Mamilioni ya watoto hawataweza kusomea nyumbani -UNICEF

Get monthly
e-newsletter

Mamilioni ya watoto hawataweza kusomea nyumbani -UNICEF

UN News
5 May 2020
By: 
Balozi wa amani akizungumza na wanafunzi katika shule mjini Kinshasa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo DRC , kuhusu kuchagiza amani na usawa wa kijinsia
MONUSCO/Dominique Cardinal
Balozi wa amani akizungumza na wanafunzi katika shule mjini Kinshasa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo DRC , kuhusu kuchagiza amani na usawa wa kijinsia

Taarifa ya shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF, iliyotolewa leo mjini Nairobi Kenya na Johannesburg Afrika Kusini, imeeleza kuwa zaidi ya watoto milioni 127 wa shule za awali, shule za msingi na sekondari Afrika Mashariki na Kusini, ambao walitakiwa kurejea shuleni wiki hii, wanasalia nyumbani kutokana na mlipuko wa ugonjwa wa COVID-19.

 Katika Kushughulikia hali hiyo, UNICEF imetangaza usaidizi zaidi kwa janga hili la elimu ambalo halijawahi kutokea, wakati ikiendelea kupigia upatu ufunguzi wa shule unaozingatia mwongozo wa usalama.

"Katika maeneo mengi ya dunia, kujifunzia nyumbani kumesaidiwa na zana za mtandaoni. Hata hivyo katika maeneo ya Afrika Mashariki na Kusini, kupenya au kusambaa kwa intaneti ni kugumu, ambapo ni kaya moja tu kati ya tano sawa na asilimia 22 ambao wana intaneti, wakati asilimia 84 ya watu wa vijijini ambako idadi kubwa ya wanafunzi wanapatikana, hawana umeme.” Imeeleza taarifa hiyo.

Kwa hivyo, UNICEF imekuwa ikifanya kazi muda wote na washirika kusaidia kuendelea kujifunza kupitia njia kama vile redio, ujumbe mfupi wa simu na maandashi ya kuchapishwa.

UNICEF tayari,kupitia wadau, imezisaidia serikali zaidi ya dola milioni 5.4 kwa ajili ya masomo na pia kwa ajili ya maandalizi ya kuzifungua shule huku ufadhili zaidi ukiwa katika mipango.

Taarifa imeendelea kueleza kuwa, “hata hivyo, hata hatua mbadala za ujifunzaji zinazofanywa na Serikali, UNICEF na wadau, mamilioni ya watoto hayatafikiwa. Kwa mfano, redio hufikia watoto wapatao milioni 53, au watoto wanne katika katika maeneo ya Mashariki na Kusini mwa Afrika. Wale ambao hawafikiwi mara nyingi huwa watoto walio katika mazingira yaliyotengwa sana  au walioko katika mazingira magumu ambao hutegemea sana shule kwa elimu yao, afya, usalama na lishe. Kwa kweli, athari za COVID-19 na kufungwa kwa shule ni mbaya: kwa Afrika Mashariki na Kusini, hadi kufikia watoto milioni 16 hawapati tena milo muhimu ya kila siku shuleni na unyanyasaji unaongezeka.”

Kwa maana hiyo UNICEF inakaribisha mwongozo mpya wa kiufundi uliopewa jina "Mfumo wa kufungua Shule" ambao unatoa muundo wa kufungua upya shule, na uliandaliwa pia kwa ushirikiano wa WFP, Benki ya dunia, Shirika la elimu, sayansi na utamaduni UNESCO na UNICEF yenyewe.