Msaada zaidi kwa Tanzania wahitajika ili ihudumie vyema wakimbizi- Grandi

Get monthly
e-newsletter

Msaada zaidi kwa Tanzania wahitajika ili ihudumie vyema wakimbizi- Grandi

UN News
By: 
Soko la pamoja ambako wakimbizi kutoka Burundi na DR Congo wanaweza kukutana na wenyeji watanzania walio jirani na kambi ya wakimbizi ya Nyarugusu wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma nchini Tanzania. Picha: UNHCR/Georgina Goodwin
Picha: UNHCR/Georgina Goodwin. Kamishna Mkuu wa shirika la wakimbizi duniani, UNHCR Filippo Grandi akizungumza na mwanamke aliyebeba mwanae kwenye kambi ya wakimbizi ya Nyarugusu wilayani Kasulu, mkoani Kigoma nchini Tanzania tarehe 7 Februari 2019
Picha: UNHCR/Georgina Goodwin. Soko la pamoja ambako wakimbizi kutoka Burundi na DR Congo wanaweza kukutana na wenyeji watanzania walio jirani na kambi ya wakimbizi ya Nyarugusu wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma nchini Tanzania.

Kamishna Mkuu wa shirika la wakimbizi la Umoja wa Mataifa ,UNHCR, Filippo Grandi amehitimisha ziara yake ya siku nne nchini Tanzania akitoa wito kwa jamii ya kimataifa kuwekeza zaidi mikoa ya kaskazini-magharibi mwa nchi hiyo ambayo ni nyumbani kwa wakimbizi 330,000. 

Ziara hiyo ya siku nne ilimfikisha Bwana Grandi kwenye kambi ya Nyarugusu wilayani Kasulu mkoani Kigoma nchini Tanzania ambako alishuhudia jinsi wakimbizi walivyo na matumaini licha ya kuishi ugenini.

Akiwa kambini alikutana na mkimbizi kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC Selemani Boaz ambaye ni mchuuzi kambini humo na akimweleza kuwa soko hilo linasaidia utangamano na wenyeji na pia wakimbizi wanapata vyakula tofauti na vile vya msaada.

Kisha alijerejea Dar es salaam ambako alizungumza na waandishi wa habari akipongeza jinsi taifa hilo la Afrika Mashariki lilivyoendelea kuwa pepo ya wale wanaokimbia ghasia nchini mwao, akisema,  “ni muhimu kwamba hakuna tu anayelazimishwa kurejea nyumbani na zoezi la kurejea ni la hiari. Tunaomba usaidizi zaidi wa kimataifa ili kuhakikisha wakimbizi wanaorejea nyumbani kwa hiari wanaweza kutangamana na jamii zao na pia kusaidia kuwezesha ufuatiliaji kwa kuwa hivi sasa fedha hazitoshelezi.”’

Naye Naibu Mwakilishi wa UNHCR nchini Tanzania Zephania Amuiri amezungumzia huduma kambini akigusia huduma ya afya akisema kwa magonjwa kama vile saratani na afya ya akili huwa wanaomba kuhamishia wagonjwa kwenye hospitali kama vile Bugando mkoani Mwanza na Muhimbili jijini Dar es salaam.

Hata hivyo amesema wakati mwingine wanaomba madaktari mabingwa wafike kambini ili kutoa huduma kwa wakimbizi wengi zaidi.