UNAIDS yaonya kuhusu mamilioni ya vifo vinavyohusiana na UKIMWI na hujuma zinazoendelezwa na majanga kama viongozi hawatakabili tofauti

Get monthly
e-newsletter

UNAIDS yaonya kuhusu mamilioni ya vifo vinavyohusiana na UKIMWI na hujuma zinazoendelezwa na majanga kama viongozi hawatakabili tofauti

Kumaliza tofauti ni uamuzi wa kisiasa unaohitaji mageuzi madhubuti ya kisera na fedha
Afrika Upya: 
1 December 2021
Na: 
.

Mpango wa pamoja wa Umoja wa Mataifa kuhusu VVU/UKIMWI umetoa onyo kali kwamba iwapo viongozi hawatazikabili tofauti, ulimwengu unaweza kushuhudia vifo milioni 7.7* vinavyohusiana na Ukimwi katika miaka 10 ijayo. 

UNAIDS inaendelea kuonya kwamba iwapo hatua za kimageuzi yanayohitajika kuuangamiza ukimwi hazitachukuliwa, ulimwengu utaendelea kunaswa na tatizo la COVID-19 na kusalia katika hali ya mbaya ya kutojiandaa kwa majanga ya baadaye.

“Huu ni wito wa dharura kuchukua hatua,” alisema Mkurugenzi Mkuu wa UNAIDS Winnie Byanyima. 

“Hatua dhidi ya janga la UKIMWI, ambazo tayari zilikuwa dhaifu, zinatatizika hata zaidi sasa huku tatizo la COVID-19 likiendelea kutamalaki, huku zikitatiza hudumua za uzuiaji na matibabu, mafundisho, uzuiaji wa dhuluma na nyinginezo,” alisema. Hatuwezi kulazimishwa kuchagua kati ya kuliangamiza janga la ukimwi leo na kufanya maandalizi dhidi ya majanga ya kesho. Mwelekeo fanifu pekee ndio utayatimiza yote. Kwa sasa, hatuko katika mkondo sahihi wa kulitimiza lolote.”

Onyo hiyo inatolewa kupitia Ripoti Mpya ya UNAIDS iliyozinduliwa kabla ya Siku ya UKIMWI Ulimwenguni  yenye mada Isiyo na Usawa, isiyojiandaa, inayokabiliwa na tishio: haja ya kuwa na hatua madhubuti dhidi ya tofauti ili kuangamiza UKIMWI kusitisha COVID-19 na kujiandaa kwa majanga ya siku za usoni.

Baadhi ya mataifa, ikiwa ni pamoja na yale yenye viwango vya juu VVU, yamepiga hatua kuu dhidi ya UKIMWI, huku yakidhihirisha yanayowezekana.

Hata hivyo, maambukizi mapya ya VVU hayapungua kwa kasi inayotakikana ulimwenguni ili kulisitisha janga hili, huku kukiwa na maambukizi mapya milioni 1.5 mwaka 2020 na kuongeza viwango vya maambukizi katika baadhi ya mataifa

Maambukizi yanafuata mikondo ya tofauti pia. Maambukizi mapya sita juu ya saba ya UKIMWI miongoni mwa vijana waliobalehe katika Afrika Kusini mwa Sahara yanatokea miongoni mwa wasichana waliovunja ungo.

Masenge na wanaume wanaoshiriki ngono na wanaume wenzao, makahaba na watumizi wa dawa za kulevya wamo katika hatari zaidi ya mara 25–35 ya kupata VVU ulimwenguni kote.

COVID-19 inadhoofisha uwajibikiaji wa UKIMWI katika maeneo mengi

Kasi ya kupima VVU ilididimia karibu kwa upatani na watu wachache sana wanaoishi na VVU walianza matibabu mwaka 2020 katika mataifa 40 kati ya 50 yanayoripoti kwa UNAIDS.

Huduma za kuzuia VVU zimeathiriwa—mwaka 2020, huduma za kupunguza makali kwa wanaotumia dawa za kulevya zilitatizwa katika 65% ya mataifa 130 yaliyochunguzwa.

“Bado inawezekana kulimaliza janga hili kufikia 2030,” aliyakinisha Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres katika ujumbe wake Siku ya Ukimwi Duniani. “Lakini hilo litahitaji hatua zaidi na ushirikiano mkuu. Ili kuushinda UKIMWI—na kuujenga unyumbufu dhidi ya majanga mengine ya siku za usoni—tunahitaji hatua za pamoja.”

Ripoti hii mpya kutoka UNAIDS inatathmini vipengele vitano muhimu kuhusu mpango uliokuibaliwa na Mataifa Wanachama wa Mkutano wa Upeo wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kuhusu UKIMWI unaostahili kutekelezwa kwa dharura ili kusitisha janga la UKIMWI  na ambavyo ni muhimu ila vinayopokea ufadhili finyu na kutopewa kipaumbele katika kuzuia janga hili, maandalizi na uwajibikiaji.

Vinajumuisha:

  • Miundomsingi inayoongozwa na jamii.
  • Uwezo sawa wa kupata dawa, chanjo na teknolojia za kiafya.
  • Kuwasaidia wafanyakazi walio katika mistari ya mbele ya majanga.
  • Haki za kibinadamu katika kitovu cha uwajibikiaji majanga.
  • Mifumo ya data inayolenga watu ambayo inazibainisha tofauti. 

Wito wa kuongeza uwekezaji na mabadiliko katika sheria na sera kuzimaliza tofauti zinazoendeleza UKIMWI na majanga mengine unapigwa jeki na viongozi katika afya ya kimataifa na uwajibikiaji majanga ulimwenguni kote.

“Tusipozichukua hatua zinazohitajika kuzikabili tofauti zinazoendeleza VVU leo, hatushindwa tu kuliangamiza janga la UKIMWI, bali pia tutuuwacha ulimwengu wetu katika hali hatari za maandalizi ya kuyakabili majanga ya siku za usoni,” alisema Helen Clark, Mwenyekiti mwenza wa Jopo Huru la Maandalizi na Uwajibikiaji Majanga, katika dibaji maalumu ya ripoti ya UNAIDS.

“Majanga hupata fursa ya kukua katika mianya ya jamii zilizogawika. Wanasayansi hodari, madaktari, wauguzi na jamii zinazojizatiti kuyaangamiza majanga hawawezi kufaulu iwapo viongozi wa kimataifa hawatachukua hatua zitakazowawezesha kufaulu,” aliongeza.

Viongozi wanaweza kuchukua hatua za madhubuti

UNAIDS na wataalamu wa afya wa kimataifa wanasisitiza kwamba ingawaje mazoea yanaweza kuwaua mamilioni  na kuuwacha ulimwengu na majanga mengi kwa miongo mingi, viongozi wanaweza, kwa kushirikiana kuzikabili kijasiri tofauti ambazo hutoa mazingira murwa kwa majanga kunawiri, kuangaizi UKIMWI, kulishinda tatizo la  COVID-19 na kulinda kutokana na majanga ya siku za usoni.

“Viini vya magonjwa kuanzia VVU hadi kwa virusi vya COVID-19 vinazishambulia nyufa na migawanyiko ya jamii yetu kwa ubinafsi wa kushangaza,” alisema Paul Farmer wa Partners in Health, shirika lisilo la faida ambalo limekuwa likitibu UKIMWI kwa uafanisi kwa miongo mingi katika mazingira ya umaskini mkuu wa mali.

“Hali kwamba janga la UKIMWI linaelekezwa kwa tofauti kuu za kimuundo haistahili kutufanya kutochukua hatua, hata hivyo. Timu zetu, katika maeneo ya mashambani ya Haiti na ulimwenguni kote, zimeonyesha kila mara kwamba uangalizi mkamilifu ukitolewa, kukiwa na miundo thabiti ya uandamnaji na msaada wa kijamii na haki kuu ya kijamii, tofauti katika matokeo ya UKIMWI zinaweza kupungua kwa kasi, na mifumo ya kijamii ikaimarishwa upesi. Hatustahili kuridhika na mengine machache,” alisema. 

Huu ni mwaka wa 40 tangu kisa cha kwanza cha UKIMWI kuripotiwa. Tangu wakati huo, ambako uekezaji umesadifiana na nia, kumekuwa na maendeleo makuu, haswa katika kupanua ufikiaji matibabu.

Kufikia Juni 2021, watu milioni 28.2 walikuwa na uwezo wa kupata matibabu, kutoka milioni 7.8 mwaka 2010, japo kasi ya maendeleo imepungua sana.

Mataifa yaliyo na sheria na sera zinazolenga ushahidi, uhusishaji na ushirikishi madhubuti wa jamii na mifumo thabiti na jumuishi ya afya yamekuwa na matokeo bora, ilhali kanda zenye tofauti kubwa zaidi za raslimali na mataifa yenye sheria kandamizi na ambayo hayajaufuata mwelekeo wa haki yamekuwa na matokeo mabaya zaidi.

“Tunajua taratibu faafu kwa kuona uwajibikiaji bora wa UKIMWI katika baadhi ya maeneo,” Bi Byanyima alisema, “lakini tunastahili kuzitekeleza kila mahali kwa kila mtu. Tuna mkakati fanifu uliochukuliwa na viongozi mwaka huu, ila unastahili kutaekelezwa kikamilifu. Kumaliza tofauti ili kuuangamiza UKIMWI ni uamuzi wa kisiasa na mageuzi thabiti ya kisera na fedha. Tumefika wakati wa kuamua. Uamuzi unaostahili kufanywa na viongozi ni kati ya hatua madhubuti na hatua dhaifu.”

* Makadirio ya vifo milionin7.7 vinavyohusiana na UKIMWI kati ya 2021 na 2030 ni vile ambavyo vielelezo vya UNAIDS vinatabiri iwapo utoaji wa huduma za VVU zitasalia katika viwango vya 2019. Kama mkakati wa kimataifa wa UKIMWI 2021–2026: Maliza tofauti, Angamiza UKIMWI utatekelezwa na shabaha za 2025 kutimizwa, UNAIDS inakadiria kwamba angalau milioni 4.6 ya vifo hivyo vinaweza kuzuiwa kwa kipindi cha mwongo huo.

Mada: