Afrika ni chanzo cha masuluhisho, Rwanda tuko tayari kufanya sehemu yetu-Paul Kagame

Get monthly
e-newsletter

Afrika ni chanzo cha masuluhisho, Rwanda tuko tayari kufanya sehemu yetu-Paul Kagame

UN News
25 September 2019
By: 
Paul Kagame, President of the Republic of Rwanda, addresses the general debate of the General Assembly’s seventy-fourth session. 24 September 2019
UN Photo/Cia Pak
Rais Paul Kagame wa Jamhuri ya Rwanda akihutubia mjadala mkuu wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa jijini New York, Marekani tarehe 24 Septemba 2019

Rais Paul Kagame wa Rwanda ameitumia hotuba yake katika mjadala mkuu wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, UNGA74 mjini New York hii leo, kueleza kuwa Afrika inaweza pia kuwa chanzo cha masuluhisho ya matatizo yanayoukabili ulimwengu.

Rais Kagame amelifahamisha Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kuwa katika wiki za hivi karibuni, nchi yake Rwanda itawapokea wakimbizi kutoka Libya, na kisha akawautambua mchango wa Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi na pia Muungano wa Ulaya katika kufanikisha tukio hilo.

“Afrika pia ni chanzo cha masuluhisho. Rwanda tuko tayari kufanya sehemu yetu," amesema Rais Kagame.

Aidha akielezea kuhusu jinsi Rwanda inavyotekeleza malengo ya maendeleo endelevu SDGs, Rais Kagame amesema katika suala la afya Rwanda imejizatiti kwa upande wa kuhakikisha kila mtu anapata uhakika wa matibabu akisema, “hivi sasa asilimia 90 ya watu nchini Rwanda wana bima ya afya. Hii imeboresha matokeo ya kiafya. Pia hii inaonesha kuwa nchi bila kujali viwango vya uwezo wao wanaweza kulifanikisha hili.”

Bwana Kagame pia amesema kuwa mwezi Julai mwaka ujao wa 2020 Afrika itaanza utekelezaji wa wa eneo huru la biashara barani humo (AfCFTA). AfCFTA inalifanya bara la afrika kuwa ndilo kubwa zaidi kwa eneo huru la biashara duniani likiwa na nchi 54 na jumla ya watu bilioni 1.2.

Akihitimisha hotuba yake, Bwana Kagame amewaalika viongozi wenzake kuhudhuria mkutano wa dunia kuhusu masuala ya kijinsia yaani Global Agenda Summit utakaofanyika mwishoni mwa mwaka huu mwezi Novemba mjini Kigali Rwanda.

 

Mada: