe wa Baraza la Usalama kuwa hivi sasa nchini DRC maandalizi ya uchaguzi yanaendelea katika uchaguzi unaotegemewa kufanyika mwishoni mwa mwezi huu kwenye maeneo ambayo kutokana na sababu za kiusalama na kiafya hayakuweza kushiriki katika uchaguzi uliopita, “tutafanya kila linalowezekana kuzuia jambo lolote linaloweza kusababisha vurugu katika kipindi hiki nyeti cha kisiasa.”

Akionesha namna ambayo vurugu zinaweza kuleta madhara makubwa zisipodhibitiwa, Bi Zerrougui amekumbushia vurugu za Yumbi zilizotokea Desema 2018 na kusababisha vifo 535, majeruhi 111 na watu 19,000 kupoteza kubaki bila makazi.

Aidha ameliomba Baraza la Usalama kuendelea kusaidia juhudi ambazo zimefikiwa hivi sasa na serikali ya DRC ili iweze kutimiza matarajio ya wananchi.

Kwa upande wake Balozi Dian Triansyah Djan ambaye ni mwakilishi wa kudumu wa Jamhuri ya Indonesia katika Umoja wa Mataifa amempongeza Bi Zerrougui kwa kazi nzuri anayoifanya nchini DRC na pia akaipongeza kazi kubwa ya MNUSCO hivyo akaomba kuwa ni muhimu waungwe mkono ili waweze kufanikisha kazi zao, “kwa kusikia mafanikio ambayo yamefikiwa na pia changamoto ambazo bado zipo, ni wazi kuwa kazi ya MONUSCO ni dhahiri na mchango wa MONUSCO ni wa muhimu nchini DRC hivi sasa kuliko wakati mwingine wowote.”