Vipaumbele vya kimkakati vya Afrika ili kurejesha hali yake

Get monthly
e-newsletter

Vipaumbele vya kimkakati vya Afrika ili kurejesha hali yake

— Simulizi mpya ya maendeleo inahitajika kuwasilisha Bara la Afrika kama mdau muhimu na lililo na mafanikio na mazoea bora ya kushiriki
Cristina Duarte
Afrika Upya: 
16 July 2021
Wafanyakazi wanatayarisha meli katika Walvis Bay, bandari kuu nchini Namibia.
World Bank/John Hogg
Walvis Bay kwenye Bahari ya Atlantiki ndiyo bandari kuu nchini Namibia na nyumbani kwa makampuni mengi ya uvuvi. Meli ya wavuvi imepakiwa na vyombo safi kwa safari yake inayofuata.
Ikiwa huwezi kusoma sasa, sikiliza tu toleo la sauti: 
Sauti ya Kiingereza

Afrika inatambua fursa anuwai za ndani na za kimataifa inayopaswa kutumia, na changamoto ambazo lazima ishinde ili kuimarisha misingi ya maendeleo yake.

Nchi za Kiafrika zilijitolea kufuata mpango wa pamoja wa bara kwa miaka 50 ijayo kupitia Agenda 2063. Hii ni ruwaza inayoangazia mtazamo jumuishi ili kuhakikisha mageuzi na maendeleo endelevu kwa vizazi vijavyo.

Mwelekeo wa mageuzi ya Ajenda 2063 umekusudiwa kuongoza matendo ya wadau wa Afrika kukuza kuibuka kwa chumi thabiti na ukuaji endelevu na uwezo wa kuzalisha utajiri na ajira.

Ajenda 2063 inawasilisha hadithi mbadala kuhusu mwelekeo wa maendeleo ya Afrika; inachunguza masuala ya ndani na ya nje ambayo yanaleta changamoto na fursa kwa watu wa bara hili katika harakati zao za kutatufa maisha bora; inaeleza hali mbadala za sera na matokeo yao yaliyotarajiwa; na inazingatia uhusiano kati ya mipango ya kikanda na bara, huku ikiweka Nchi za Afrika katika kiini cha utekelezaji.

Kuzingatia matakwa ya kina ya watu ni sehemu ya ajenda ya mfumo wa Umoja wa Mataifa. Tangu alipochukua wadhifa wake, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres ameonya kuwa licha ya kuongezeka kwa utandawazi wa uchumi, "hisia zetu za jamii ya ulimwengu huenda zinasambaratika" na kwamba ulimwengu una tatizo la "upungufu wa uaminifu". 

Ili kushinda changamoto hizi, Katibu Mkuu aliahidi "kuufanya Umoja wa Mataifa kuwa na ufanisi zaidi katika kukabili mahitaji na matarajio yetu kama jamii" na akapendekeza mabadiliko kwenye mtazamo wa kupambana na vitisho vinavyoibuka kama mabadiliko ya hali ya hewa, kuhakikisha kuwa teknolojia mpya inakuwa kiini cha amani na uendelevu na "kufanya biashara za kimataifa na mifumo ya kifedha iwe sawa kwa lengo la kuendeleza maendeleo endelevu na kukuza utandawazi wa haki."

Janga la COVID-19 limeweka wazi ulegevu wa mfumo uliopo wa uchumi wa kimataifa. Janga hili limethibitisha kuwa hakuna nchi inayoweza kushinda changamoto za siku za usoni peke yake na kwamba ushirikiano wa kimataifa umepungukiwa. Janga hili limevuruga mfumo uliowekwa na kuunda fursa ya mabadiliko.

Licha ya kutambua upungufu wa kiutendaji, majadiliano baina ya serikali kadhaa yameendelea kushughulikia masuala kwa njia ileile ya zamani. Taratibu za kukabiliana na COVID-19 zimejumuisha hatua za kifedha ambazo zina masuluhisho ya muda mfupi, kama vile kusimamishwa kwa deni au ahadi rasmi za Usaidizi wa Maendeleo (ODA) ambazo hazishughulikii visababishi vikuu vya tatizo hili. Afrika inaendelea kuonyeshwa kama bara masikini linalohitaji msaada kutoka kwa "jamii ya kimataifa" ili ijijenge tena.

Janga la COVID-19 na athari zake kwa Malengo 17 ya Maendeleo Endelevu (SDGs) limeonyesha kuwa kile kilichoanza kama janga la kiafya kilibadilika haraka na kuwa janga la kibinadamu, kijamii na kiuchumi. Huku janga lenyewe likiwa limedidimiza hatua za kufikia SDGs, pia linafanya kuyafikia malengo hayo kuwa jambo la dharura na lazima.  Ni muhimu kwamba mafanikio yaliyoafikiwa hivi karibuni yalindwe iwezekanavyo. Tunapaswa kulenga kuangamiza COVID-19 kabisa, na kushughulikia janga lenyewe, kupunguza hatari zinazoweza kutokea kwa majanga ya usoni na kuzindua tena juhudi za utekelezaji unaolenga kufikia Ajenda ya 2030 na SDGs wakati huu wa Mwongo wa Utekelezaji wa maendeleo endelevu.

Kutokana na haya, ni dhahiri kwamba ikiwa Afrika itatimiza matakwa ya watu wake kama ilivyoainishwa katika Ajenda 2063 kuna haja ya simulizi mpya ya maendeleo yanayokuza uwezo wa bara kufikia Agenda 2063 na SDGs, na kuimarisha wajibu wa Afrika kama mtendaji muhimu katika mawanda ya kiulimwengu.

Kwa msingi huu, ni muhimu kwa Afrika kuwa na mkakati thabiti wa kujirejesha katika hali yake ya awali.  Ofisi ya Mshauri Maalum kuhusu Afrika (OSAA) imeanzisha ajenda ya kimkakati iliyoainisha vipaumbele sita vyenye uwezo mkubwa wa kukuza maendeleo ya Afrika. Ajenda ya kimkakati imegawika katika maeneo sita ya mada:

  • Fedha za Maendeleo: Kutetea upatikanaji wa fedha, kupambana na usambazaji haramu wa fedha, kuimarisha ushirikiano wa kimataifa kuhusu ushuru, kushirikisha mashirika ya ukadiriaji wa mikopo, na kupunguza gharama za kutuma fedha.
  • Maendeleo Endelevu ili Kuimarisha Amani Endelevu: Kuendeleza mazoea jumuishi ya kitaasisi katika kukabiliana na chumi za nchi zilizo na mizozo na kujenga jamii zenye uwiano kama msingi wa amani.
  • Utawala, Ustahimilivu na Mtaji wa Kibinadamu: Kuhimiza kuweka mtaji wa kibinadamu katika kiini cha utungaji wa sera barani Afrika ili kujenga jamii zenye ustahimilivu.
  • Teknolojia na Uvumbuzi: Kutetea kuziba pengo la uelewa wa kidijitali na tofauti za kidijitali; na kushughulikia masuala ya hakimiliki ili kuanzisha maendeleo katika sehemu mbalimbali.
  • Viwanda, Gawio la kidemografia, na Eneo Huru Afrika (AfCFTA): Kuhimiza kutumia gawio la kidemografia ili kuchochea ukuaji viwanda kupitia AfCFTA.)
  • Nishati na Matendo ya Hali ya Hewa: Kuzingatia mchanganyiko wa nishati barani Afrika, mabadiliko ya hali ya hewa na uendelezaji wa hewa safi, mabadiliko ya nishati, na sera za mazingira.

Changamoto ya Afrika sio umasikini wala ukosefu wa ujuzi, bali ni ukosefu wa hela au fedha za kukuza ujenzi na kufikia maendeleo endelevu. Matatizo ya Afrika ni miundo ya kijamii, kisiasa na kiuchumi yanayonyonya uwezo wake na kuzuia uwezo wa bara.

Usafirishaji haramu wa fedha unalemaza uwezo wa ufadhili wa Afrika. Mfumo wa haki wa kifedha wa kimataifa unazuia ufikiaji wa nchi za Kiafrika wa vyanzo vya fedha kwa usawa. Ukosefu wa umiliki kuhusu maliasili unazuia nchi za Kiafrika kutekeleza jukumu muhimu katika mfumo wa uongezaji thamani wa ulimwengu.

Afrika inakabiliwa na athari za janga la hali ya hewa ambazo zimesababishwa na mataifa yaliyostawi zaidi na inavumilia athari za majanga magumu zinazotokana na  visababishi kadhaa vya kihistoria, kijamii na kiuchumi vya sasa.

Kwa jumla, Afrika inakabiliwa na changamoto ya kuendeleza mabadiliko katika sheria za mfumo wa pande nyingi ambao, kwa sasa, sio wa haki wala sio sawa kwa wote. Hii inahitaji simulizi mpya ambayo inawasilisha Bara la Afrika kama mdau muhimu na lililo na mafanikio na mazoea bora ya kushiriki. Simulizi ya Afrika na inayotoka Afrika katika Umoja wa Mataifa na kwingineko.


Bi Duarte ni Katibu Mkuu Masaidzi na Mshauri Maalum kuhusu Afrika.

Cristina Duarte
More from this author