Afrika magharibi na kati, wasio na uhakika wa chakula wanaweza kuongezeka zaidi ya maradufu kutokana na COVID-19

Get monthly
e-newsletter

Afrika magharibi na kati, wasio na uhakika wa chakula wanaweza kuongezeka zaidi ya maradufu kutokana na COVID-19

UN News
6 July 2020
By: 
Ulinzi wa raia ni agizo muhimu kwa shughuli nyingi za kulinda amani za Umoja wa Mataifa pamoja na Jamhuri ya Afrika ya Kati.
UN Photo/Herve Serefio
Ulinzi wa raia ni agizo muhimu kwa shughuli nyingi za kulinda amani za Umoja wa Mataifa pamoja na Jamhuri ya Afrika ya Kati.

WFP kupitia msemaji wake hii leo mjini Geneva Uswisi limesema changamoto za kijamii na kiuchumi zilizoletwa na njia zilizolenga kudhibiti kusambaa kwa COVID-19, zimeathiri kwa kiasi kikubwa uhakika wa chakula Afrika ya kati na magharibi.

WFP inakadiria kwamba idadi ya watu wasio na uhakika wa chakula katika eneo hilo la Afrika inaweza kuongezeka zaidi ya maradufu hadi milioni 57.6 kufikia mwishoni mwa mwaka.

“Kufungwa kwa mipaka na kuzuia kwa maghulio ya kila wiki na masoko ya wazi katika ukanda huu yamesababisha kupungua kwa biashara na kuwazuia wakulima kuuza bidhaa zao, wakati mwingine kusababisha uhaba wa vyakula vinavyopatikana katika maeneo haya na hata kupanda kwa bei.  Ongezeko la bei kati ya asilimia 15 hadi 25 lilishuhudiwa mwezi Aprili katika Jamhuri ya Afrika ya Kati, Chad na Nigeria."  Ameeleza Msemaji Mkuu wa WFP, Elisabeth Byrs. 

Kwa mujibu wa WFP, COVID-19 ilijitokeza katika kipindi ambacho njaa na utapiamlo ulikuwa katika kiwango cha juu.

WFP na UNICEF wanakadiria kuwa watoto milioni 11.6 wanaweza kupata utapiamlo mkali katika ukanda huo wa Afrika Magharibi na Afrika ya kati katika mwaka huu wa 2020 kutokana na madhara ya janga la virusi vya corona ikiwa ni ongezeko la asilimia 18 la hali ivyokuwa kabla ya janga la ugonjwa huo.

WFP ilikuwa inapanga kuwasaidia watu milioni 23 katika eneo hilo la Afrika kwa kuwapatia vyakula vya kuokoa maisha na msaada wa lishe. Hiyo ni ongezeko la watu milioni 8.9 katika mpango wa awali mwanzoni mwa mwaka huu.