Benki ya Maendeleo ya Afrika, Tume ya Umoja wa Afrika (AUC), na UNECA zinaahidi kutoa fedha ili kuimarisha usimamizi wa ardhi barani Afrika

Get monthly
e-newsletter

Benki ya Maendeleo ya Afrika, Tume ya Umoja wa Afrika (AUC), na UNECA zinaahidi kutoa fedha ili kuimarisha usimamizi wa ardhi barani Afrika

Afrika Upya: 
11 Novemba 2021
Na: 
Mkutano wa 2021 wa Sera ya Ardhi Barani Afrika.
UNECA
Mkutano wa 2021 wa Sera ya Ardhi Barani Afrika.
Ikiwa huwezi kusoma sasa, sikiliza tu toleo la sauti: 
Sauti ya Kiingereza

Benki ya Maendeleo ya Afrika, Tume ya Umoja wa Afrika (AUC), na Tume ya Umoja wa Mataifa kuhusu Uchumi wa Afrika (UNECA) zimeahidi kufanya kazi kwa karibu zaidi na serikali ili kuimarisha mifumo ya utawala wa ardhi.

Katika azimio la pamoja mwishoni mwa Kongamano la 2021 la Sera ya Ardhi barani Afrika lililofanyika Kigali, Rwanda huvi karibuni, mashirika haya yaliahidi kutoa msaada wa kifedha na kiufundi "kuhakikisha kwamba usimamizi wa ardhi na michakato ya sera ya ardhi barani Afrika ina uwazi, ni pana na inapatikana na kwamba mifumo ya serikali na ya kijadi inaunganishwa kwa urahisi.”

Pia waliahidi kushirikiana na wataalamu wa sanaa, utamaduni na turathi ili kuboresha uelewa na kuthamini masuala ya ardhi barani.

Mada ya kongamano hilo ilikuwa "Utawala wa Ardhi kwa ajili ya kulinda sanaa, utamaduni na turathi kuelekea Afrika Tunayoitaka."

Serikali ya Rwanda iliandaa hafla ya mwaka huu kwa njia mseto, huku washiriki wakikusanyika ana kwa ana mjini Kigali na wengine mtandaoni. Waandaaji walijumuisha sanaa na utamaduni katika kongamano hilo, wakisisitiza nguvu ya sekta ya sanaa katika masuala ya ardhi.

"Wakati huu ambapo dunia nzima inashiriki katika mchakato wa COP26, tunataka kusisitiza ukweli kwamba sehemu kubwa za bara letu ni jangwa au nusu kame na inakabiliwa na uharibifu wa mfumo wa mazingira. Hata hivyo, mara nyingi, ugavi usio sawa wa ardhi umechangia kuongezeka kwa idadi ya wakulima wadogo, wanawake na vijana kwenye maeneo yaliyotelekezwa, na kusababisha shinikizo la ongezeko la uharibifu wa ardhi na rasilimali za ardhi, " azimio hilo lililosomwa na Leontine Kanziemo, Mshauri wa Usimamizi wa Maliasili katika Benki ya Maendeleo ya Afrika lilieleza.

Azimio hilo lilitoa wito wa kuwepo kwa usawa zaidi wa ardhi ili kupanua upatikanaji wa maliasili. Azimio hilo pia lilieleza kuwa ni muhimu kushirikiana na serikali, wasanii na viongozi wa kitamaduni ili kuhakikisha kuwa wanawake na vijana wanapata ardhi. "Wengi wa watu wetu wanategemea ardhi kujitafutia riziki. Kwa hivyo, sera ya ardhi inayopendelea maskini inapaswa kuwa wazi kwa watumiaji wote wa ardhi, yenye usawa na bila ufisadi,” washirika hao walisema.

Kongamano la 2021 la Sera ya Ardhi barani Afrika.
UNECA

Azimio hilo lilitoa wito  kuwa watunzaji wa kijadi wa sanaa, urithi na utamaduni wa Kiafrika wajumuishwe katika sera zote za ardhi zinazopendelea maskini. "Aidha, baada ya Mkutano Mkuu wa Mfumo wa Chakula wa Umoja wa Mataifa uliokamilika hivi majuzi, utawala wa ardhi unapaswa kuchukuliwa kama kiwezeshaji kikuu katika mageuzi ya mifumo ya chakula ya Kiafrika."

Naye Mfalme Mfumu Difima Ntinu, Rais wa Mamlaka ya Kijadi ya Afrika, alieleza kuwa utawala bora wa ardhi unahitaji nia njema ya kisiasa na kuzitaka nchi za Afrika kuzingatia zaidi nafasi ya wanawake katika masuala ya ardhi. "Kwa usaidizi wenu, tutafika," aliongezea.

Katika maelezo yake, Rexford Ahene, Mwenyekiti wa Kamati ya Kisayansi ya Kongamano hilo, alisema kuwa kuna uhusiano kati ya ardhi na viwanda vya sanaa, akisema uwezo wa kiuchumi wa ardhi, na manufaa ya viwanda vya sanaa, haupaswi kupuuzwa.

Kulingana na Baraza la Biashara na Utalii Duniani, viwanda vya sanaa vitaongeza dola bilioni 269 kwenye Pato la Bara la Afrika ifikapo 2026 na zaidi ya ajira milioni 29 zenye ujuzi unaovutia vijana. "Ni muhimu kuzingatia hilo," Bw. Ahene alieleza.

Alitoa wito kwa serikali na washirika wa maendeleo kuwekeza rasilimali katika kuboresha uwezo wa sekta ya sanaa na kuhifadhi hakimiliki na haki ili "kulinda na kuhifadhi ubunifu na uvumbuzi unaozalishwa na sekta hii."

Kongamano kuhusu Sera ya Ardhi Barani Afrika, ambalo hufanyika kila baada ya miaka miwili, liliandaliwa na Kituo cha Sera ya Ardhi cha Afrika, mkakati wa pamoja wa UNECA, AUC na Benki ya Maendeleo ya Afrika.