Eneo la Soko Huru Afrika: Safari Yaanza

Get monthly
e-newsletter

Eneo la Soko Huru Afrika: Safari Yaanza

— Vera Songwe
Christabel Ligami
Afrika Upya: 
7 August 2019
Vera Songwe, Executive Secretary, United Nations Economic Commission for Africa
Vera Songwe, Katibu Mtendaji, Kamisheni ya Uchumi ya Afrika ya Umoja wa Mataifa.

Mnamo tarehe  21 Machi, 2018 mataifa ya Afrika yalitia saini mkataba wa makubaliano ya Eneo Huru la Biashara la Afrika (AfCFTA) jijini Kigali Rwanda. Kufikia tarehe 29 Aprili, 2019, zaidi ya mwaka mmoja baadaye, mataifa 22 (idadi inayohitajika kwa mkabaka kuidhinishwa) yalikuwa yamewasilisha mikataba yao ili iidhinishwe. Kwa soko la pamoja la zaidi ya watu bilioni 1.2 na Pato la Taifa la trilioni $2.5 AfCFTA inaweza kuifanya Afrika iwe na eneo huru la biashara kote duniani.  Msaada wa Umoja wa Mataifa kwa Umoja wa Afrika wakati wa mazungumzo na kuidhinisha uliongozwa na Vera Songwe, Katibu Mtendaji wa Kamisheni ya Uchumi ya Afrika ya Umoja wa Mataifa (ECA). Kwa mujibu wa Africa Renewal, Christabel Ligami alimhoji Bi. Songwe kuhusu hatua ya utekelezaji wa AfCFTA, kuwawezesha wanawake wa Afrika na ruwaza yake kwa ECA. Ifuatayo ni sehemu ndogo ya mahojiano hayo.

Africa Renewal: Kwa kuwa sasa AfCFTA imezinduliwa, je unafikiri mataifa yatatekeleza makubaliano katika muda uliowekwa?

Vera Songwe: Ni jambo zuri kwamba mataifa mengine yanasonga mbele. Inaonyesha jinsi biashara ilivyo muhimu kwa mataifa ya Afrika na kwamba mataifa yako tayari kufungua mipaka yao. Kwa hivyo, ndio, tunatarajia mataifa yatatimiza makubaliano hayo kikamilifu. Mataifa yanafahamu yanahitaji kufanya biashara zaidi na wengine ili kuongeza mapato na kuunda ajira, haswa kwa vijana. Biashara ya ndani kwa ndani barani Afrika inatarajiwa kuongezeka hadi asilimia 53.3, kumaanisha kwamba mapato yataongezeka.

Je, mataifa wanachama yanawezaje kuhakikisha kuwa makubaliano yametekelezwa kikamilifu?

Mawaziri wa fedha wa mataifa wanachama wanaotia saini AfCFTA wana jukumu muhimu la kusaidia mataifa kutekeleza makubaliano hayo. Mawaziri hawa wanaelewa kuwa ushuru na forodha, kwa mfano, ambazo ni sehemu muhimu ya AfCFTA, ni masuala yaliyo chini ya wizara ya fedha. Ni wajibu wa mawaziri wa fedha kutathmini ikiwa, vipi na lini mapato yataongezeka kwa mataifa yao na jinsi mapato hayo yatakavyotumika. Mataifa yakishaidhinisha waraka huu, yana miaka 10 na mengine miaka 13, kubuni sera muhimu ili kunufaika kwa AfCFTA kikamilifu.

Tunatarajia mataifa kuhakiki sera zao za kiuchumi, yakizingatia sera za kifedha ambazo zinafaa kwa malengo yao, na kutusaidia sio tu kuzizoea, na kufaidika zaidi kwa AfCFTA, lakini kwa upana zaidi kufikia Agenda 2063 na Ajenda ya 2030  ya Maendeleo Endelevu. Hatua ya haraka ni kuunda nafasi ya kuwezesha kifedha kukuza uwekezaji wa umma na wa kibinafsi huku yakizingatia uwekezaji katika sekta tofauti za uchumi.

Baadhi ya mazungumzo bado hayajakamilika. Je, kuna masuala tata ambayo mataifa bado hayajakubaliana kuyahusu?

Masuala yaliyobaki ya majadiliano ni mambo yanayohusu ushindani, vifungu vinavyohusiana na uwekezaji, hakimiliki, bishara katika mtandao na kadhalika. Mataifa yalikubali kuchukua muda zaidi kujadili masuala hayo. Masuala hayo yanajadiliwa na yatakamilika katika awamu ya pili ya mazungumzo. Mchakato huu huwa hivi hata kwa mikataba mingine ya biashara ya kimataifa. Mazungumzo huwa hayakamiliki mara moja; majadiliano kuhusu masuala ya biashara ni mapana na huchukua muda kukamilika. Tunataka kuzuia hali ambayo AfCFTA inayafungulia mataifa mashindano yasiyofaa. Afrika inazidi kusonga mbele katika teknolojia, ndio maana tayari tunazungumzia biashara ya katika mtandao. Hii ni muhimu sana kwa mataifa ambayo yameendelea sana katika teknolojia. Kwa yale ambayo hayajaendelea sana katika teknolojia, tunahakikisha yameeleza vizuri masuala yanayohusu biashara katika mtandao.

Umoja wa Afrika na mawaziri wa biashara wa Afrika, baada ya kukamilisha sheria kadhaa, walizindua rasmi awamu ya utekelezaji wa AfCFTA  wakati wa mkutano wa kipekee wa marais na wakuu wa serikali mnamo tarehe 7 Julai 2019.

Biashara ya kidijitali Afrika inakua kwa kiwango kinachokaridiriwa kuwa asimilia 40. Je, ni ushauri gani unaoweza kuyapa mataifa yanayofanya chumi zao kuwa za kidijitali?

Programu za kidijitali zikitumika kikamilifu, zinasaidia kuziba mapengo ya kifedha, kuwawezesha wanawake kuwa wajasiriamali, kutoa data halisi za soko kwa wakulima walio mashambani na vijijini pamoja na uchanganuzi wa data zinazohusu habari za hali ya hewa. Faida ya matumizi ya dijitali ni kuwa inaweza kugeuza uchumi kwa kupunguza vizuizi vya kiingilio na kupanua uafikiaji wa soko kwa biashara, kuunda kazi na kuinua biashara ya nje ya bidhaa na huduma. Pia kuna fursa kwa mataifa ya Afrika kunufaika kwa maendeleo haya ili kufaidi utoaji wa huduma za umma, ikiwemo ufanisi na uafikiaji wa maeneo salama, elimu na afya.

Tayari mataifa mengine yanakubali hatua kwa hatua matumizi ya mitambo ya dijitali katika sera za ushuru na matumizi ya fedha, usimamizi wa fedha za umma na utoaji wa huduma za umma. Ununuzi na mauzo ya kidijitali yana uwezo wa kupunguza ufujaji wa fedha za umma na kuboresha ukusanyaji wa ushuru kwa mabilioni ya dola. Hiyo ni fedha ambayo inaweza kuziba pengo kubwa katika mahitaji ya fedha za kila mwaka barani Afrika.

Je,  ruwaza yako kwa ECA ni nini?

Wazo langu ni kuona ECA ikitoa mawazo ya kubadilisha bara hili na kuunda hali za kukua kwa uchumi na ustawi wa watu. Tunataka kuwa akiba ya mawazo ya Afrika, kupitia vitendo na  matokeo.

Je,  utatumia mkakati ipi kuona kwamba haya yanatendeka?

Nitaimarisha uwezo wa wafanyakazi na kuongeza idadi yao ili kusaidia mataifa kuzingatia ukarabati wa chumi zao na kuongeza ukuaji. Ninakusudia kufanya kazi kwa karibu zaidi na sekta ya kibinafsi, kuwajumuisha katika majadiliano yetu na ushauri.

Nitazingatia zaidi masuala ya kikanda yanayovuka mipaka kama vile uendelevu wa maji, na masuala ya kisiasa kama vile mzozo kati ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kiarabu ya Sahrawi na Moroko. Nitatetea Afrika duniani kote kuhusu ushuru, uhamiaji, mabadiliko ya hali ya hewa, amani, usalama na biashara.

Ninabadilisha mfumo wa ECA kwa kuanzisha vitengo maalumu kuhusu masuala kadhaa. Sasa tunayo sekta ya kibinafsi, uchumi mdogo na fedha na vitengo vya kupunguza umaskini.

Je, mpango wako kwa wanawake ni upi?

Licha ya tafiti anuwai kugundua kuwa wanawake ni msingi wa ukuaji wa uchumi wa taifa au eneo lolote, wanawake wa Kiafrika bado  wana uwakilishi mdogo katika sekta nyingi, ikiwemo ile ya teknolojia. Kuanzia kenye ECA, nilipanga kulinganisha idadi ya wafanyakazi wanaume na wanawake waliohitimu kwa usawa. Ninakusudia kutafuta maoni ya wanawake katika kuunda mapendekezo ya sera. Uchunguzi wetu umegundua kuwa ni wanawake wachache sana wanaohusika katika majadiliano ya sera na maamuzi. Sasa tunashughulikia Hazina ya Ujasiriamali ya Wanawake itakayowawezesha wanawake kiuchumi.

Je, utatafutiaje ECA rasilimali?

Tunakusudia kutafuta rasilimali kutoka washirika wa jadi na kujenga ushirikiano mpya na sekta ya kibinafsi. Pia, tutaongeza ushiriki wetu na mashirika yasiyokuwa ya kiserikali. Tunatumaini kushirikiana na vyuo vikuu na taasisi zingine ili kupata maoni yao ambayo ni muhimu, utafiti na masuala mengine.