AfCFTA: Sekta ya uchukuzi barani Afrika kunufaika kutokana na biashara huru

Get monthly
e-newsletter

AfCFTA: Sekta ya uchukuzi barani Afrika kunufaika kutokana na biashara huru

Biashara kupitia barabara, reli, ndege na huduma za usafiri wa meli kuongezeka kwa 50%
Afrika Upya: 
11 February 2022
Franck Kuwonu/AR
Africa’s road network is inadequate but implementing planned projects will significantly increase its size.

Eneo la Biashara Huru Barani Afrika (AfCFTA) linatarajiwa kuongeza biashara miongoni mwa nchi za Afrika katika huduma za usafiri kwa takriban kwa asilimia 50, kulingana na makadirio ya hivi karibuni ya Kamisheni ya Uchumi ya Afrika (ECA). 

Makadirio ya, 'Athari za Eneo la Biashara Huru Barani Afrika kutokana na uhitaji wa usafiri, miundombinu na huduma' yaliyotolewa na ECA katika Kongamano la tano la Kibiashara la Afrika mnamo tarehe 7 Februari, yanaashiria kwamba baada ya AfCFTA kuanzishwa kikamilifu, zaidi ya asilimia 25 ya  mapato ya biashara ya ndani ya Afrika kutokana na huduma itaenda kwenye usafiri pekee; na takriban asilimia 40 ya ongezeko katika uzalishaji wa huduma barani Afrika itakuwa katika usafiri.

Utafiti uliofanywa na wataalamu katika kitengo cha nishati, miundombinu na huduma cha ECA kinaweka wazi fursa za uwekezaji za AfCFTA  katika sekta ya usafirishaji.

Vera Songwe, Afisa wa Umoja wa Mataifa chini ya Katibu Mkuu na Katibu Mtendaji wa ECA alisema kwamba AfCFTA “inatarajiwa kuongeza kwa kiasi kikubwa mitiririko ya trafiki kwenye njia zote za usafiri: Barabara, Reli, Maji na Angani," lakini hatua hizo zitafanikiwa tu kama AfCFTA itaendana na utekelezaji wa miradi ya miundombinu ya kikanda.

Robert Lisinge, Mkuu wa Kitengo cha Nishati, Miundombinu na Huduma katika ECA, alisema “barabara kwa sasa zinachukua mgao mkubwa wa uchukuzi barani Afrika.” Alisema kwamba “AfCFTA inatoa fursa ya kujenga mtandao wa reli barani Afrika. Hii itaongeza hitaji la uchukuzi wa ndani ya Afrika kwa asilimia 28; hitaji la uchukuzi wa meli litaongezeka zaidi."

Kulingana na matokeo ya utafiti, AfCFTA itahitaji lori 1,844,000 za mizigo mikubwa na lori 248,000 za kontena za mizigo kufikia 2030. Hii inaongeza lori 1,945,000 na 268,000 kwa pamoja ikiwa miradi ya miundombinu iliyopangwa pia itatekelezwa.

Hitaji kubwa zaidi la malori kusaidia AfCFTA linatoka Afrika Magharibi (asilimia 39); hitaji kutoka Afrika ya Magharibi hadi Kusini ni asilimia 19.8 na kutoka Afrika ya Kusini hadi Afrika ya Magharibi kwa asilimia 9.9.

Maswali muhimu yaliyozingatiwa kwenye utafiti yalikuwa ni kwa vipi utekelezaji wa AfCFTA utaathiri hitaji la miundombinu ya usafiri na huduma? Hitaji la njia mbalimbali za usafiri ni kiasi gani, na athari za kuwekeza katika maendeleo ya miundombinu ni zipi? ​

Je, mahitaji ya miundombinu na vifaa kwa njia mbalimbali za usafirini yatakuwa ni kwa kiasi gani?​

Bw. Lisinge alibaini kwamba AfCFTA na programu za miundombinu ya uchukuzi barani Afrika zinahusiana kwa karibu na zinapaswa kutekelezwa kwa pamoja. Alisema, Mamlaka ya Barabara Kuu za Afrika (TAH) na Mpango wa Maendeleo ya Miundombinu (PIDA) na Soko Moja la Usafiri wa Anga Afrika (SAATM) vinapaswa kupewa kipaumbele sawa na AfCFTA.​

Usafiri wa Barabarani

"Mtandao wa barabara Afrika hautoshi lakini utekelezaji wa miradi iliyopangwa utaongeza ukubwa wake kwa kiasi kikubwa. Afrika inahitaji kuboresha sehemu za barabara zake ili kukabiliana na ongezeko la uchukuzi linalosababishwa na AfCFTA," alisema Bw Lisinge.

"Ukuaji wa trafiki ya uchukuzi unatazamiwa kuwa mkubwa katika baadhi ya sehemu za mitandao ya Barabara za Afrika kuliko kiasi cha ukuaji wa wastani katika bara zima. Utekelezaji wa AfCFTA utakuza maradufu uchukuzi kwa barabara kutoka tani milioni 201 hadi tani milioni 403."

Utekelezaji wa miradi ya TAH na PIDA, alisema, unaongeza uwezo wa mitandao ya barabara kuwezesha ukuaji wa uchukuzi. Kuvuna manufaa makubwa ya AfCFTA katika sekta ya uchukuzi kunahitaji utekelezaji wa programu za miundombinu na huduma za kikanda.

Usafiri wa Reli

Kuhusu usafiri wa reli, ECA inakadiria kwamba mtandao wa reli ya Afrika hautoshi, lakini utekelezaji wa PIDA na miradi mingine iliyopangwa utaongeza kwa kiasi kikubwa ukubwa wake. Utekelezaji wa miradi iliyopangwa utaongeza mtandao kwa takriban kilomita 26,500.

AfCFTA itahitaji magari 97,614 ya kubeba mizigo mikubwa na magari 20,668 ya kubeba kontena za mizigo ifikapo mwaka 2030. Hii inaongeza hadi magari 132,857 na 36,482 kwa pamoja ikiwa miradi ya miundombinu iliyopangwa pia itatekelezwa.

Usafiri wa meli

Utekelezaji wa AfCFTA utaongeza maradufu usafiri wa meli kutoka tani milioni 58 hadi tani milioni 131.5. Mtandao wa meli barani Afrika unajumuisha viungo 142 vinavyounganisha bandari 65 na kuchangia 22.1% ya usafirishaji wa ndani ya Afrika. Mgao utaongezeka kutoka 0.6% hadi 22.7% ikiwa AfCFTA na miradi ya miundombinu iliyopangwa itatekelezwa.

AfCFTA itahitaji meli 126 za shehena kubwa na meli 15 za kontena za shehena ifikapo mwaka 2030. Hii inapunguza meli 121 na 14 mtwalia ikiwa miradi ya miundomsingi iliyopangwa pia itatekelezwa.

Usafiri wa anga

Mtandao wa usafiri wa anga barani unajumuisha jumla ya njia za anga 14,762 (unaunganisha kila uwanja wa ndege na viwanja vingine 121 vya ndege).

Utekelezaji wa AfCFTA unaweza kuongeza maradufu idadi ya tani zinazosafirishwa kwa ndege kutoka milioni 2.3 hadi milioni 4.5.

Mwaka 2019, usafiri wa anga ulichangia 0.9% pekee ya uchukuzi wa mizigo ndani ya Afrika. Utekelezaji wa AfCFTA utaongeza maradufu usafirishaji kwa njia ya anga kutoka tani milioni 2.3 hadi tani milioni 4.5. Hivyo, usafiri wa anga unatarajiwa kuongezeka maradufu ifikapo mwaka 2030 ikilinganishwa na mwaka 2019.

Kuhusu AfCFTA

Makubaliano ya Eneo la Biashara Huru Barani Afrika (AfCFTA) yalifanywa mwaka 2019. Utekelezaji wake ukaanza 2021.

Makubaliano bado yanaendelea kuhusu uwekezaji, hakimiliki, sera ya ushindani na biashara ya mtandaoni. Lengo la AfCFTA ni kuunda soko moja barani kwa bidhaa na huduma, kukiwa na uhuru wa watu kutoka sehemu moja kwenda sehemu nyingine na uwekezaji, kuimarisha hali ya ushindani na kuwezesha mabadiliko ya kiuchumi.

Mada: