Dexamethasone waachiwe wagonjwa mahututi wa COVID-19, kulikoni?

Get monthly
e-newsletter

Dexamethasone waachiwe wagonjwa mahututi wa COVID-19, kulikoni?

UN News
19 June 2020
By: 
Mgonjwa akifikishwa katika hospitali ya Mount Sinai huko Astoria jijini New York, Marekani
UN Photo/Evan Schneider
Mgonjwa akifikishwa katika hospitali ya Mount Sinai huko Astoria jijini New York, Marekani

Shirika la afya la Umoja wa Mataifa, WHO, limekaribisha matokeo ya awali uchunguzi unaoonesha kuwa dawa ya Dexamethasone, inaweza kuokoa maisha ya wagonjwa mahututi wa Corona au COVID-19.

Akizungumza na waandishi wa habari hii leo mjini Geneva, Uswisi, Mkurugenzi Mkuu wa WHO, Dkt. Tedros Ghebreyesus kuwa uchunguzi huo umefanywa nchini Uingereza ambapo “kwa wagonjwa waliokuwa wanahitaji Oksijeni, walipopatiwa dawa hiyo, mgonjwa mmoja kati ya watano alipona, ilhali kwa wale wanaohitaji mashine ya kusaidiwa kupumua, mgonjwa mmoja kati ya watatu alipona baada ya kupatiwa dawa hiyo.”

Dexamethasone, ni dawa ambayo imekuwa ikitumika tangu miaka ya 1960 ili kupunguza uvimbe katika mazingira mbalimbali ikiwemo ile ya saratani. 

WHO inasema kuwa, “dawa hiyo hivi imekuwepo kwenye orodha ya WHO ya dawa muhimu tangu mwaka 1977 na haina tena hataza kwa hiyo inapatikana kwa bei nafuu katika nchi nyingi.”

Dexamethasone haitibu virusi!

Hata hivyo, Dkt. Michael Ryan, Mkurugeni Mtendaji wa programu ya dharura, WHO amesema kuwa, “ni muhimu sana dawa hii ikatumiwa chini ya uangalizi mkubwa wa kitabibu. Matumizi yake si kwa mazingira ya kati ya ugonjwa. Hii siyo prophylaxis. Hii ni dawa kali sana ya kupunguza uvimbe. Inaweza kuokoa wagonjwa ambao hali yao iko mahututi sana ambao mapafu na mfumo wao wa moyo kuzunguka mapafu umevimba. Kwa hiyo hii inawezesha wagonjwa waendelee kupata oksijeni kwenye mfumo wa damu kutoka kwenye mapafu katika kipindi muhimu sana kwa kupunguza haraka uvimbe wakati wa kipindi hatari cha ugonjwa.”

Amesisitiza kuwa Dexamethasone si tiba ya virusi vyenyewe, “ni kwamba dawa za kupunguza uvimbe, hasa zile zenye nguvu kubwa zinaweza kuhusishwa na kuongezeka maradufu kwa virusi kwenye mwili wa binadamu. Ni muhimu sana dawa hii ikaachiwa wagonjwa mahututi ambao wanaweza kunufaishwa nayo.”

Watafiti wamesema kuwa taarifa kwa kina matokeo kuhusu majaribio hayo pamoja na uchambuzi wake vitachapishwa siku chache zijazo.

Hadi tarehe 16 mwezi huu wa Juni, zaidi ya watu 440,000 duniani kote wamefariki dunia kutokanana COVID-19.