Maendeleo ya kituo cha mRNA cha Afrika Kusini ni msingi wa kujitegemea

Get monthly
e-newsletter

Maendeleo ya kituo cha mRNA cha Afrika Kusini ni msingi wa kujitegemea

Kitahakikisha Afrika ina uwezo wa kuzalisha ambao ni muhimu kwa utoaji wa chanjo wenye usawa
World Health Organization
Afrika Upya: 
14 February 2022
Na: 
Rodger Bosch for MPP/WHO
Tedros Ghebreyesus(C) WHO Director-General and Meryame Kitir, Belgian Minister of Development, see a vial-labelling machine at work, during a visit to Biovac, in Cape Town.

Dkt. Tedros Adhanom Ghebreyesus, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Afya Duniani (WHO), Buti Manamela, Naibu Waziri wa Elimu ya Juu na Mafunzo wa Jamhuri ya Afrika Kusini, Dkt Blade Nzimande, Waziri wa Elimu ya Juu, Sayansi na Teknolojia wa Afrika Kusini, Dkt. Joe Phaahla, Waziri wa Afya wa Afrika Kusini na Meryame Kitir, Waziri wa Ushirikiano wa Maendeleo na Sera ya Miji wa Ubelgiji, waliwatembelea washirika kadhaa kutoka sekta ya umma na binafsi wanaoshirikiana ili kutengeneza na kujenga kituo cha kimataifa cha WHO cha uhamisho wa teknolojia ya chanjo ya mRNA nchini Afrika Kusini.

Katika kipindi kirefu cha mwaka 2021, upungufu wa upatikanaji wa chanjo duniani ulisababisha tofauti kubwa ya ufikiaji wa chanjo za Uviko-19, na kuacha mabilioni ya watu- hususan katika nchi zenye uchumi wa chini na wa kati- bila ulinzi dhidi ya ugonjwa mbaya na vifo kutokana na Uviko-19.

Viwango vya chini vya upatikanaji wa chanjo pia vilitoa mazingira yaliyowezesha kutokea kwa aina mpya za ugonjwa.

Ingawa usambazaji wa chanjo sasa umeongezeka, uwezo wa kufikia chanjo mpya za Uviko-19 - zilizotengenezwa maalum kwa aina mpya za ugonjwa huu huenda pia usiwe na usawa kwa sababu uwezo wa kuzitengeneza unabaki kuwa mikononi mwa kampuni na nchi chache tu.

"Uviko-19 umedhihirisha umuhimu wa uwekezaji katika sayansi, teknolojia na uvumbuzi. Hivyo, kujiandaa kwa tandavu za siku zijazo ni muhimu na kituo cha kimataifa cha mRNA cha WHO ni nguzo muhimu katika kuhakikisha kwamba Afrika Kusini na bara zima lina uwezo wa uzalishaji, ambao ni muhimu kwa utoaji wa chanjo kwa usawa," alisema Dkt Blade Nzimande, Waziri wa Elimu ya Juu, Sayansi na Teknolojia wa Afrika kusini.

"Teknolojia ya mRNA sio ya Uviko-19 pekee, tunatumaini inaweza kutengenezwa maalum ili kutusaidia katika kupambana na virusi vya Ukimwi, kifua kikuu na malaria, na ndiyo maana tunawekeza sana, kwa kushirikiana na washirika wa kimataifa katika mpango huu."

Kulingana na maono ya serikali za Afrika Kusini na Ufaransa ya kuongeza utengenezaji wa chanjo na hasa kuendesha kwa kasi uzalishaji wa chanjo ndani ya Afrika, muungano unaojumuisha Medicines Patent Pool, Biovac, Afrigen Biologics and Vaccines, Idara ya Sayansi na Uvumbuzi ya Afrika Kusini, Baraza la Utafiti wa Kimatababu la Afrika Kusini (SAMRC), mtandao wa vyuo vikuu na Kituo cha Udhibiti na Uzuiaji wa Magonjwa (CDC) cha Afrika Kusini vinaendesha mpango huu.

Lengo kuu ni kuanzisha kituo cha mafunzo ambacho teknolojia ya mRNA itakuzwa kwa kiwango kinachohitajika kwa ajili ya uzalishaji wa chanjo kwa wingi na kisha kuweza kuhamishiwa kwa wapokeaji wengi walio katika nchi za uchumi wa chini na wa kati.

"Bado hatujatoka kwenye hatari na kuna uwezekano wa kuzuka aina nyingine mpya ya Uviko-19 na wimbi la tano linaloambatana na msimu wetu wa baridi, ambao ni msimu wa mafua na baridi kwetu. Hata hivyo, tunaweza kupunguza athari kwa kuhakikisha watu wengi wamepata chanjo, hususan makundi yaliyo hatarini zaidi," alisema Waziri wa Afya wa Afrika Kusini, Dkt Joe Phaahla.

"Kituo hicho kipya sio tu cha Afrika Kusini, bali kinatoa duka moja lenye bidhaa zote kwa nchi za uchumi wa chini na wa kati duniani kote ili zinufaike kutokana na teknolojia iliyohamishwa, pamoja na ujuzi, na pia ziweze kuzalisha chanjo za mRNA, ambayo ni muhimu ikiwa tunataka kukomesha ukosefu wa usawa wa upatikanaji wa chanjo."

Wiki iliyopita, Afrigen, ambayo ni sehemu ya muungano wa mRNA wa WHO, ilisifiwa kimataifa baada ya kutangaza kwamba ilikuwa imetengeneza toleo lake la chanjo ya mRNA, kutokana na data zinazopatikana hadharani kuhusu viambato vya chanjo ya Uviko-19 ya Moderna, ambayo itafanyiwa majaribio katika miezi ijayo.

“Virusi hivi vinaonyesha jinsi wote tunavyounganika, na ninaona fahari kwamba Ubelgiji – na nchi nyingine za Umoja wa Ulaya – sasa zinashirikiana ili kukuza uwezo wa chanjo kila mahali,” alisema Meryame Kitir, Waziri wa Ushiriano wa Maendeleo na Sera ya Miji wa Ulebgiji.

"Kuendelea mbele, tunahitaji kushirikiana zaidi kwenye mambo ya leseni, uhamisho wa teknolojia na ujuzi ili kwenye janga hili, na  majanga yajayo, tuweze kutoa chanjo haraka na kwa usawa kwa watu wote duniani kote."

Kituo cha kimataifa cha mRNA kimeanzishwa ili kuhudumia nchi za uchumi wa chini na wa kati na kitawezesha nchi si tu kuweza kutengeneza chanjo zao zenyewe za mRNA bali pia hatimaye kuwa na chaguo la chanjo zipi zingependa kutengeneza.

Watengenezaji kutoka nchi za uchumi wa chini na wa kati wanahimizwa kuonyesha nia yao ili waweze kupata mafunzo, uhamisho wa teknolojia na leseni zozote muhimu. WHO na washirika wake wataleta ujuzi kuhusu uzalishaji, udhibiti wa ubora na leseni muhimu kwa chombo kimoja ili kuwezesha uhamisho mpana na wa haraka wa teknolojia kwa wapokeaji wengi.

"Tandavu hii imeonesha hitaji la kuongeza uzalishaji wa chanjo ndani ya mataifa yote duniani, hususan katika nchi za uchumi wa chini na wa kati," alisema Dkt Tedros Adhanom Ghebreyesus, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Afya Duniani. "Kituo cha kimataifa cha mRNA cha WHO ni hatua kuu katika kufikia hayo, kwa kushirikiana teknolojia na kukuza uwezo na utaalamu wa kisanyasi ambao tayari upo nchini Afrika Kusini."

Vituo vya kimataifa vitatumika kama sehemu za mafunzo ambapo teknolojia inawekwa katika ngazi ya kiviwanda na maendeleo ya kimatibabu kufanywa. WHO itasaidia shughuli hii na kusaidia nchi nyingine barani Afrika na nchi nyingine za uchumi wa chini na wa kati kuimarisha uwezo wao wa kutengeneza dawa na vilevile uwezo wa kiudhibiti.

Dkt. Matshidiso Moeti, Mkurugenzi wa Kanda wa Shirika la Afya Dunia katika Ofisi ya Kikanda ya Afrika, alisema: “Vituo hivi vya mRNA ni fursa ambayo haikutarajiwa ya kukuza uwezo, na kuiweka Afrika katika njia ya kujitegemea. Mpango huu utawezesha bara hili kujilinda vyema zaidi dhidi ya milipuko, kudhibiti tandavu la Uviko-19 na kutengeneza chanjo mpya, kuweka kasi katika kuondoa magonjwa hatari kama vile ukimwi, malaria na kifua kikuu. Tunafungua mlango wa afya bora na ustawi wa watu wetu."

"Katika Medicines Patent Pool, tunafuraha isiyo na kifani kuweza kukipa kituo cha mRNA ujuzi wetu kuhusu udhibiti wa hakimiliki na leseni ya hiari. Inafurahisha kuona jinsi ambavyo tumefanya kazi kwa ushirikiano na katika muda mfupi, na tumeweza kuweka msingi wa shirika hili ambao teknolojia hii mpya inaweza kushirikishwa katika nchi zote zenye uchumi wa chini na wa kati," alisema Charles Gore, Mkurugenzi Mtendaji wa Medicines Patent Pool.

"Serikali ya Afrika Kusini na washirika wake wameonyesha kujitoa kwao kwa dhati, na bila shaka hii imewezekana tu kwa hisani ya wafadhili wetu, ambao wametafuta rasilimali ndani ya kipindi kifupi na kuunga mkono mradi huu kwa kiasi kikubwa.”

Ziara hiyo pia itajumuisha Kituo cha Kushughulikia Magonjwa ya Milipuko na Uvumbuzi, ambacho ndicho kiini cha mpango maalum wa kimataifa wa uchunguzi wa genomiki wa Afrika Kusini, mikutano na makundi ya asasi za kiraia na ziara katika vituo vya kutoa chanjo mjini CapeTown.