Mchango wa vijana unahitajika katika kufanikisha ajenda ya 2030-Ripoti

Get monthly
e-newsletter

Mchango wa vijana unahitajika katika kufanikisha ajenda ya 2030-Ripoti

UN News
By: 
Vijana wa kike na wa kiume wanashiriki kwenye programu za kuelimisha umma kuhusu madhara ya ukeketaji na wito unaotolewa juu ya utekelezaji wa lengo namba 5 la malengo ya maendeleo endelevu, SDGs linalotaka usawa wa kijinsia. Picha: Warren Bright/UNFPA TZ
Picha: Warren Bright/UNFPA Tanzania. Vijana wa kike na wa kiume wanashiriki kwenye programu za kuelimisha umma kuhusu madhara ya ukeketaji na wito unaotolewa juu ya utekelezaji wa lengo namba 5 la malengo ya maendeleo endelevu, SDGs linalotaka usawa wa ki
Picha: Warren Bright/UNFPA Tanzania. Vijana wa kike na wa kiume wanashiriki kwenye programu za kuelimisha umma kuhusu madhara ya ukeketaji na wito unaotolewa juu ya utekelezaji wa lengo namba 5 la malengo ya maendeleo endelevu, SDGs linalotaka usawa wa kijinsia.

Umoja wa Mataifa leo umezindua leo ripoti yake ya kimataifa kuhusu vijana, ikisema ushirikiswhwaji wa vijana bilioni 1.2 wenye umri wa kati ya miaka 15 hadi 24  ni muhimu katika kufanikisha jamii endelevu, jumuishi na thabiti.

Ikipatiwa  jina Vijana na ajenda ya 2030 kwa ajili ya maendeleo endelevu, ripoti hiyo  imeangazia vijana  hao ambao ni asilimia 16 ya idadi ya watu wote duniani.

Kwa mujibu wa ripoti iliyoandaliwa na idara ya uchumi na masuala ya kijamii, DESA ya Umoja wa Mataifa, vijana wanaweza kuchangia katika kuepusha hatari na changamoto zinazokabili utekelezaji wa malengo ya maendeleo endelevu,SDGs, ikiwemo athari za mabadiliko ya tabianchi, ukosefu wa ajira, umasikini, ukosefu wa usawa wa kijnsia, mizozo na uhamaji.

Hata hivyo ripoti inasema vijana, licha ya kwamba wana uwezo mkubwa bado wanakabiliwa na elimu duni ambayo kiwango chake ni cha chini kuweza kuajiriwa  katika viwango vinavyokubalika.

Mathalani vijana milioni 142 walioko vidato vya juu katika shule za sekondari hawahudhurii shule na katika ajira vijana milioni 71 hawana ajira na wengine wengi wakiwa katika ajira zisizo na uhakika au zisizo rasmi.

Ripoti imeonyesha kuwa kuna tofauti baina ya nchi na nyingine katika masuala ya elimu na ajira huku waathirika wakubwa wakiwa ni wanawake, watu masikini zaidi, walio vijijini na wahamiaji au wakimbizi. 

Ili kubadili mwelekeo wa sasa, ripoti imependekeza nchi wanachama na wadau kutathmini hatua zilizopigwa, kuchunguza pengo kwenye sera na namna ya kurekebisha.

Ripoti imependekeza sera zipangwe kwa kuzingatia matakwa ya vijana kuanzia ngazi ya kitaifa hadi mashinani, pia kubuni programu zinazolenga vijana katika maeneo wanakoishi, kutambua haki za vijana na maendeleo yao kwa kuzingatia kwamba wana ndoto zao ambazo wangependa kutimiza.

Aidha kutumia takwimu za sasa na kutumia ujuzi wa vijana na uzoefu wao katika kupanga, kutekeleza na kutathmini sera za vijana.