Mfumo mpya wa malipo wa Afrika yote wawapa wanabiashara wa Afrika kitulizo

Get monthly
e-newsletter

Mfumo mpya wa malipo wa Afrika yote wawapa wanabiashara wa Afrika kitulizo

Uzinduzi wa PAPSS utaokoa dola bilioni 5 kila mwaka na kupiga jeki biashara kati ya mataifa ya Afrika
Kingsley Ighobor
2 Novemba 2021

Wakati Fidelis Adele, Afisa Mkuu Mtendaji wa kampuni ya uchapishaji na mawasiliano iliyoko mjini Freetown, Solid Graphics, alipohitaji kuagiza vifaa vya uchapishaji kutoka Nijeria mwezi wa Septemba, alilipa $ 165 zaidi juu ya $10,000 malipo kwa muuzaji kupitia kwa benki. Ilhali ilichukua siku tatu kwa pesa zilizotumwa kutoka Sierra Leone kuwekwa katika akaunti ya mpokezi nchini Nijeria. 

“Nililipa $30 kama gharama ya huduma, $35 kama gharama ya SWIFT na $100 zaidi kama gharama ya benki,” Bw. Adele aliiambia AfrikaUpya. SWIFT inasimamia Society for Worldwide Interbank Financial Telecommunication, mtandao wa ulimwengu unaofanikisha mchakato wa malipo ya kimataifa.

Bw. Adele hakutaka kujaribu kutumia kampuni za huduma za kifedha kama Western Union au MoneyGram kwa kuwa “viwango vya ubadilishaji wa fedha vya kampuni hizo ni vibovu mno.” 

Chaguo jingine lilikuwa asafiri Lagos kwa ndege, safari ya saa tatu, akiwa amebeba pesa. “Nimefanya hivyo mara chache,” alisema, “ila si nafuu isipokuwa tu kama ni pesa nyingi, na ni hatari.”

Wanabiashara kote frika wanapata shida kama hizi kulipia bidhaa au huduma baina ya mipaka ya kitaifa. Katika mchakato huu, wanapoteza fedha na muda wa thamani.

Mchakato huu wa kuudhi na wa kupoteza muda “unatugharimu [Waafrika] takriban dola bilioni 5 katika [kutuma pesa] malipo kila mwaka,” kulingana na Benedict Oramah, Rais wa African Export-Import Bank (Afreximbank), katika mahojiano na AfrikaUpya. “Sisi ni bara maskini. Hatustahili kupoteza pesa hivyo.”

Mfumo wa kulipa wazinduliwa

Ili kuikabili hali hii, Afreximbank imeshirikiana na Ofisi ya Soko Huru la Bara Afrika (AfCFTA) kuzindua Mifumo ya Malipo ya Mwelekeo wa Afrika (Pan-African Payments and Settlement Systems) (PAPSS), ukumbi unaowezesha malipo katika mataifa tofauti kwa fedha za taifa husika mara moja.  

Mfumo wa PAPSS umefanyiwa majaribio kwa ufanisi katika mataifa sita ya Ukanda wa Kifedha wa Afrika Magharibi (WAMZ)—Nijeria, Gambia, Sierra Leone, Liberia, Ghana na Guinea. Kwa sababu ya wingi-fedha na uwililugha wake, WAMZ inachukuliwa kama kanda inayosawiri sifa sawa katika bara hili.

Kuhusu kutumia WAMZ kwa majaribio, Prof. Oramah anasema: “Mataifa sita ya WAMZ yana sarafu tofautitofauti. Moja kati ya mataifa hayo linatumia Kifaransa na mengine Kiingereza. Una uchumi mkuu kama Nijeria na pia una chumi ndogo mno.  Kwa hivyo, lolote linaloweza kuharibika katika kanda nyingine ya Afrika litakuwa limeharibika katika WAMZ, na tutakuwa tumefaulu kulikabili katika awamu ya majaribio.”

Uzinduzi wa mfumo wa PAPSS ulitangazwa mwishoni mwa Septemba, kumaanisha kwamba benki kuu za mataifa husika ambazo ndizo mawakala wa kutoa kibali, zinaweza kushirikiana sasa na Afreximbank, ambayo ndio wakala mkuu wa kutoa kibali na mtoaji wa dhamana ya malipo na huduma ya ovadrafti.

Fidelis Adele, Mkurugenzi Mtendaji Solid Graphics, Freetown, Sierra Leone

Afreximbank ilitoa dola milioni 500 kuhudumia Afrika Magharibi na inakusudia dola bilioni 3 zaidi kwa operesheni ya PAPSS katika Afrika nzima.

Wachanganuzi wanatarajia wanabiashara wa Afrika, haswa wale walioko Afrika Magharibi kuanza kutumia ukumbi huu kufikia mwisho wa 2021.

Bw. Oramah, ambaye anafanyia shughuli zake Kairo, Misri, anafafanua changamoto zinazowakabili Waafrika kama zilivyomkabili binafsi: “Ninataka kutuma pesa Nijeria kutoka Misri. Zinapitia katika benki patanifu nje ya Afrika kabla ya kuwasili Nijeria. Ninalipia gharama kabla mtu aliye Nijeria kuzipokea.

“Na zinachukua muda mrefu. Wakati mwingine majuma. Kwa hivyo, sisi [Afreximbank] tulifanya hesabu kujua gharama ya hayo kwa bara—sahau kuhusu muda—yanawagharimu Waafrika dola bilioni 5 kila mwaka. 

“Aidha, kama niko Misri, na ningependa kutazama filamu ninazozienzi za Nollywood, nitahitajika kulipa kwa dola za Marekani. Lakini PAPSS inakubadilishia hayo. Unachohitajika kufanya ni kumlipa mzalishaji wa Nijeria kwa Naira ya Nijeria.”

Afisa Mkuu Mtendaji wa PAPSS Mike Ogbalu asema kwamba katika awamu ya majaribio katika Afrika ya Magharibi, akaunti za benki katika mataifa mbalimbali ziliwekwa na kutolewa pesa kwa dakika 10. Inahakikisha kuhusu kuwepo kwa teknolojia madhubuti inayoweza kushughulikia pesa nyingi.

Jinsi PAPSS inavyofanya kazi

Kutuma pesa kutumia PAPSS ni mchakato wa hatua tano:

  • Hatua ya kwanza ni kutoa agizo la malipo kwa benki yake au kwa mtoa huduma ya malipo.
  • Pili, benki hiyo au mtoa huduma ya malipo anatuma maagizo kwa PAPSS.
  • Tatu, PAPSS inathibitisha agizo la malipo.
  • Nne, pindi agizo linapothibitishwa, PAPSS itatuma agizo hilo kwa benki ya yule anayenufaika na malipo au mtoa huduma malipo.  
  • Mwisho, benki hiyo au mtoa hudma ya malipo analipa pesa zilizotumwa, kwa sarafu za nchi husika, kwa mpokezi.  

Katika kutangaza uzinduzi wa PAPSS, Afreximbank inasema kwamba “kusahilisha malipo kati ya mipaka ya kitaifa na kupunguza utegemezi kwa sarafu halisi kwa malipo hayo, PAPSS inalenga kupiga jeki biashara kati ya mataifa ya Afrika pakubwa.” Kwa sasa biashara kati ya mataifa ya Afrika ni ya asilimia ndogo ya 17.

Mfumo wa PAPSS pia unatarajiwa kusababisha ongezeko la nyongeza ya thamani ya bidhaa, ubunaji wa nafasi za ajira na mapato mengi kwa wanabiashara.

Wamkele Mene, Katibu Mkuu wa Ofisi ya AfCFTA, alisema kwamba PAPSS itasababisha malipo bora ya biashara ya kati ya mipaka ya kitaifa na kuiweka Afrika katika mwelekeo mpya wa kiuchumi.

"Kuna sarafu 42 barani Afrika. Tunataka kuhakikisha kwamba mwanabishara katika Ghana anaweza kutuma cedi za Ghana kwa mwenzake nchini Kenya ambaye atapokea shilingi za Kenya," Bw. Mene aliiambia AfrikaUpya katika mahojianow awali.

Bw. Adele anakubali kwamba PAPSS itaisaidia biashara yake. “Kama ninaweza kupeleka Leones katika benki hapa [Sierra Leone] na kulipia uchapishaji nchini Nijeria, na pesa zinawekwa katika benki ya mnufaika nchini Nijeria mara moja, hilo litakuwa jambo la ajabu,” anasema.

Kabla ya kupashwa habari na AfrikaUpya, Bw. Adele hakuwa anafahamu kuhusu PAPSS, hali inayodhihirisha kikwazo cha kimawasiliano cha kuwafahamisha wanabiashara wa mataifa kati ya Afrika kuuhusu ukumbi huo.

Bw. Oramah anatambua, hata hivyo, kwamba kuna kampeni inayoendelea kuuza na kusaidia PAPSS, ikitarajiwa kwamba wanabiashara wa Afrika watakuwa wameufahamu kikamilifu mfumo huo na kuutumia kufikia mwisho wa mwaka.