Mauaji ya halaiki hutendeka demokrasia inapokosekana

Get monthly
e-newsletter

Mauaji ya halaiki hutendeka demokrasia inapokosekana

—Tali Nates, Mkurugenzi Mkuu wa Kituo cha Johannesburg cha Mauaji na Mauaji ya Halaiki
Kingsley Ighobor
Afrika Upya: 
22 October 2020
Holocaust na Kituo cha Mauaji ya Kimbari
JHGC, Johannesburg
Holocaust na Kituo cha Mauaji ya Kimbari huangaza juu ya mauaji na mauaji ya halaiki nchini Rwanda.

Tali Nates alianzisha Kituo cha Johannesburg cha Mauaji na Mauaji ya Halaiki (JHGC) mwaka wa 2008 kuendeleza uelewa wa historia ya mauaji ya halaiki yaliyotokea kati ya 1939 na 1945 na mauaji ya halaiki ya 1994 dhidhi ya Watutsi nchini Rwanda wakati ambapo Wahutu na wengine waliopinga mauaji ya halaiki pia waliuawa. Kwa lengo la kuzuia kutokea tena kwa ukiukaji mkubwa wa haki za binadamu, Bi. Nates amepeleka utetezi wake kwa mataifa kadhaa ya Afrika na zaidi. Alizungumza na Kingsley Ighobor wa Africa Upya kuhusu kazi ya JHGC, ushirikiano wa Umoja wa Mataifa, na kuhusu kwa nini Waafrika wanalazimika kuimarisha na kulinda demokrasia. Hizi hapa dondoo kutoka kwa mahojiano hayo:

Tali Nates, Executive Director of the Johannesburg Holocaust and Genocide Centre
Tali Nates, Mkurugenzi Mkuu wa Kituo cha Johannesburg cha Mauaji na Mauaji ya Halaiki

Je, nini ilikupa motisha ya kuanzisha Kituo cha Johannesburg cha Mauaji na Mauaji ya Halaiki?

Maono ya kufungua kituo cha elimu, kumbukumbu, na mafunzo kwa binadamu yalianza miaka 12 iliyopita. Ndoto yangu ilikuwa kuunganisha historia na ulimwengu wa leo. Mimi ni binti wa manusura wa janga la mauaji. Baba yangu [Moses Turner] alinusurika kambi nne za mateso; aliokolewa na Oskar Schindler [Schindler alikuwa mfanyabiashara wa Kijerumani ambaye aliokoa Wayahudi wapatao 1,200]. Nilikua nikisikiliza hadithi za Janga la Mauaji. Nilikua na sauti ya baba yangu ya kusema, "Watu, serikali na jamii zina chaguo ambazo lazima zifanye; tunahitaji kujifunza kutoka kwa historia.'' Alifariki nikiwa ningali mchanga lakini nimebeba ujumbe wake. Nilisomea historia, nilifundisha katika chuo kikuu na nilifanya kazi na mashirika yasiyo na kiserikali [NGOs].  

Je, jiji la Johannesburg lilikujaje katika taswira yako?

Jiji la Johannesburg lilishirikiana nasi mnamo 2010 na liligeuza ndoto yangu kuwa hali halisi. Nilitaka kituo cha mauaji ya halaiki nchini Afrika Kusini kwa sababu nchi hii bado inapambana na historia ngumu na chungu ya kukandamizwa na ukoloni. Ubaguzi wa rangi bado ni tatizo hapa. Ni kiingilio cha historia zingine za mateso, ya kukandamizwa, au mapambano ambayo yamefanyika au yanafanyika katika maeneo ya mbali—kote ulimwenguni. Kutoka kiingilio hicho mtu anaweza kujifunza kuhusu, kwa mfano, historia ya mauaji ya halaiki ya 1994 nchini Rwanda.

Kujifunza kuhusu ukandamizaji wa zamani wa haki za binadamu ni muhimu ili ukandamizaji huo uepukwe katika siku zijazo. Je, unaelezaje chuki kwa wageni iliyoendelezwa na watu wengine nchini Afrika Kusini?

Ukichunguza mauaji ya halaiki barani Uropa, kati ya 1939 na 1945, ambayo tunayaita janga la mauaji ya Wayahudi, unajifunza kuhusu  hatua za mauaji ya halaiki zinazojumuisha udhalilishaji, ubaguzi, ukatili na unyama na unajifunza kuhusu matokeo ya sheria mbovu, au propaganda za serikali ya kiimla, ambayo hufanyika demokrasia inapofeli.

Unaweza kujifunza mafunzo kutoka kwa historia ya mauaji ya halaiki dhidi ya Watutsi nchini Rwanda, au ya ukoloni. Unaweza sasa kuunganisha historia hiyo na hali halisi ya leo. Kwa hivyo, tunajaribu kuunda uelewa wa kutuzuia kuwa watazamaji tu. Badala yake, lazima tuwe wakereketwa wa mageuzi ya kijamii.

Je, unaleta athari gani na shughuli zako za uhamasishaji?

Kabla ya janga la COVID-19, maelfu ya watu, wakiwemo wanafunzi, walizuru Kituo cha Johannesburg cha Mauaji na Mauaji ya Halaiki. Shule zilikuwa zikileta wanafunzi wao na walimu kila siku  kwa maonyesho, majadiliano, makongamano, na michezo na sinema.

Watu wanapozuru Kituo hiki, wanahisi wako katika nafasi salama ya kuwasilisha masuala ya haki za binadamu, masuala yanayohusu, kwa mfano, watu wenye ulemavu, hususan Afrika Kusini.  Tulipata janga miaka michache iliyopita wakati wagonjwa wa akili 144 walifariki katika kituo chetu [Afrika Kusini]. Hilo lilikuwa janga kuu. Tulifanya nini? Tuliunda nafasi salama kwa familia za watu 144 kukumbuka wapendwa wao, kujifunza kuhusu haki za watu wenye ulemavu na kuungana na historia kuhusu kile kilichotokea kwa watu wenye ulemavu nchini Ujerumani wakati wa vita vya Nazi—jinsi walivyolengwa, kudhulumiwa na kuuawa. Zaidi ya watu 200,000 waliuawa na Nazi.

Je, unawezaje kufanya kazi katikati ya janga?

Afrika Kusini ilifanya mfungo mkali mnamo Machi 26 kwa wiki tano. Kituo chetu kilifungwa mara moja kwa umma. Tumehamia kwenye ulimwengu wa dijitali. Tunaandaa webinar kila wiki ambazo zinavutia jamii mbalimbali kutoka ulimwenguni kote lakini pia kutoka Afrika Kusini. Tunatoa mafundisho mtandaoni kupitia Zoom, Google au Microsoft Teams, au njia zingine. Watu wengi hawafikii mtandao nchini Afrika Kusini. Kwa hivyo, tunarekodi maelezo ya sauti, hadithi fupi—dakika tatu, dakika mbili—na kuzituma kwenye WhatsApp kwa wanafunzi katika shule zaidi ya 200 nchini. Tunatumia podcast kuzungumzia wakimbizi, chuki kwa wageni, watoto walio hatarini, unyanyasaji wa kijinsia na mambo mengine.

Tunataka wale wanaohusika na mafunzo yetu waelewe kuwa hawawezi kuwa watazamaji tu, kwamba kuna matatizo katika jamii zetu ambayo yanatuhitaji sote kusimama na kufanya kitu. Kwa mfano, ingawa sisi ni makavazi, kwa sababu watu wana njaa kwa sasa, tulifungua kituo chetu kukusanya chakula na vifaa vingine kwa usambazaji kwa wale wanaohitaji. 

Dhuluma mara nyingi hutokana na hamu ya wengine kutaka kulinda vitambulisho fulani—dini, rangi, kabila, na kadhalika. Je, unaona hitilafu fulani barani Afrika leo?

Katika bara letu pendwa tunaona mivutano inayokua kuhusu na dini na lugha. Tunaona hitilafu nyingi kuhusu maoni ya kisiasa, utambulisho wa kikabila na jinsia—unyanyasaji wa kijinsia unaongezeka kutokana na mfungo huu. Sisi sote lazima tuchukue jukumu la kulinda maadili ya Afrika ya ubuntu, amani na uvumilivu.

Tunafanya kazi na vituo wenza huko Cape Town na Durban, na washirika wetu kwenye Makumbusho ya Mauaji ya Halaiki jijini Kigali [Rwanda]—kukuza maadili haya kote Afrika. Tuna programu ya uongozi wa vijana inayoitwa Programu ya Wanamageuzi wa Uongozi katika nchi nyingi, ambayo inakusudia kuimarisha vijana wetu kusimama dhidi ya itikadi kali na matatizo mengine tuliyotambua. Tunawafundisha viongozi wa vijana na tunawapa mafunzo pia wakufunzi kama vile waalimu, wawezeshaji, maprofesa, wakutubu, na wengine, kufundisha maadili yetu shuleni.

Tulifanya kazi, kwa mfano, huko Yola, Nijeria, kaskazini mashariki, na UNESCO [Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni] na Chuo Kikuu cha Kimarekani cha Nijeria kutoa mafunzo kwa wawezeshaji kutazama mifano maadili, kwa historia yetu ngumu barani Afrika na Nijeria, na kujifunza mafundisho ili wasirudie makosa ambayo yalifanywa.

Je, unawalenga watu wanaosababisha matatizo katika nchi?

Kama Shirika la kielimu na lisilo la kisiasa, hatuwezi kuwafikia wadau muhimu kama wanasiasa na wale ambao tayari wana itikadi kali. Lakini tunafanya kazi na watu ambao walitoroka kutoka makundi ya waasi. Kwa mfano, huko Yola, Nijeria, tulifanya kazi na wasichana wengine ambao waliachiliwa kutoka kwa utumwa wa Boko Haram mnamo 2018. Katika maeneo mengine, tulifanya kazi na askari watoto wa zamani ambao wanahitaji kurekebishwa tabia.

Je, munashirikiana na serikali au taasisi za Afrika kama vile Umoja wa Afrika?

Hakika! Hatupaswi kujaribu kufanya kazi peke yetu. Katika kila nchi, tunafanya kazi na washirika tofauti. Huko Gambia, kwa mfano, tulifanya kazi na Wizara ya Elimu. Huko Msumbiji, tulikuwa na bahati ya kushirikiana na Wizara ya Vijana na Michezo. Huko Mauritius, tulifanya kazi na wizara inayowajibikia na watoto. Tunafanya kazi na mashirika ya kimataifa na ya bara. Kwa mfano, tunafanya kazi na Aegis Trust [ambayo inafanya kazi kuzuia mauaji ya halaki] nchini Rwanda na katika Jamhuri ya Afrika ya Kati, Sudan, Sudani Kusini, Kenya, na kadhalika.

Je, munashirikiana na Umoja wa Mataifa pia?

Ndiyo. Tunashirikiana na Kituo cha Habari cha Umoja wa Mataifa huko Pretoria [Afrika Kusini] kwenye hafla za makumbusho na miradi ya usambazaji wa habari. Na uhusiano ni mzuri. Tunafanya kazi pia na makao makuu ya Umoja wa Mataifa huko New York na kwa ofisi tofauti za Umoja wa Mataifa barani Afrika—kwa mfano huko Dakar. Tunafanya kazi pia katika miradi tofauti na UNESCO na mashirika mengine ya Umoja wa Mataifa.

Sheria za kimataifa kama vile Mkataba wa Adhabu ya Jinai ya Mauaji ya halaiki na Azimio la Kimataifa la Haki za Binadamu zimesaidia vipi utetezi wako?

Hizi ni sheria muhimu sana, kama kama vile Wajibu wa Kulinda. Pia tunayo Siku ya Kimataifa ya Kuadhimisha kumbukumbu ya Waathirika wa janga la mauaji, inayoadhimishwa tarehe 27 Januari kila mwaka na ni siku muhimu sana kufundisha na kujifunza mafunzo kutoka historia.

Je, maoni yako ni gani kuhusu maandamano ya Matukio ya Umuhimu wa Maisha ya watu weusi huko Marekani na sehemu zingine za ulimwengu?

Taasisi yetu ilitoa taarifa ya kuunga mkono Matukio ya Maisha ya watu weusi. Ingawa huu ni wakati wa kusema kuwa maisha ya watu weusi ni muhimu, jambo hili limechelewa kwa mamia ya miaka. Lazima tutafakari sana jinsi ya kuondoa ubaguzi wa kimfumo nchini Marekani na ulimwenguni kote.

Je, una ujumbe gani kwa nchi ambazo zina migogoro au pale ambapo demokrasia inaweza kuwa dhaifu?

Ikiwa tunajifunza chochote kutoka kwa mauaji ya halaiki—tafadhali, nchi za Afrika, sikilizeni hili: mauaji ya halaiki hayatokei katika demokrasia. Kamwe hayatokei! Mauaji ya halaiki hufanyika wakati demokrasia imefeli au inatishiwa.  Hutokea katika serikali za kiimla au za kimabavu, ambazo hutumia vibaya sheria za seriakali na kutumia propaganda, hofu, ugaidi, na kila kitu kingine kulenga watu wachache. Ujumbe wangu ni, linda na kustawisha demokrasia yako.

Ili kufahamu zaudi kuhusu Kituo cha Janga la Mauaji na Mauajia ya Halaiki,  Johannesburg, bonyeza hapa.