Kuridhiwa kwa sarafu ya Kidijitali barani Afrika: Changamoto na manufaa

Get monthly
e-newsletter

Kuridhiwa kwa sarafu ya Kidijitali barani Afrika: Changamoto na manufaa

Changamoto ni pamoja na ukosefu wa intaneti ya kuaminika na ukosefu wa maarifa ya kifedha
Afrika Upya: 
10 June 2021
Cryptocurrency
Unsplash/Dmitry Demidko
Africa is booming in terms of cryptocurrency adoption, according to the 2020 Geography of Cryptocurrency Report by Chainalysis.

Afrika inazidi kushamiri katika suala la kuridhia sarafu ya kidijitali, kulingana na Ripoti ya Kifedha kuhusu maeneo yaliyoridhia sarafu ya Kidijitali ya 2020 iliyoandaliwa na Chainalysis - kampuni ya uchanganuzi wa sarafu ya kidijitali inayotoa data, programu, huduma, na utafiti kwa taasisi za serikali, mabadilishano, taasisi za kifedha, na kampuni za bima na usalama mtandaoni katika nchi  zaidi ya 50.

Kulingana na ripoti hiyo, shughuli za sarafu ya kidijitali za Afrika zimejumlishwa zaidi kwenye huduma 10 kubwa kwa wingi barani, huku sehemu ya huduma hizo ikiwa sehemu ya huduma za jumla katika eneo hili ikiongezeka kutoka asilimia 67 kuanzia Oktoba 2019 hadi asilimia 78 ilipofika 2020 .

Shughuli nyingi kutoka Afrika zikiendea Binance- ubadilishanaji mkubwa sana wa safaru ya kidijitali duniani katika masuala ya wingi wa biashara. Inatoa jukwaa la kufanya baishara katika sarafu tofauti za kidijitali.

Sehemu ya Binance ya shughuli zote za sarafu ya kidijitali barani Afrika imeongezeka sana tangu mwanzo wa 2020, ripoti inasema. Uhamishaji wa kiwango cha rejareja (uhamisho chini ya $ 10,000) unachukua sehemu kubwa ya shughuli za sarafu za kidijitali barani Afrika kuliko eneo lingine lolote, na mahitaji ya utumaji pesa huchukua sehemu yake kubwa.

Hata hivyo, Benki Kuu ya Nijeria hivi karibuni iliagiza benki kuacha kutoa huduma kwa watoa huduma za sarafu za kidijitali.

"Uridhiaji ndio ulikuwa umeanza kushika kasi barani Afrika, haswa nchini Nijeria mambo yalikuwa yalikuwa mazuri mwaka jana," anasema Buchi Okoro, mwanzilishi mwenza na Mkurugenzi Mtendaji wa Quidax, jukwaa ambalo linaruhusu watu kununua na kuuza sarafu za kidijitali. "Bado biashara inaendelea kwa kubadilishana [ambapo] utaona ishara lakini hakujakaribia kiasi tulichoshuhudia."

Huku Nijeria ikiwa imetengwa na kile Bwana Okoro anachokiita "ustawi wa ulimwengu," raia wake wengi sasa wanageukia ubadilishanaji wa mwenzi kwa mwenzi (P2P). Kwa bahati mbaya, ukosefu wa sheria katika baadhi ya nchi unaweza kuleta matatizo katika suala la umiliki wa mali.

"Tunaona shughuli nyingi kupitia ubadilishanaji wa P2P, kisha ubadilishanaji mwingine pia unajaribu kukabiliana na matatizo ya kupata pesa," anasema. "Lakini kimsingi, bado inahusu uwezo wa kutimiza masharti."

Hakika, biashara ya P2P ni mtindo maarufu nchini Kenya.  Hata ingawa Benki kuu ya Kenya ilitoa ilani ya tahadhari kuwaonya wawekezaji kuhusu majukwaa ya sarafu ya kidijitali, hii haikuzuia watu wachache kuijaribu.

"Watu wengi walituma jumbe kwa tweeter kuhusu benki kufunga akaunti zao zikiwa na pesa zao kwa sababu kwa njia moja au nyingine walikuwa wakiwezesha shughuli ya sarafu ya kidijitali," anasema Roselyne Wanjiru, Mkurugenzi wa Ukuaji na Utafutaji wa Watumizi katika Pesabase, jukwaa ambalo linaruhusu watu kutuma pesa na kufanya malipo. "Lakini watu pia walihisi kuwa ikiwa wanaweza kupata pesa kutokana na haya katikati ya janga, ni jambo ambalo wataendelea kufanya."

Kuelewa ulimwengu wa sarafu ya kidijitali

Sehemu ya tatizo linalokumba uridhiaji wa sarafu ya kidijitali barani Afrika, mbali na ukosefu wa intaneti ya kuaminika na ya bei nafuu, haswa mbali na maeneo ya mijini, ni kiwango tofauti cha maarifa ya kifedha.

Watu wengi hawajui aina za uwekezaji zaidi ya masuala ya kimsingi kama vile majumba na ardhi au hisa. Hata wale ambao husikia kuhusu mabilionea fulani labda hawajui mengi kuhusu jinsi walivyojenga utajiri wao, zaidi ya kufikiria kuwa ina uhusiano fulani na pesa.

"Kadiri habari hii inavyochukua muda mrefu kuufikia umma, haswa vijana, ndivyo uwezekano wao wa kutazamia haya utakuwa mdogo,'' Bi. Wanjiru anasema. "Hiyo inamaanisha kuwa fedha zilizogatuliwa na sarafu ya kidijitali zinaweza kuwa katika hatari ya kunga’ng’aniwa siku zijazo"

Kufanya sarafu ya kidijitali iwe ya kawaida zaidi inafaa kuanza kwa kurahisisha dhana zenyewe kwa lugha ya wenyeji. Lakini ingawa Bi. Wanjiru ameona juhudi kadhaa za kutafsiri makala ya kielimu kwa Kiswahili, bado kuna mamia ya lugha na lahaja zingine barani kote.

"Bado kuna juhudi nyingi zinazohitajika kutafsiri makala haya kwa lugha tofauti za wenyeji ili wazee na wale ambao hawaishi mijini waweze kupata habari hii," anasema.

"Aidha, majukwaa mbalimbali yanahitaji kuifanya iwe rahisi kwa watu ambao hawaifahamu sarafu ya kidijitali kuielewa vizuri.

Mahitaji ya sheria na uaminifu

Kwa kuzingatia hali inayobadilika kila wakati katika ulimwengu wa sarafu ya kidijitali, moja ya hatari kubwa ni ukosefu wa sheria sahihi katika baadhi ya nchi za Kiafrika. Hii inaweza kupokonya kampuni biashara mara moja bila kosa, licha ya kuwa sheria ndiyo inahitajika zaidi katika sekta hii.

''Hatuna mfumo wa kisheria. Tunafuata sera zilizowekewa benki kuhusu masuala kama vile kiwango kinachohitajika cha mtaji na kikomo cha manunuzi, ”Bwana Okoro anasema. "Lakini chochote kinaweza kutokea wakati wowote. Kwa hivyo, kulingana na kile tumekuwa tukifanya hivi sasa, tumeandika barua kadhaa kuomba sheria zitungwe.''

Uaminifu nao unafungamana na mahitaji ya sheria. Akiwa mtu aliyezungumzia sarafu ya kidijitali kwa miaka mingi, Bi. Wanjiru amewaona marafiki zake wakitoka katika hali ya kudadisi hadi kupata hamu kubwa ya kutaka kushiriki.

Bi. Wanjiru anaamini kuwa kufikia uridhiaji kamili, hasa wakati kuna maoni mengi yanayokinzana kuhusu mada hii, kunahitaji uthabiti zaidi kutoka kwa sekta yenyewe.

"Ikiwa hawakuniamini au hawakuona msimamo wangu thabiti, uaminifu huo haungekuwa na thamani yoyote," anasema.

Watu wasipoamini jukwaa lako, au kupakua programu yako, au kujiandikisha kuwa sehemu ya jamii yako, lazima bado uwepo kwa sababu ya kuwa na sauti kwa kushirikiana nao na kujibu maswali yoyote ambayo wanaweza kuwa nayo, anasema Bi. Wanjiru: "Kuwa tu, uwe thabiti na ujenge uaminifu ambao utawaruhusu watu hawa kuja (hata ikiwa baada ya miaka miwili au mitatu) na kuwa baadhi ya wateja wako waaminifu zaidi."

Ingawa bara la Afrika bado lina uchumi mdogo zaidi wa sarafu ya kidijitali katika eneo lolote lililochanganuliwa katika ripoti hiyo, ambapo dola bilioni 8.0 zilizopokelewa huku dola bilioni 8.1 zilitumwa kidijitali mwaka huo, idadi ndogo ya shughuli hiyo inaunda thamani ya kubadilisha maisha kwa watumizi katika eneo linalokabiliwa na uchumi legevu, kutoa malipo ya ada ya chini na njia mbadala ya kuweka akiba.

More from this author