Hali usugu kwa antibayotiki pamoja na dawa nyingine inaleta wasiwasi duniani

Get monthly
e-newsletter

Hali usugu kwa antibayotiki pamoja na dawa nyingine inaleta wasiwasi duniani

Kuweka lebo kwenye dawa na maelekezo ya matumizi kunaweza kusaidia kukabiliana na hali ya usugu wa dawa za kuua bakteria
Afrika Upya: 
2 February 2022
Most people buy self-prescribed antibiotic drugs over the counter and end up developing resistance to other drugs.

Wakati Winnie Chepkoech akiwa mwanafunzi wa chuo kikuu, alipata maambukizi ya njia ya mkojo (UTI). Badala ya kwenda kumuona daktari, alienda katika duka la dawa lililo mtaani na kununua antibayotiki ili kutibu tatizo hilo. Dalili zake zilipotea lakini zikarudi tena baada ya wiki kadhaa. Kilichofuata ni miaka miwili ya mahangaiko akijaribu kutibu UTI.

Winnie mwenye umri wa miaka 28, ambaye ni mama wa watoto wawili anasema amehangaika na maambukizi hayo kwa miaka kadhaa kwa sababu kila dawa aliyopewa ilionekana haifanyi kazi. 

"Kutajwa kwa dawa za antibayotiki kunanipa kiwewe kwa sababu ninafahamu nilichokipitia miaka yote hii. Ninapozungumza sasa, ninahofia UTI huenda ikatokea tena na ni lazima nianze kujaribu kuitibu tena," anasema.

Bi. Chepkoech ni mmoja kati ya watu wengi barani Afrika - ambapo dawa za antibayotiki zinapatika kwa urahisi kwenye maduka - ambao kutumia kwao bila ushauri, kutumia vibaya au kutumia dawa kupita kiasi, hususan dawa za antibiotiki, kumewapa na hali ya usugu kwa dawa hizi.

Je, dawa za kuua viini ni nini?

Dawa za kuua viini – ni pamoja na antibayotiki, dawa za kupambana na virusi, dawa za kupambana na kuvu na dawa za kupambana na vimelea – ni dawa zinazotumika kuzuia na kutibu maambukizi kwa binadamu, wanyama na mimea.

Hali ya usugu wa dawa za kuua viini (AMR) hutokea wakati viini, virusi, kuvu na vimelea vimebadilika baada ya muda na haviwezi tena kutibika kwa dawa hivyo kufanya maambukizi hayo kuwa magumu kutibika. Hii inaongeza hatari ya kuenea kwa ugonjwa, ugonjwa kuzidi kuwa mbaya na hata kifo.

Shirika la Afya Duniani (WHO) limetangaza kwamba AMR ni moja ya matishio makuu 10 ya afya ya umma duniani yanayowakabili binadamu.

Matumizi mabaya ya dawa na matumizi ya dawa za kuua viini kupita kiasi ndiyo chanzo kikuu kinachopelekea vimelea vya magonjwa kukinzana na dawa.

Kemikali za kilimo

Zaidi ya hayo, kushika kasi kwa uzalishaji katika kilimo kumesababisha kuongezeka kwa matumizi ya dawa za kuua viini - matumizi ambayo yanatarajiwa kuongezeka maradufu ifikapo mwaka 2030.

AMR inaweza kukua kwenye mimea na wanyama pia kwa kupitia matumizi au kutumia antibayotiki na kemikali zingine za kilimo kupita kiasi, na inaweza kwenda kwa binadamu wanapokula bidhaa za shambani.

Kulingana na Shirika la Chakula na Kilimo Duniani (FAO), inakadiriwa kwamba watu 700,000 hufa kila mwaka kutokana na maambukizi yanayotokana na hali ya usugu wa dawa za kuua viini na kuna idadi isiyojulikana ya wanyama ambao huenda hawatibiki. Hili ni tishio kubwa kwa afya ya umma duniani, upatikanaji wa chakula salama, maisha ya watu, uzalishaji wa wanyama na maendeleo ya kiuchumi na kilimo.

WHO inasema kwamba hali ya usugu wa dawa za kuua viini inaleta wasiwasi kimataifa. Hii ni kwa sababu kuibuka na kuenea kwa pathojeni zinazokinzana na dawa ambazo zimepata mbinu mpya za usugu wa dawa kunatishia uwezo wa kutibu maambukizi ya kawaida. Kinachotia wasiwasi zaidi ni kuenea kote ulimwenguni kwa "wadudu sugu" wanaosababisha maambukizi ambayo hayawezi kutibika kwa kutumia dawa zilizopo za kuua viini kama vile antibayotiki.

Mnamo Machi 2017, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa aliitisha mkutano wa dharula kwa Kikundi cha Umoja wa Mataifa kinachoratibu Mashirika hayo kuhusu Usugu wa Dawa za Kuua Viini, ili kutoa mwongozo unaofaa kwa mbinu zinazohitajika ili kuhakikisha hatua endelevu za kimataifa zinachukuliwa ili kutatua hali ya usugu wa dawa za kuua viini. 

Ripoti ya 2019 ya kikundi hicho ilionyesha kwamba magonjwa yanayosababishwa na hali ya usugu wa dawa yanaweza kusababisha vifo milioni 10 kila mwaka kufikia 2050 na uchumi kuwa mbaya kama janga la kifedha la kimataifa la 2008-2009. Kufikia 2030, hali ya usugu wa dawa za kuua viini itaweza kulazimisha hadi watu milioni 24 kujikuta katika umaskini uliokithiri.

Uzalishaji wa mayai

Kulingana na Dkt.Stella Kiambi, mwanaepidemiolojia wa FAO, moja ya matatizo makubwa katika uzalishaji wa kilimo ni kwamba baadhi ya wakulima hawafahamu athari za dawa wanazotumia kwa wanyama wao.

"Katika utafiti uliofanywa na Kaunti ya Nyeri nchini Kenya, mhudumu wa agroveti (duka la bidhaa za kilimo na mifugo) alisema kwamba mkulima anapokuja na kusema kwamba kuku wake wamepunguza kuzalisha mayai, mhudumu ataangalia lebo za dawa zinazopatikana na ikiwa inasema inaboresha uzalishaji wa mayai, basi atampa mteja dawa hiyo," alisema.

Dkt. Kiambi alisema wanafanya kazi na mamlaka husika kuhakikisha kwamba suala la kuweka lebo kwenye dawa linatatuliwa ili kuepuka matumizi mabaya ya dawa hizi.

"Suala jingine ni kwamba viwango vya usalama-biolojia na usafi ni vya chini sana miongoni mwa baadhi ya wanajamii, pamoja na wakulima. Suluhisho linaweza kuwa ni kuimarisha huduma za ugani za kilimo ili kusaidia kuelimisha wakulima kuhusu njia bora ili waelewe baadhi ya tahadhari za kimsingi wakati wakitumia kemikali hizi," Dkt. Kiambi alisema. 

Hata hivyo, hali ni ileile katika nchi nyingi za Afrika Mashariki, na ndani ya ukanda huu, ambazo pia zinahangaika na usugu wa dawa za kuua viini. 

Nchini Tanzania

Dkt. Deus Kitapondya, daktari anayetoa dawa za dharura kwa jamii jijini Dar-es-Salaam anasema hali ya usugu wa dawa za kuua viini pia ni tatizo nchini Tanzania, ingawa hakuna takwimu halisi kuhusu athari yake nchini humo.

"Tatizo ni kwamba uingizaji, uuzaji, na utoaji wa baadhi ya dawa hizi haujadhibitiwa barabara. Mtu yeyote anaweza kuingia katika duka la dawa na kuzinunua bila mapendekezo yanayofaa kutoka kwa daktari aliyehitimu," asema Dkt. Kitapondya.

Ili kufikia matumizi salama ya dawa, lazima dozi ziwe sahihi ili kuhakikisha ufanisi katika kutibu hali husika.

Kadhalika, Dkt. Kitapondya alisema kwamba njia moja ya kukabiliana na tatizo hilo ni kuweka maaabara za kutosha na zenye ufanisi zinazoweza kutumika kujaribu dawa zinazotumika kupambana na viini [upimaji husaidia kutambua jinsi dawa inavyopambana na viini].

Kadhalika, alisema kwamba ni muhimu kuelimisha watu kuhusu hatari za kutumia antibayotiki bila maelekezo yanayofaa kutoka kwa daktari aliyehitimu. 

Kila mwaka kati ya tarehe 18 na 25 Novemba, ulimwengu huadhimisha Wiki ya Kuhamasisha kuhusu Dawa za Kuua Viini Duniani (WAAW). Mwaka 2021, tukio hilo liliadhimishwa chini ya kaulimbiu, "Sambaza Ufahamu, Komesha Hali ya Usugu", iliyotoa mwito kwa wadau wa afya, watunga sera, watoa huduma za afya na umma kwa ujumla kuwa mabalozi wa Kuhamasisha kuhusu Hali ya Usugu wa Dawa za Kuua Viini (AMR).

 

 

More from this author