Nishati itakuwa sehemu muhimu sana katika kufanikisha eneo huru la biashara Afrika

Get monthly
e-newsletter

Nishati itakuwa sehemu muhimu sana katika kufanikisha eneo huru la biashara Afrika

—Damilola Ogunbiyi, Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa wa Nishati Endelevu kwa Wote
Kingsley Ighobor
Afrika Upya: 
15 July 2021
 Olkaria geothermal complex and power station, kiwanda cha kwanza cha kuzalisha umeme kwa jotoardhi
IRENA
Olkaria geothermal complex and power station, kiwanda cha kwanza cha umeme kwa jotoardhi barani Afrika kilichopo Nairobi, Kenya.
Ikiwa huwezi kusoma sasa, sikiliza tu toleo la sauti: 
Sauti ya Kiingereza

Damilola Ogunbiyi ni Mkurugenzi Mtendaji wa Nishati Endelevu kwa Wote (SEforALL) na Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa wa Nishati Endelevu kwa Wote. Pembeni mwa Mkutano wa Siasa wa Kiwango cha Juu wa Umoja wa Mataifa ukifanyika New York, Bi Ogunbiyi alizungumza na Kingsley Ighobor wa Afrika Upya kuhusu masuala kadhaa, yakiwemo jinsi ya kukabiliana na uhaba wa nishati barani Afrika. Hizi hapa ni dondoo:

Damilola Ogunbiyi
Damilola Ogunbiyi, Mkurugenzi Mtendaji wa Nishati Endelevu kwa Wote (SEforALL) na Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa wa Nishati Endelevu kwa Wote

Kama kiongozi wa kiulimwengu na mtetezi wa kufanikiwa kwa Lngo Endelevu la saba (SDG7), linalotoa wito wa upatikanaji wa nishati thabiti, ya bei nafuu, endelevu na ya kisasa kwa wote ifikapo mwaka 2030, ni mambo gani matatu muhimu ambayo nchi za Afrika zinahitaji kufanya kukomesha uhaba wa nishati? 

Mojawapo ya mambo ya kwanza muhimu, ambayo nchi zimeanza kufanya, ni kutambua ni wapi watu wanaohitaji umeme na nishati safi wako. Kufanya hivi kutawezesha nchi kutambua njia bora ya kufikia lengo hili kwa kutumia mchanganyiko wa nishati kadhaa, wakijua kuwa safi ni bora.

Jambo la pili ni kwa nchi kuhakikisha zina sera na sheria thabiti kusaidia kuvutia uwekezaji na kusaidia soko lao mbadala la nishati safi.

Kisha mwishowe - na suala hili ni la kiulimwengu pamoja na suala la nchi za Kiafrika — ufadhili lazima uwepo. Kwa hivyo, ufadhili wa umma, ufadhili wa kibinafsi, ufadhili wa kibiashara, ufadhili usio wa kibiashara, hela za wahisani- zote zinahitajika ili kukomesha uhaba wa nishati.

Leo hii, zaidi ya watu milioni 700 hawana umeme kabisa. Taribani watu bilioni 2.6, karibu thuluthi moja ya idadi ya watu ulimwenguni, hawana ufikiaji wa nishati safi ya kupikia.

Barani Afrika, watu milioni 570 wanakosa huduma ya umeme. Tunazungumzia tatizo litakalotugharimu karibu dola za Marekani bilioni 40 kila mwaka kutoka sasa hadi mwaka 2030. Na hivi sasa, barani Afrika, tunapata chini ya dola za Marekani bilioni 4. Kwa hivyo, inakuonyesha kibarua kikubwa tulichonacho ili kuhakikisha kiwango sahihi cha rasilimali kinatumika kutatua uhaba wa nishati.

Kwa hivyo karibu Waafrika milioni 600 hawana uafikiaji wa nishati. Hii ni karibu nusu ya idadi ya watu barani. Je, nchi za Afrika zimefanya vipi katika mabadiliko ya kutumia nishati safi? Mifano yoyote mizuri?

Kuna mifano mizuri sana. Nikitumia nchi yangu, Nijeria, kwa mfano, niliongoza mradi mkubwa sana wa upatikanaji wa nishati, ambao ulilenga miradi ya nishati mbadala chini ya mradi inaoitwa Mradi wa Umeme wa Nijeria. Mradi huo ulitekelezwa kwa ushirikiano mzuri na Benki ya Dunia na Benki ya Maendeleo ya Afrika. Tulisambaza nishati na kulenga nishati ya jua na tuliweza kuvipa vyuo vingine vikuu nishati.

Mifano mingine mizuri pia inatoka Rwanda na Senegali. Lakini tatizo ni kwamba nishati hiyo ni kidogo; sasa tunapaswa kulenga kuiongeza.

Sio kwamba hakuna hatua inayopigwa katika nchi za Afrika kwenye suala la umeme, isipokuwa ongezeko la idadi ya watu ni kubwa kuliko umeme. Kwa hivyo, hata ukipiga hatua nyingine ya kuongeza watu milioni moja au mbili zaidi kufikia nishati kila mwaka, lakini kuna ukuaji wa idadi ya watu ya karibu milioni 10, ni vigumu kutimiza mahitaji yao ya nishati. Ndiyo sababu tunahitajika kuongeza kasi. Na ndiyo sababu tunahitaji, kama nilivyosema, pesa kutoka kwa wahisani, taasisi za maendeleo, taasisi za kifedha, serikali — zote ziwekwe pamoja katika kutafuta suluhisho lenye ubunifu ambalo litahakikisha kuwa hakuna mtu aliyeachwa nyuma katika kupata wa nishati.

Je, kuna hatua gani inayopigwa katika kutafuta fedha kufaidi sekta ya nishati barani Afrika?

Ni hatua muhimu sasa, hasa mwaka huu wakati Umoja wa Mataifa una mazungumzo ya kiwango cha juu kuhusu nishati, kwa mara ya kwanza katika miaka 40. Tunajadili mada hii katika Mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa. Watu sasa wanatambua kuwa uhaba wa nishati ni mbaya sana, na ni muhimu sana kwetu wakati tunajaribu kuhamia nishati mbadala ya kijani, safi na inayoweza kutumika tena, ambayo ni muhimu sana, kwamba upatikanaji wa nishati na uhaba wa nishati lazima uwe sehemu ya mpito wa nishati kwa nchi nyingi za Afrika.

Nina matumaini mengi kwamba mwaka huu, kutakuwa na mabadiliko makubwa katika suala la taratibu za kupata nafuu kutokana na COVID-19 na taratibu nyingine za kuelekea nishati safi barani Afrika, mabadiliko ambayo hatujawahi kuona hapo awali. 

Janga la COVID-19 limepunguza fursa za fedha za nchi nyingi. Na Afrika hivi sasa inakabiliwa na wimbi la tatu la maambukizi. Je, ni ushauri gani unaweza kuzipa nchi hizi kuhusu jinsi zinavyoweza kuweka kipaumbele katika uwekezaji wa nishati wakati huu? 

Kwa kila $ 1 unayowekeza katika nishati safi katika nchi yoyote, tunaona faida ya karibu senti 0.93 kwa Pato la Taifa. Kwa hivyo, ni uamuzi mzuri tu wa kiuchumi. Kazi zaidi zinaundwa, na kutakuwa na ongezeko la upatikanaji wa nishati na ufaafu wa nishati. Kuna faida nyingi, mbali na zile wazi, ikiwemo kuwa na watu wenye afya, mavuno mengi katika kilimo, n.k.

Na kwa wanawake?

Ukimpa mwanamke ufikiaji wa nishati endelevu, anapata 59% zaidi. Kwa hivyo hata ikiwa una orodha ndefu ya matakwa ya vitu vinavyohitaji matumizi ya pesa, nishati safi ndio unapaswa kuzingatia kwa sababu ni hesabu nzuri katika ukuaji wa uchumi. 

Eneo Huru la Biashara Barani Afrika (AfCFTA) lilianza Januari mwaka huu, na linatarajiwa kuchochea ukuaji wa viwandani barani Afrika. Je, nishati inayopatikana kwa wote, na kufanikisha uzalishaji usioweza kuharibu mazingira, inaweza kuendesha ukuaji kama huo wa viwandani? 

Naam, ukweli kwamba Afrika ni moja ya maeneo ambayo yatahitaji nishati zaidi, hasa eneo la Kusini mwa Sahara, ni muhimu sana. Isitoshe, kwa kuweka katika mtazamo: uwezo wa Afrika Kusini mwa Sahara, ukiondoa Afrika Kusini, ni gigawati 81 tu. Huo ndio uwezo sawia na ule unaozalishwa na Ujerumani. Kwa hivyo, ni gigawati 81 kwa zaidi ya watu bilioni. Afrika Kusini mwa Sahara inahusika kwa chini ya asilimia moja ya uzalishaji gesi inayoharibu mazingira, na tunataka uzalishaji huu usalie chini na kuendelea kuwa chini katika mkondo wa chini wa kaboni. Tungehitaji paneli za jua, betri za lithiamu na vigeuzi. Tunahitaji teknoloja nyingi. Teknolojia hizi hazipaswi kuletwa kutoka nje kuja barani; tunapaswa kutazamia kuziunda barani Afrika ili kukabiliana na mahitaji.

Nishati itakuwa sehemu muhimu sana katika kufanikisha eneo huru la biashara Afrika.