Guterres apongeza matokeo ya mkutano uliofanyika Angola kuhusu amani na usalama DRC

Get monthly
e-newsletter

Guterres apongeza matokeo ya mkutano uliofanyika Angola kuhusu amani na usalama DRC

UN News
Afrika Upya: 
28 Novemba 2022
Na: 
MONUSCO/Sylvain Liechti
Askari ya kijeshi wa MONUSCO wakijificha kwenye kilima cha Munigi wakati wa shambulio la FARDC dhidi ya maeneo ya M23 huko Kanyaruchinya karibu na Goma, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amekaribisha matokeo ya mkutano wa viongozi kuhusu amani na usalama mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC, mkutano uliofanyika Luanda Angola tarehe 23 mwezi huu wa Novemba kwa mwaliko wa Rais wa taifa hilo João Lourenço.

Taarifa iliyotolewa Ijumaa tarehe 25 Novemba na Naibu Msemaji wa Umoja wa Mataifa, Farhan Haq, imemnukuu Katibu Mkuu akikaribisha pia uamuzi uliotokana na mkutano huo ambao ni kuweko kwa sitisho la mapigano na wakati huo huo waasi wa M23 kuondoka mara moja maeneo ambayo wanashikilia.

Mkutano huo ulioitishwa na Rais Lourenço wa Angola, ulihudhuriwa na Rais Evariste Ndayishimiye, Rais wa Burundi na mwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, EAC, Rais Felix-Antoine Tchisekedi Tshilombo, wa DRC, Vincent Biruta, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Rwanda akimwakilisha Rais Paul Kagame na Rais wa zamani wa Kenya, Uhuru Kenyatta ambaye ni Msuluhishi aliyeteuliwa na EAC kwenye mchakato wa amani DRC.

FARDC na waasi wekeni silaha chini

Katibu Mkuu ameongeza sauti yake kwa wale waliotia saini taarifa ya pamoja ya mkutano huo na kutoa wito kwa jeshi la DRC na vikundi vya kigeni vilivyojihami kuweka silaha zao chini na kuanza mara moja mchakato wa kusalimisha silaha, kuvunja makundi, kujumuika kwenye jamii na kurejea makwao vile inavyoonekana inafaa.

Kama ilivyoombwa na watiaji saini kwenye taarifa hiyo ya pamoja, Katibu Mkuu amesisitiza uwepo wa ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini DRC, MONUSCO katika kusaidia utekelezaji wa makubaliano hayo kwa mujibu wa mamlaka yake na utayari wa kuratibu na jeshi la kikanda la Jumuiya ya Afrika MAshariki, EAC ili kutoa usaidizi wa haraka wa mfumo wa uthibitishaji utakaondwa kwa mujibu wa Mpango wa Luanda na wakati huo huo kuendelea kusaidia mchakato wa Nairobi kuhusu amani na usalama DRC.

Katibu Mkuu pia amesisitiza uwepo wa Umoja wa Mataifa katika kusaidia kurejea makwao kwa wakimbizi wa ndani kwa uratibu na mamlaka husika chini ya mifumo iliyoko, na sambamba na sheria na kanuni za kibinadamu za kimataifa.