COVID-19: Walemavu wakabiliwa na wakati mgumu

Get monthly
e-newsletter

COVID-19: Walemavu wakabiliwa na wakati mgumu

Umoja wa Mataifa Wataka walemavu wawe katika msitari wa mbele wa kufikiriwa
Kingsley Ighobor
Afrika Upya: 
8 May 2020
Ms. Wafula-Strike is founder of the Olympia-Wafula Foundation
Ms. Anne Wafula-Strike
Bi. Wafula-Strike ni mwasisi wa Wakfu wa Olympia-Wafula kutetea haki za walemavu.

Bankole Labody Oyou, mwanafunzi wa miaka 24 wa uanahabari jijini Freetown, jiji kuu la Sierra Leone, alizaliwa kipofu.

Anamtegemea jamaa au rafiki kutembea jijini na darasani katika Chuo cha Fourah Bay, kilicho juu ya Mlima Aureol katikati mwa jiji la Freetown. Anasema kwamba COVID-19 imeyafanya maisha ya walemavu kuwa magumu mno.

“Tunateseka,” aliiambia AfrikaUpya. “Baadhi [ya walemavu] hawana jamaa wa kuwatunza. Tunaambiwa kusalia nyumbani, ila hatuna chakula. Serikali na jamii zinasahau kwamba tupo. Sijamsikia yeyote akijadili shida zetu katika redio.”

Kulingana na Umoja wa Mataifa, walemavu ni miongoni mwa watu walioathiriwa sana na COVID-19. Hata katika mazingira ya kawaida, ni nadra kwa walemavu bilioni moja duniani kote kupata huduma za kiafya, elimu, ajira na wamo katika hatari kuu ya kuishi katika umaskini na kushuhudia vurugu.

COVID-19 inazidisha hali hii, hasa kwa walemavu katika miktadha dhaifu na mazingira ya uhitaji wa kibinadamu. Wanakabiliwa na ukosefu wa elimu ya umma kuhusu afya, vikwazo vikuu kutekeleza hatua za kimsingi kuhusu usafi, na vituo vya afya visivyofikiwa.

Mwanariadha wa Kenya wa Olimpiki ya walemavu, Anne Wafula-Strike anakubaliana na maoni hayo, anasema “Walemavu wamesahauliwa kabisa. Janga hili lilizidisha tu hali iliyokuwa mbaya awali.”

Bi. Wafula-Strike ni mwasisi wa Wakfu wa Olympia-Wafula wenye lengo la kutetea haki za walemavu.

Katika mahojiano na AfrikaUpya, aliorodhesha vikwazo kadhaa vinavyowakabili walemavu kwa sasa. “Maoni yao hayachukuliwa kabla ya kuwazia jumbe kuhusu COVID-19, na mifumo ya kutangaza jumbe hizo haiwaafiki,” anasema. “Wengi wao hawana redio au runinga; baadhi wana ulemavu wa macho na hawawezi kusoma wala kuandika.”

Ms. Wafula-Strike
Ms. Anne Wafula-Strike

Hapendezwi pia na utekelezwaji wa aina moja ya utangazwaji wa hatua za kukabili COVID-19, bila kuwajali walemavu. “Polisi wanawakabili walemavu kama wafanyavyo watu wengine wote. Watunzaji ambao, kwa mfano, wanawasaidia kukalia viti vyao vya magurudumu na shughuli nyinginezo, wanatakiwa kutekeleza kanuni ya kutotangamana na watu. Je, walemavu wataishi vipi?”

Bi. Wafula-Strike anahofishwa na ongezeko la visa vya dhuluma za kijinsia, hasa dhidi ya wanawake walemavu “wanaolazimika kusalia nyumbani.”

Kufikia tarehe 2 Mei, visa takribani 39,749 vya COVID-19 na vifo 1,660 vilikuwa vimeripotiwa barani Afrika. Iwapo visa hivi vitaongezeka ghafla, Bi. Wafula-Strike anahofia kwamba hospitali zitalemewa, na kuwazuia walemavu kupata huduma muhimu za kiafya wanazostahili. “Wanaweza kuanza kufariki ndani ya nyumba zao.”

Shirika la Afya Duniani (WHO) linakariri hofu ya Bi. Wafula-Strike, huku likiongeza kwamba hatua za kimsingi kuhusu usafi kama “kuosha mikono, makaro au mabomba ya maji huenda zisifikiwe” na walemavu.

Shirika hilo limechapisha orodha ya hatua za kujilinda na zinazoweza kutumiwa na walemavu, serikali, jamii na wahudumu wa afya kupunguza makali ya COVID-19.

Ni sharti kwa walemavu, ikiwezekana, kujizuia kwenda katika maeneo yenye umati na wafanyie kazi nyumbani, Shirika la Afya Duniani linashauri.

Linapendekeza vyombo vya habari vinapotoa maagizo kuhusu COVID-19 vijumuishe maelezo mafupi kwa lugha ya ishara … kugeuza vyombo vya umma kuwa vya ‘kusomeka upesi’ kwa manufaa ya walemavu wa akili.”

Aidha, panastahili kuwa na fidia ya kifedha kwa jamaa na watunzaji wa walemavu, ikiwa ni pamoja na “kulipia, kwa kipindi cha wakati mfupi, jamaa kwa msaada wanaoutoa kwa wakati wa kawaida.”

Wahudumu wa afya wanaweza kuanza huduma ya afya-kwa-simu kama vile kutoa ushauri kupitia simu, arafa na mikutano ya video ili kutoa huduma za tiba na msaada wa kisaikolojia na kijamii kwa walemavu.

Ni muhimu pia kuhakikisha hapana anayesalia nyuma katika mchakato wa kujikomboa kutokana na COVID-19.

“Ninazihimiza serikali kuwashirikisha walemavu katika juhudi za kuwajibikia na kupata suluhu la COVID-19 pamoja na kushauriana na kuwahusisha walemavu,” alisema Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres hapo jana katika hafla ya kuzindua ripoti ya Umoja wa Mataifa ambayo inapendekeza kuwajibika kunakowashirikisha walemavu na ukombozi kwa wote.

Miongoni mwa mapendekezo ya ripoti hiyo ni haja ya serikali mbalimbali, wafadhili, mashirika ya Umoja wa Mataifa na washikadau wengine kuweka taratibu za uwajibikaji ili kuwezesha uangalizi wa uwekezaji na kuhakikisha ulemavu unashirikishwa katika kuwajibikia COVID-19, ikiwa ni pamoja na kupitia kwa kukusanya na kuiratibu data kuhusu ulemavu.

Zaidi ya hayo, uwekezaji mpya haustahili kuzua vikwazo vipya kwa walemavu— ikiwa utazingatiwa katika hatua ya kubuni, kuhakikisha hali ya kufikiwa kwaweza kugharimu kiwango kidogo tu kama 1% au zaidi.

Tayari baadhi ya serikali na mashirika yasiyo ya kiserikali yanachukua hatua kuwalinda walemavu kutokana na athari za janga hili. Kwa mfano, serikali ya Sierra Leone imetoa dola 25 na nusu gunia la mchele kwa kila mlemavu.

Lakini Bwana Oyou anasema kuwa pesa hizo hazitoshi kamwe. “Hatuwezi kuishi kwa $25 kwa kipindi cha miezi kadhaa.

Uhabeshi inatafsiri jumbe za COVID-19 kwa lugha asilia na taifa hilo linapanga kuhakikisha kwamba vyombo vya mawasiliano vinawafikia walio na changamoto za kusikia, kuona na kusoma, na hata wale walio na maradhi ya akili.

Afrika Kusini imetenga dola milioni 10.6 kuzisaidia biashara ndogo na wastani katika sekta za hoteli na utalii, huku walemavu na wanawake wakipewa kipaumbele.

Nchini Nijeria, shirika la maendeleo la Kikristo la kimataifa la asili ya Kijerumani, Christian Blind Mission, linasaidia kutafsiri jumbe za COVID-19 kwa lugha ya ishara.

International Disability Alliance — muungano wa mashirika zaidi ya 1,000 yanayoshughulika na masuala ya ulemavu — umezindua mpango wa COVID-19 “Disability Rights Monitor” kufuatilia hatua zinazochukuliwa na mataifa kuhusu “haki kuu za walemavu ikiwa ni pamoja na haki ya kuishi, kupata huduma za kiafya na huduma nyingine muhimu.”

Haya yanaweza kuwa na athari kuu, anasema Bi. Wafula-Strike; hata hivyo, ana hofu iwapo visa vya COVID-19 vitaongezeka ghafla barani Afrika. “Ni lazima hatua fulani zichukuliwe ili kujiandaa kwa hali kama hiyo. Taifa linatathminiwa kulingana na namna linavyowashughulikia raia wake walio hatarini.” Alisema.