Wanawake katika siasa: ni maili nyingi kabla ya kutimiza usawa

Get monthly
e-newsletter

Wanawake katika siasa: ni maili nyingi kabla ya kutimiza usawa

Zipporah Musau
8 April 2019
Women discuss politics at a women’s conference in Darfur, Sudan.
Alamy Photo/Richard Baker
Wanawake wanazungumzia siasa katika mkutano wa wanawake huko Darfur, Sudan.

Wanawake ulimwenguni wameendelea kwa namna tofauti katika kupigania usawa wa kijinsia. Hata hivyo, kwa wanawake barani Afrika, maendeleo hayo ni machache mno na bado kuna mengi ya kufanya ili kufikia lengo.

Habari njema ni kwamba uwakilishi wa wanawake katika maamuzi ya kisiasa umekuwa ukiimarika kimataifa. Habari za kusikitisha ni kwamba kuimarika huko kumekuwa kwa kasi ya chini kabisa, 1% tu katika mwaka wa 2018 ikilinganishwa na mwaka uliotangulia. Mwaka wa 2018 idadi ya wanawake mawaziri ulimwenguni ilifikia upeo wa juu zaidi kuliko wakati mwingine ule kwa 20.7% (812 kati ya 3922).

Katika mataifa ya Afrika chini ya Jangwa la Sahara, idadi ya wabunge wa kike iliongezeka mwaka wa 2018, kwa mgao wastani wa kieneo wa 23.7% kulingana na toleo la hivi karibuni la Chapisho la 2019 la Umoja wa Mabunge [Inter-Parliamentary Union (IPU)]  Map of Women in Politics.

IPU, inajumuisha zaidi ya mabunge ya kitaifa 170 kutoka kote ulimwenguni, huchunguza idadi ya wanawake waliochaguliwa kujiunga na mabunge ya kimataifa kila mwaka na hutoa uchanganuzi unaosaidia kuchunguza maendeleo, changamoto na mienendo.

Jibouti, ambayo haikuwa na mwanamke yeyote katika bunge mwaka wa 2000, ilishuhudia ongezeko kubwa katika nchi za mabunge ya chini na bunge moja kimataifa. Mgao wa wanawake katika bunge uliimarika mwaka 2018 kutoka 10.8% hadi 26.2% (ongezeko la 15.4%), jumla ya wanawake 15, inaeleza ripoti, ambayo iliidhinishwa wakati wa Tume kuhusu Hali ya Wanawake (CSW) katika makao makuu ya Umoja wa Mataifa, New York, Machi 2019. 

Uhabeshi ilishuhudia ongezeko kubwa la uwakilishi wa wanawake kisiasa katika serikali, kutoka 10% ya wanawake mawaziri 2017 hadi 47.6% 2019.

Kuhusu nafasi za uwaziri, ripoti hiyo inabainisha ongezeko jingine la kushangaza — wanawake zaidi barani Afrika wanasimamia wizara ambazo kwa kawaida zilishikiliwa na wanaume kuliko 2017. Kuna zaidi ya 30% ya wanawake mawaziri wa usalama (17 kimataifa), zaidi ya 52.9% ya wanawake mawaziri wa fedha, na zaidi ya 13.6% ya wanawake mawaziri wa masuala ya nje (30).

Utaratibu wa kawida umekuwa kuwachagua wanawake kusimamia wizara za masuala mepesi hasa ya kijamii, watoto na familia.

 

“Bado tuna barabara yenye miinuko mbele, lakini idadi inayoongezeka ya wanawake mawaziri inatia moyo, hasa tunaposhuhudia ongezeko la idadi ya mataifa yaliyo na usawa wa kijinsia katika mabaraza ya mawaziri,” alisema Phumzile Mlambo-Ngcuka, Mkurugenzi Mtendaji wa Masuala ya Wanawake wa Umoja wa Mataifa wakati wa kuidhinishwa kwa ripoti hiyo. Alizihimiza nchi kuchukua hatua za ujasiri ili kuongeza uwakilishi wa wanawake katika kufanya maamuzi.

“Wanawake zaidi katika siasa huwezesha maamuzi jumuishi zaidi na hii huweza kubadilisha namna watu wanavyomwona kiongozi,” aliongeza Bi. Mlambo-Ngcuka, ambaye alikuwa waziri na Naibu wa Rais nchini Afrika Kusini.

Kati ya mataifa ya Afrika yenye asilimia kubwa ya wanawake katika nafasi za uwaziri  ni pamoja na Rwanda (51.9%), Afrika Kusini (48.6%), Uhabeshi (47.6%), Ushelisheli (45.5%), Uganda (36.7%) na Mali (34.4%).

Asilimia ya chini kabisa Afrika ni Moroko (5.6%), ambayo ilikuwa na waziri mwanamke mmoja pekee katika baraza la mawaziri 18. Mataifa mengine yaliyo na chini ya 10% ya mawaziri wanawake ni Nijeria (8%), Morisi (Mauritius) (8.7%) na Sudan (9.5%).

Rwanda, taifa la linaloongoza katika idadi ya wanawake bungeni, lilishuhudia upungufu mdogo wa idadi yao, kutoka 64% mwaka wa 2017 hadi 61.3% mwaka wa 2018. Mataifa mengine yaliyo na asilimia kubwa ya wanawake wabunge kulingana na ripoti hiyo ni Namibia (46.2%), Afrika Kusini (42.7%) na Senegali (41.8%).

Mataifa ambayo yametimiza 30% yanaonekana kuchukua hatua za hiari kuhakikisha usawa wa kijinsia. Kwa mfano, Rwanda ina vipengele vya kikatiba vinavyowatengea wanawake 30% ya viti vya mabunge yake mawili ilhali Sheria ya utawala wa Manispaa ya Afrika Kusini ya 1998 inavihitaji vyama vya kisiasa “kuhakikisha 50% ya wagombeaji katika orodha ya vyama ni wanawake” na kwamba “wanawake wamewakilishwa kwa usawa katika kamati za wadi.” Ingawaje hakuna adhabu ya kutotimiza hitaji hilo Afrika Kusini, chama tawala cha African National Congress (ANC) huwatengea wanawake 50% ya viti vya bunge.

Kulingana na Wanawake wa Umoja wa Mataiafa (UN Women), vikwazo viwili vikuu huwazuia wanawake kushiriki kikamilifu katika maisha ya kisiasa. Hivi ni vikwazo vya kimuundo, ambapo sheria baguzi na taasisi bado zinabana uwezo wa wanawake kugombea nafasi, na mianya ya kiuwezo, ambayo hutokea wakati wanawake kuliko wanaume hukosa elimu, mahusiano na raslimali zihitajikazo kuwa viongozi bora.

Huku nchi zikijizatiti kutimiza lengo la 5 la Malengo ya Maendeleo Endelevu, “Kutimiza usawa wa kijinsia na kuwawezesha wanawake wote na wasichana,” ni lazima pia serikali zijizatiti  kushirikisha usawa wa kijinsia katika katiba na katika mifumo ya kisheria. Zinastahili kuhakikisha sheria inatiiwa kikamilifu, kuondoa aina zote za vurugu dhidi ya wanawake na kuhakikisha wasichana wanapata elimu bora.

Mada: