COP26 inayohitaji Afrika

Get monthly
e-newsletter

Washiriki wa Glasgow kwa Mkutano wa Umoja wa Mataifa wa Mabadiliko ya Tabianchi.
UN Climate Change
Washiriki wa Glasgow kwa Mkutano wa Umoja wa Mataifa wa Mabadiliko ya Tabianchi.

Viongozi wa dunia wanapokutana Glasgow kwa ajili ya Mkutano wa Umoja wa Mataifa wa Mabadiliko ya Hali ya Hewa, Afrika inahitaji zaidi hatua madhubuti za pamoja badala ya maneno ya kutia moyo. Hasa, nchi tajiri zinapaswa kuunga mkono maelezo ya sehemu nne za kifedha na biashara ambayo yanaweza kuhakikisha mabadiliko ya rasilimali kwenye kanda.

ABIDJAN – Takriban miaka miwili ya janga la COVID-19, hali ya kutofautiana ya mkabilio ya kimataifa wa janga hili iko wazi.

Ingawa nchi chache sana za Kiafrika zimeweza kutumia asilimia 1 ya Pato lao la Taifa ili kukabiliana na dharura hii ya afya ambayo haijawahi kushuhudiwa, mataifa ya Magharibi yamekusanya zaidi ya dola trilioni 10, au asilimia 30 ya Pato lao la Taifa kwa pamoja, ili kukabiliana na janga hili.

Ulaya na Marekani zimechanja kwa kikamilifu 75%  na 70% mtawaliwa ya watu wazima dhidi ya COVID-19, lakini ni chini ya asilimia 6 ya Waafrika, wamechanjwa. Na huku baadhi ya nchi za Magharibi tayari zikitoa chanjo za ziada, Afrika bado haipati hata dozi za kwanza.

Ukosefu wa usawa huu wa kimfumo unaonekana katika juhudi za kushughulikia janga la hali ya hewa. Maafa ya hali ya hewa, kama vile virusi, hayajui mipaka. Lakini huku serikali za Kaskazini mwa Dunia zikiwa zinakabili matukio kama haya kwa kukopa kwenye masoko ya mtaji kwa gharama za chini ili kufadhili vichocheo na uwekezaji, nchi za Kiafrika lazima zitegemee ama mtiririko wa fedha kupitia mipango ya kusitisha kulipia deni, ahadi za misaada, au ufadhili ghali mno kupitia soko la mtaji. Kwa sasa hakuna chaguzi kati yazo zinazopatia chumi hizi uwekezaji wa awali wa mtaji unaohitaji ili kuboresha matarajio yao ya muda mrefu.

Viongozi wa dunia wanapoelekea Glasgow kwa Kongamano la Umoja wa Mataifa la Mabadiliko ya Hali ya Hewa (COP26), Afrika inahitaji zaidi hatua madhubuti za pamoja badala ya maneno ya kutia moyo tu. Kwa hivyo tunapendekeza mgao wa kimkakati wa kifedha na biashara ambao unaweza kubadilisha ukosefu wa usawa katika mabadiliko ya hali ya hewa na kuwa jumuishi kwa kuhakikisha mabadiliko ya rasilimali kutoka kwa watoa gesi chafu (GHG) kwenda Afrika.

Mpango wetu una msingi wake kwenye nguzo nne:

Kwanza, chumi zinazostawi lazima zitimize ahadi zilizotoa katika mkataba wa hali ya hewa wa Paris wa 2015 wa kutoa dola bilioni 100 kwa mwaka ili kusaidia kufidia gharama za urekebashiji na mpito za nchi zinazoendelea. Hatimaye, ahadi ambazo nchi zinazostawi zilitoa huko Paris zilikuwa na masharti kuyahusu.

Kushindwa kutimiza ahadi hizi ambazo sasa zimechelewa, huku nusu ya dola bilioni 100 ikitengewa gharama za kukabiliana na hali hizi, kunakwaza kanuni yenyewe ya hatua za nchi nyingi. Ni kifungu katika makubaliano ya kimataifa, na lazima kitimizwe.

Ukweli kwamba nchi zilizostawi zilikusanya dola trilioni 10 kukabiliana na janga hili katika mwaka 2020 pekee unaonyesha jinsi kiasi cha dola bilioni 100 kwa mwaka kilivyo kidogo. Hata hivyo, katika kipindi hicho, usaidizi rasmi wa maendeleo uliongezeka kwa asilimia 3.5 pekee katika hali halisi.

Nguzo ya pili ni kuwianisha masoko ya fedha na malengo ya makubaliano ya Paris. Kujumuisha athari za mabadiliko ya hali ya hewa katika maamuzi ya uwekezaji ni muhimu, na uwekaji bora wa mitaji ya kibinafsi katika sekta za kijani kibichi utabadilisha nchi za Kiafrika na nchi zinazoendelea kwa ujumla.

Ili kutimiza hilo, Muungano wa Kifedha wa Glasgow wa Net Zero, unaoongozwa na aliyekuwa Gavana wa Benki Kuu ya Uingereza, Mark Carney, umeleta pamoja makampuni yenye mali ya dola trilioni 90 trilioni.

Furahia ufikiaji usio na kikomo wa mawazo na maoni ya mabingwa duniani, ikijumuisha makala ya kila wiki, tahakiki za vitabu, mikusanyiko ya mada na mahojiano; Jarida la The Year Ahead machapisho ya kila mwaka; kumbukumbu kamili ya PS; na zaidi - kwa chini ya dola 9 kwa mwezi.

Ni sharti sasa kuwe na juhudi za haraka na zilizodhamiriwa za kuelekeza ufadhili huu wa kibinafsi katika sekta zinazohifadhi hali ya hewa barani Afrika na nchi zingine zinazoendelea. Kwa kuzingatia hilo, Tume ya Umoja wa Mataifa ya Kiuchumi ya Afrika mapema mwaka huu ilipendekeza mfuko wa kifedha na uendelevu unaolenga kupunguza gharama za kukopa zinazohusishwa na uwekezaji katika kijani kibichi kwa kuendeleza soko la ununuzi upya (“repo”) kwa ajili ya bara.

Mkakati huo, ambao kwa hakika utafadhiliwa kupitia ufadhili wa mwanzo wa dola bilioni 3 katika haki maalum (mali ya akiba ya Shirika la Fedha la Kimataifa), unanuiwa kuondoa hatari za uwekezaji wa kibinafsi barani Afrika na kusaidia kanda kuongeza hisa yake - kwa sasa iliyo chini ya asilimia 1 – ya soko la kimataifa la dhamana ya kijani kibichi.

Jamhuri ya Afrika Kusini hivi majuzi ilitoa dhamana ya kijani ya bilioni 3 (dola milioni 196) ili kufadhili upya sekta yake ya nishati. Matoleo kama haya ni mfano wa aina ya uwekezaji unaowezekana kwa kufungua soko la dhamana kwa Afrika. Tunahitaji kufanya uwekezaji kama huo kuwa sheria badala ya kwa hiari.

Aidha, Kundi la Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) limependekeza kuanzishwa kwa Mfumo wa Uthabiti wa Kifedha wa Afrika. Mpango kama huo utasaidia kuzuia vikwazo vya kifedha vya siku zijazo barani Afrika - bara pekee lisilo na Mpangilio wa Ufadhili wa Kikanda - kutokana na athari mbaya.

Nguzo ya tatu ni kutoa rasilimali muhimu zinazohitajika na Afŕika kuwezesha uchumi wake kukabiliana na ongezeko la joto duniani. Mabadiliko ya hali ya hewa yatagharimu bara hili dola bilioni 7-15 kila mwaka na yanatishia usalama wa chakula na matumizi ya nishati inayozalishwa kwa maji. Lakini Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara, ambayo inayozalisha GHC iliyo chini ya asilimia 4 duniani, inapokea tu asilimia 5 ya jumla ya fedha za mbadiliko ya hali ya hewa nje ya OECD.

Badala ya kusubiri tu ufadhili kama huo kutekelezwa, Afrika inakabiliana mabadiliko ya hali ya hewa vilivyo kwa kutumia masuluhisho ya kinyumbani. Kwa sasa AfDB inatoa asilimia 63 ya fedha zake za hali ya hewa kwa kukabiliana na hali hiyo, sehemu kubwa zaidi ya taasisi yoyote ya fedha ya kimataifa, na imejitolea kuongeza ufadhili huo maradufu hadi dola bilioni 25 ifikapo 2025. AfDB na Kituo cha Urekebishaji wa Kidunia pia kimeunda Programu ya Haraka ya Urekebishaji (AAAP) ili kusaidia kuongeza uwekezaji wa benki wa kukabiliana na madabiliko ya hali hewa katika eneo hili. Uchangishaji wa dola bilioni 25 kupitia AAAP utakuwa hatua ya kwanza kuelekea kwenye uwekezaji wa kufufua hali ya kijani barani Afrika.

Mwishowe, suluhu yoyote ya mabadiliko ya hali ya hewa lazima ishughulikie biashara, ambayo ndiyo uti wa mgoingo wa uchumi wa dunia. Ufunguo wa kukomesha udhaifu wetu wa sasa wa kiuchumi ni kuhakikisha uwazi unaoendelea na uthabiti, ikijumuisha kujitolea kwa sheria za biashara za kimataifa ambazo zinaambatana na malengo ya makubaliano ya Paris.

Jumuiya za kikanda kama vile Eneo la Biashara Huru la Afrika (AfCFTA) zinaweza kutoa msukumo wa kuimarisha dhamira yetu ya maendeleo yanayozalisha kaboni kidogo.

Ni lazima tutambue mahitaji mahususi ya Afrika, tutambue kuathiriwa kwa bara hili na mabadiliko ya hali ya hewa, na kubainisha maeneo na kanda na jamii ambazo athari zake zimemesababisha madhara zaidi.

Mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa kuhusu hali ya hewa mwaka ujao, COP27, utafanyika barani Afrika, na tunatazamia kuukaribisha ulimwengu. Lakini nchi zilizostawi lazima zitimize ahadi zao za muda mrefu kuhusu hali ya hewa kwa eneo hili kabla ya wakati huo - kuanzia Glasgow.

Akinwumi A. Adesina ni Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika.

Ngozi Okonjo-Iweala, ambaye ni Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Biashara Duniani, pia alikuwa Mkurugenzi Mkuu katika Benki ya Dunia awali, waziri wa fedha wa Nigeria, mwenyekiti wa bodi ya Gavi, Muungano wa Chanjo, na mjumbe maalum wa Umoja wa Afrika kuhusu COVID-19. Ni mtafiti katika Taasisi ya The Brookings Institution na Kiongozi wa Kimataifa wa Umma katika  Shule Kuu ya  Utawala ya John F. Kennedy, Chuo Kikuu chs Havard.

Vera Songwe ni Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa na Katibu Mtendaji wa Tume ya Uchumi ya Umoja wa Mataifa ya Afrika.

Ibrahim Assane Mayaki, Waziri Mkuu wa zamani wa Niger, ni Mkurugenzi Mtendaji wa African Union Development Age

Mada: 
More from this author